Nyumba ikosayo haki, baba huwa mnafiki,
Limbwata ikimwashiki, ya wana hatoafiki,
Akaachia mikiki, rabsha na taharuki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Biblia hutaliki, na Daudi hasemeki,
Qurani haifunguki, ya Selemani kucheki,
Akili zao riziki, na kisha umamuluki,
Nyumba isiyo na haki, maisha haijengeki!
Wangeata unafiki, mistari ina haki,
Wasingejaribu hiki, hofu ingetamalaki,
Ujinga wauafiki, dunia haisomeki,
Nyumba isiyo na haki, milele haisimamiki!
Nyumba ikosayo haki, baba huwa mnafiki,
Limbwata ikimwashiki, ya wana hatoafiki,
Akaachia mikiki, rabsha na taharuki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Nuru haimpeleki, na aendako haafiki,
Katikati huafiki, akakwaza ushtaki,
Akawa haaminiki, na leke halithaminiki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Huzaa huambiliki, na mkubwa unafiki,
Ya usawa na ya haki, yawe kwake
hayasikiki,
Wakasepa washtaki, yawe hayaeleweki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Ya haki akataliki, na kuikwaza milki,
Baraka ikahamaki, na hekima kuishtaki,
Ukazuka umamluki, pia nao uzandiki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Nyumba isiyo na haki, wevi wataibariki,
La kweli halitamkwi, na uongo huafiki,
Wema ukawa kisiki, waovu hawautaki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Umma huudhhaki, yeye ndio mwenye haki,
Kusema wasidiriki, wanaihofia dhiki,
Ila wakitaharuki, nao huja kuhamaki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Huukataa uzandiki, na kubwaga unafiki,
Wakaililia haki, kila kona kutamalaki,
Ukaisha umamluki, kwa kumhofu Maliki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Nyumba yetu ibariki, ewe bwana mtoa haki,
Hakikisha hawafiki, wote wenye unafiki,
Kiwatibue kisiki, wawe juu hawaamki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina amani!
Huzaa huambiliki, na mkubwa unafiki,
Ya usawa na ya haki, yawe kwake
hayasikiki,
Wakasepa washtaki, yawe hayaeleweki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
Madaraka
huwanoki, injini haziamki,
Ya mwana hawashtuki, ila yao huhamaki,
Usanaa huulaki, sera wakaiafiki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina amani!
Umma huudhhaki, yeye ndio mwenye haki,
Kusema wasidiriki, wanaihofia dhiki,
Ila wakitaharuki, nao huja kuhamaki,
Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!
No comments:
Post a Comment