Thursday, November 29, 2012

Vijiji sio Ulaya

KUZURU mapambo huwa, kitu kisichosadia,
Ni mkubwa udhia, wanavijiji wajua,
Wao mbuga hawajawa, wanyema kuangalia,
Vijiji sio Ulaya, mnaenda kutembea ?

Nchi kuendelea, makada wanatakiwa,
Vijijini kwenda kaa, mema wakayaamua,
Dhiki wakizielewa, ni rahisi kutatua,
Vijiji sio Ulaya, mnaenda kutembea ?

Ukenda kutembelea, nini utakiongea,
Watu hukuangalia, mate wakajitemea,
Shere mnawachezea, wala dawa  hamjawa,
Vijiji sio Ulaya, mnaenda kutembea ?

Kwingine watachimbua, afu wakajipatia,
Hawatakutegemea, mjini unaykeaa,
Mzigo umeshakua, kiondoka huridhia,
Vijiji sio Ulaya, mnaenda kutembea ?

Kijijini ukikaa, mengi utayasikia,
Tena ukajionea, mepesi yaliyokuwa,
Ila miamba yakaa, ugumu wakautia,
Vijiji sio Ulaya, mnaenda kutembea ?

Vijisenti kadhaa, matatizo hutatua,
Watu wakachekelea, na dua kukuomboa,
Mpango ukiuzua, bora hujayakazaliwa,
Vijiji sio Ulaya, mnaenda kutembea ?

Akili mkitumia, vijijini mtakaa,
Babu tunamtambua, hawa aliyojaliwa,
Butiama alikaa, tena akijilimia,
Vijiji sio Ulaya, mnaenda kutembea ?

Ardhi budi kujua, kitovu yakichukua,
Nayo si ya kuiachia, watakiwa kurejea,
Kwa muda ukendakaa, kiungo kinarejea,
Vijiji sio Ulaya, mnaenda kutembea ?

Akili huzifungua, ukaanza pambanua,
Ya jua na ya mvua, tofauti ukajua,
Na kisha ukiamua, manufaa huzaliwa,
Vijiji sio Ulaya, mnaenda kutembea ?


No comments: