Mwapasa kuyasikia, kutengwa budi ikawa,
Kati mkiwaachia, wengine wataugua,
Wakoma huwa watengwa, kuyaepuka madhara !
Rushwa tumeitambua, ni ukoma waingia,
Kimya tukijikalia, itakuja tuumbua,
Umma naushadidia, hili kuja lihofia,
Wakoma huwa watengwa, kuiepuka hasara !
Kut9jua nakataa, hilo haliwezi kuwa,
Huruma tumeingia, utadhani ni ukiwa,
Macho tunalifumbia, liletalo kulemaa?
Wakoma huwa watengwa, kuyaepuka madhara !
Tunatia ujamaa, na udugu kutetea,
Karibu tunawajua, pembeni hawajakaa,
Tutumialo sinia, hilohilo watumia,
Wakoma huwa watengwa, kuiepuka hasara !
Lawama tukizitoa, nini zinasaidia,
Au aibu na haya, huwa hapo zapotea,
Na katika jumuiya, ndo pekee walokuwa ?
Wakoma huwa watengwa, kuyaepuka madhara !
Kuna mengine udhia, mtu ukifikiria,
Mafuu utadhania, jinsi tunavyoamua,
Au kama twachezewa, kutogwa na wasiokuwa,
Wakoma huwa watengwa, kuiepuka hasara !
Mizizi tunaing'oa, kwa majani twapandia ?
Mbuyu haijakuwa, watu kuja kushangaa,
Watauona mzaha, wakacheka na kulia,
Wakoma huwa watengwa, kuyaepuka madhara !
Ujumbe umetimia, imebaki kuamua,
Salama kutopotea, Tanzania wangojea,
Maamuzi kusikia, ulua yaliyojaa,
Wakoma huwa watengwa, kuiepuka hasara !
No comments:
Post a Comment