Tuesday, April 9, 2013

SHETANI WA NA MIMI NICHINJE !


 

Shetani wa na mimi nichinje

 

ASILI tunaijua, itokako Tanzania,

Mababu waliamua, nani wa kutuchinjia,

Mwaikana historia, na utu kuuchezea?

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Tuliungana jamii, nasara na islamiya,

Ndugu tukawaachia, kazi ya kutuchinjia,

Mbegu tukiitambua, Ibrahimu kuanzia,

Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na alegee!

 

Yaliyoishaamuliwa, vipi twaja yafukua,

Makaburi kuyazua, walo hai kuwatia,

Au mnalololijua, sisi bado kulijua?

Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na alegee!

 

Yapo ya kuzungumzia, nchi ikaendelea,

Barabara zatakiwa, vijijini kuingia,

Na madaraja kuzua, watu wakajivukia,

Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na alegee!

 

Mashamba yanatakiwa, kulima kulisha Tanzania,

Na kiasi kuongezea, dunia kuiuzia,

Kuchinja twapigania, hivi kweli twajijua?

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Hivi kweli twajijua, kwa tunayojisemea,

Au wehu watuingia, ya ovyo kujiamlia,

Dunia kutushangaa, mfano  tuliokuwa?

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Mengi tungelifikiria, ubora kujiongezea,

Afrika kutambua, ni darasa tumekua,

Sisi tukatangulia, na wengine kufatia,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Ya wa Kongo twaamua, sasa kwenda kurejea,

Kwanza tungejichungua, kama wazima raia,

Au tumeingiliwa, na walio ni vichaa,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Burma ukiangalia, kichaa kajizukia,

Ndugu anawachukia, na uadui kuwatia,

Hivi sasa awaua, na nyumba kuwaunguzia,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Iraqi na Syria, dini zinahujumiwa,

Wauana raia, kwa hata wasiyojua,

Ni vichaa wamekuwa, nchi zinateketea,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Amiri anatakiwa, katikati akakaa,

Mstari kuutia,  hakuna wa kuuchezea,

Maaamuzi yatakiwa, sio lawama kutoa,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Maji yanatusumbua, lazima kujivunia,

Majumbani kuingia, na mashambani kumwaa,

Kuchinja wito likiwa, naona tunafulia,

Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na alegee!

 

Kongo wanatungojea, kwenda kuwahubiria,

Nchi ya kati nayo pia, uamsho yangojea,

Kimataifa tukiwa, thumni hatutapigania,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Masoko kujitafutia, nyie mngetangulia,

Wafuasi kufatia, sadaka wakajipatia,

Michango yao ikawa, na nchi kwenda chanua,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Nchi ninaiombea, kuvuka hii balaa,

Kwa uongo kukataa, na ukweli kulilia,

Salama ya Tanzania, sote yatutegemea,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

No comments: