Shetani wa na mimi nichinje
ASILI tunaijua, itokako Tanzania,
Mababu waliamua, nani wa kutuchinjia,
Mwaikana historia, na utu kuuchezea?
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Tuliungana jamii, nasara na islamiya,
Ndugu tukawaachia, kazi ya kutuchinjia,
Mbegu tukiitambua, Ibrahimu kuanzia,
Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na
alegee!
Yaliyoishaamuliwa, vipi twaja yafukua,
Makaburi kuyazua, walo hai kuwatia,
Au mnalololijua, sisi bado kulijua?
Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na
alegee!
Yapo ya kuzungumzia, nchi ikaendelea,
Barabara zatakiwa, vijijini kuingia,
Na madaraja kuzua, watu wakajivukia,
Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na
alegee!
Mashamba yanatakiwa, kulima kulisha
Tanzania,
Na kiasi kuongezea, dunia kuiuzia,
Kuchinja twapigania, hivi kweli twajijua?
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Hivi kweli twajijua, kwa tunayojisemea,
Au wehu watuingia, ya ovyo kujiamlia,
Dunia kutushangaa, mfano tuliokuwa?
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Mengi tungelifikiria, ubora kujiongezea,
Afrika kutambua, ni darasa tumekua,
Sisi tukatangulia, na wengine kufatia,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Ya wa Kongo twaamua, sasa kwenda kurejea,
Kwanza tungejichungua, kama wazima raia,
Au tumeingiliwa, na walio ni vichaa,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Burma ukiangalia, kichaa kajizukia,
Ndugu anawachukia, na uadui kuwatia,
Hivi sasa awaua, na nyumba kuwaunguzia,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Iraqi na Syria, dini zinahujumiwa,
Wauana raia, kwa hata wasiyojua,
Ni vichaa wamekuwa, nchi zinateketea,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Amiri anatakiwa, katikati akakaa,
Mstari kuutia, hakuna wa kuuchezea,
Maaamuzi yatakiwa, sio lawama kutoa,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Maji yanatusumbua, lazima kujivunia,
Majumbani kuingia, na mashambani kumwaa,
Kuchinja wito likiwa, naona tunafulia,
Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na
alegee!
Kongo wanatungojea, kwenda kuwahubiria,
Nchi ya kati nayo pia, uamsho yangojea,
Kimataifa tukiwa, thumni hatutapigania,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Masoko kujitafutia, nyie mngetangulia,
Wafuasi kufatia, sadaka wakajipatia,
Michango yao ikawa, na nchi kwenda chanua,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
Nchi ninaiombea, kuvuka hii balaa,
Kwa uongo kukataa, na ukweli kulilia,
Salama ya Tanzania, sote yatutegemea,
Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na
alegee!
No comments:
Post a Comment