Tuesday, April 9, 2013

ISIWE MIAKA HII NUHUSI !!!

 
Wakuu twawaambia, juu walioshikilia,
Macho yao kufungua, kujua kinachoendelea,
Wapunguze kusinzia, hali watu wauawa,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Awamu iloanzia, ndiyo inaendelea,
Urafiki ilizua, hadi mitano kwishia,
Kipindi kilofatia, ajabu zikazuliwa,
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
 
Kubenea kuanzia, asidi akamwagiwa,
Hadi leo analia, mbaya hajamjua,
Na wala hatujasikia, kama kapewa fidia,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Mwangosi akafatia, mchana akauawa,
Wakubwa wafatilia, hadithi hatujaijua,
Na bado hatujajua, wana kulipwa fidia,
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
 
Absalom kafatia, hadi uchongo kutiwa,
Uchunguzi waendelea, mwisho tutajionea,
Hekaya itayokuwa, ni rahisi kung'amua,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Umoja unatakiwa, mafia wameshaingia,
Waliko kuwafichua, na kubwa ni yao nia,
Nini wanaitakia, hii yetu Tanzania?
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
 
Waandishi mwatakiwa, ya kwengu kufatilia,
Ukweli mkaujua, ili kinga kuitwaa,
Mkiwa mwaangalia, kulia huwa tabia,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Haraka mnatakiwa, mitandao kuizua,
Nchi mkaichungua, na wabaya kuwajua,
Kama ni hongo wapewa, na nyie si mnayajua?
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
 
Huenda ndani kakaa, mbaya msiyemjua,
Au mahala katulia, kimulimuli akawa,
Mbele anatangulia, mumiani kufatia,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Ili nchi kuokoa, wamulikeni mafia,
Nchini walioingia, kuharibu Tanznia,
Mhanga kujitolea, salama wana kukaa,
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Huhalalisha kuua, ili cheo kupatiwa,
Au fedha kuzikwaa, kisha wakazichezea,
Yafaa kujiokoa, kwa wao kuwatambua,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
 
Mungu hawakujaliwa, shetani waabudia,
Ndivyo inavyokuwa, na roho wasiojaliwa,
Fisadi huabudia, ukuu sio raia,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Twawaomba waheshimiwa, doa hili kulitoa,
Nchi inahujumiwa, kwa kuwa na sifa mbaya,
Tujali demokrasia, na uhai kwangalia,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
 

No comments: