Monday, April 29, 2013
Sunday, April 21, 2013
Nyumba isiyo na haki
Nyumba ikosayo haki, baba huwa mnafiki,
Limbwata ikimwashiki, ya wana hatoafiki,
Akaachia mikiki, rabsha na taharuki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Biblia hutaliki, na Daudi hasemeki,
Qurani haifunguki, ya Selemani kucheki,
Akili zao riziki, na kisha umamuluki,
Nyumba isiyo na haki, maisha haijengeki!
Wangeata unafiki, mistari ina haki,
Wasingejaribu hiki, hofu ingetamalaki,
Ujinga wauafiki, dunia haisomeki,
Nyumba isiyo na haki, milele haisimamiki!
Nyumba ikosayo haki, baba huwa mnafiki,
Limbwata ikimwashiki, ya wana hatoafiki,
Akaachia mikiki, rabsha na taharuki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Nuru haimpeleki, na aendako haafiki,
Katikati huafiki, akakwaza ushtaki,
Akawa haaminiki, na leke halithaminiki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Huzaa huambiliki, na mkubwa unafiki,
Ya usawa na ya haki, yawe kwake
hayasikiki,
Wakasepa washtaki, yawe hayaeleweki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Ya haki akataliki, na kuikwaza milki,
Baraka ikahamaki, na hekima kuishtaki,
Ukazuka umamluki, pia nao uzandiki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Nyumba isiyo na haki, wevi wataibariki,
La kweli halitamkwi, na uongo huafiki,
Wema ukawa kisiki, waovu hawautaki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Umma huudhhaki, yeye ndio mwenye haki,
Kusema wasidiriki, wanaihofia dhiki,
Ila wakitaharuki, nao huja kuhamaki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Huukataa uzandiki, na kubwaga unafiki,
Wakaililia haki, kila kona kutamalaki,
Ukaisha umamluki, kwa kumhofu Maliki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Nyumba yetu ibariki, ewe bwana mtoa haki,
Hakikisha hawafiki, wote wenye unafiki,
Kiwatibue kisiki, wawe juu hawaamki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina amani!
Huzaa huambiliki, na mkubwa unafiki,
Ya usawa na ya haki, yawe kwake
hayasikiki,
Wakasepa washtaki, yawe hayaeleweki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Madaraka
huwanoki, injini haziamki,
Ya mwana hawashtuki, ila yao huhamaki,
Usanaa huulaki, sera wakaiafiki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina amani!
Umma huudhhaki, yeye ndio mwenye haki,
Kusema wasidiriki, wanaihofia dhiki,
Ila wakitaharuki, nao huja kuhamaki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Tuesday, April 9, 2013
SHETANI WA NA MIMI NICHINJE !
Shetani wa na mimi nichinje
ASILI tunaijua, itokako Tanzania,
Mababu waliamua, nani wa kutuchinjia,
Mwaikana historia, na utu kuuchezea?
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Tuliungana jamii, nasara na islamiya,
Ndugu tukawaachia, kazi ya kutuchinjia,
Mbegu tukiitambua, Ibrahimu kuanzia,
Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na
alegee!
Yaliyoishaamuliwa, vipi twaja yafukua,
Makaburi kuyazua, walo hai kuwatia,
Au mnalololijua, sisi bado kulijua?
Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na
alegee!
Yapo ya kuzungumzia, nchi ikaendelea,
Barabara zatakiwa, vijijini kuingia,
Na madaraja kuzua, watu wakajivukia,
Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na
alegee!
Mashamba yanatakiwa, kulima kulisha
Tanzania,
Na kiasi kuongezea, dunia kuiuzia,
Kuchinja twapigania, hivi kweli twajijua?
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Hivi kweli twajijua, kwa tunayojisemea,
Au wehu watuingia, ya ovyo kujiamlia,
Dunia kutushangaa, mfano tuliokuwa?
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Mengi tungelifikiria, ubora kujiongezea,
Afrika kutambua, ni darasa tumekua,
Sisi tukatangulia, na wengine kufatia,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Ya wa Kongo twaamua, sasa kwenda kurejea,
Kwanza tungejichungua, kama wazima raia,
Au tumeingiliwa, na walio ni vichaa,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Burma ukiangalia, kichaa kajizukia,
Ndugu anawachukia, na uadui kuwatia,
Hivi sasa awaua, na nyumba kuwaunguzia,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Iraqi na Syria, dini zinahujumiwa,
Wauana raia, kwa hata wasiyojua,
Ni vichaa wamekuwa, nchi zinateketea,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Amiri anatakiwa, katikati akakaa,
Mstari kuutia, hakuna wa kuuchezea,
Maaamuzi yatakiwa, sio lawama kutoa,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Maji yanatusumbua, lazima kujivunia,
Majumbani kuingia, na mashambani kumwaa,
Kuchinja wito likiwa, naona tunafulia,
Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na
alegee!
Kongo wanatungojea, kwenda kuwahubiria,
Nchi ya kati nayo pia, uamsho yangojea,
Kimataifa tukiwa, thumni hatutapigania,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Masoko kujitafutia, nyie mngetangulia,
Wafuasi kufatia, sadaka wakajipatia,
Michango yao ikawa, na nchi kwenda chanua,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Nchi ninaiombea, kuvuka hii balaa,
Kwa uongo kukataa, na ukweli kulilia,
Salama ya Tanzania, sote yatutegemea,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
ISIWE MIAKA HII NUHUSI !!!
Wakuu twawaambia, juu walioshikilia,
Macho yao kufungua, kujua kinachoendelea,
Wapunguze kusinzia, hali watu wauawa,
Isiwe miaka hii, ya historia nyeusi!
Awamu iloanzia, ndiyo inaendelea,
Urafiki ilizua, hadi mitano kwishia,
Kipindi kilofatia, ajabu zikazuliwa,
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
Kubenea kuanzia, asidi akamwagiwa,
Hadi leo analia, mbaya hajamjua,
Na wala hatujasikia, kama kapewa fidia,
Isiwe miaka hii, ya historia nyeusi!
Mwangosi akafatia, mchana akauawa,
Wakubwa wafatilia, hadithi hatujaijua,
Na bado hatujajua, wana kulipwa fidia,
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
Absalom kafatia, hadi uchongo kutiwa,
Uchunguzi waendelea, mwisho tutajionea,
Hekaya itayokuwa, ni rahisi kung'amua,
Isiwe miaka hii, ya historia nyeusi!
Umoja unatakiwa, mafia wameshaingia,
Waliko kuwafichua, na kubwa ni yao nia,
Nini wanaitakia, hii yetu Tanzania?
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
Waandishi mwatakiwa, ya kwengu kufatilia,
Ukweli mkaujua, ili kinga kuitwaa,
Mkiwa mwaangalia, kulia huwa tabia,
Isiwe miaka hii, ya historia nyeusi!
Haraka mnatakiwa, mitandao kuizua,
Nchi mkaichungua, na wabaya kuwajua,
Kama ni hongo wapewa, na nyie si mnayajua?
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
Huenda ndani kakaa, mbaya msiyemjua,
Au mahala katulia, kimulimuli akawa,
Mbele anatangulia, mumiani kufatia,
Isiwe miaka hii, ya historia nyeusi!
Ili nchi kuokoa, wamulikeni mafia,
Nchini walioingia, kuharibu Tanznia,
Mhanga kujitolea, salama wana kukaa,
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
Isiwe miaka hii, ya historia nyeusi!
Huhalalisha kuua, ili cheo kupatiwa,
Au fedha kuzikwaa, kisha wakazichezea,
Yafaa kujiokoa, kwa wao kuwatambua,
Isiwe miaka hii, ya historia nyeusi!
Mungu hawakujaliwa, shetani waabudia,
Ndivyo inavyokuwa, na roho wasiojaliwa,
Fisadi huabudia, ukuu sio raia,
Isiwe miaka hii, ya historia nyeusi!
Twawaomba waheshimiwa, doa hili kulitoa,
Nchi inahujumiwa, kwa kuwa na sifa mbaya,
Tujali demokrasia, na uhai kwangalia,
Isiwe miaka hii, ya historia nyeusi!
Subscribe to:
Posts (Atom)