Saturday, November 30, 2013

KUNA VICHAA WA FEDHA...


 

HABARI nimesikia, kuwa wa fedha vichaa,

Wameishajilimbikia, eti sasa wazimwaa,

Kusudi na yao nia, hakuna anayejua,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Kwa wingi zilivyojaa, kila mtu agawiwa,

Hakuna wa kuchagua, wote kwao abiria,

Lengo sijalitambua, nabakia kushangaa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Punda ingelikuwa, ngejuwa wamelemewa,

Mwenye punda achezewa, na dhihaka kufanyiwa,

Mtoni akajitia, chumvi  maji kwenda kuwa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Na wanaokusudiwa, kura wanaoshikilia,

Vyamani walimokuwa, waziwazi ni bidhaa,

Bei imeshaamuliwa, taslimu wanatoa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Karuni ninayemjua, japo wingi ulimzidia,

Bure kitu hakutoa, hadi alipofukiwa,

Hawa sijawaelewa, gia gani watumia?

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Nyumbani wazichukua, ugenini kufukia,

Kisha wanajichengua, na mikwara kujitia,

Ukiona yaelea, juwa wameazimia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Matofali wachukua, dhahabu yaliyokuwa,

Kaziye si kujengea, ila kuji9nyeshea,

Ukubwa uliokuwa, hasara kwenye dunia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Wanywa hadi kujinywea, ibilisi kakolea,

Hio waalofurahia, Mola hajafurahia,

Kicheko kilichokuwa, kilio kakitohoa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Milma waelemea, bondeni kulikouwa,

Huku juu umejaa, chini wazidi kupyway,

Na bado twatarajia,  kisiwa tutabakia ?

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Kama pombe ingekuwa, sababu ningeijua,

Wataka watu kulewa, ovyo wakajisemea,

Kisha lao wakalitwaa, pasina wao kujua,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Keki ingelikuwa, kwenye basi imekuwa,

Kisha dawa imetiwa, shabaha ningegundua,

Wanuia abiria, kwenda mbele waibia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Mimi hili sijajua, la tajiri kuwa na njaa,

Ikawa yamelvyaa, hadi chini twamzoa,

Kuna kitu sijajua, bado nakiangalia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Si wa bure ukichaa, ovyoovyo kuzigawa,

Kuna sababu na nia, ila sijaigundua,

Kofia nitaivua, kija mtu kunambia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Semeni Watanzania, haya mnayoyajua,

Vimbgwanga vyakaribia, mengi tutashuhdia,

Watu nguo watavua, sapoti kwenda kutoa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Ni wakati wa maridhia, watu kuyafikiria,

Akili wakatumiwa, si kwa moyo kuzainiwa,

Kisha wakaja kuyajutia, siku wasioitambua,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !