Hilo nilitangazile, wa kujua akajua,
Silo linalonogile, mabichwa wakijitia,
Ngoma hii tuchezele, waalikwa twawajua?
Mbinuze ni zilezile, mwele kutibu mganga!
Majini na misukule, huko yalikotokea,
Zumari na vibwagile, mila havijaridhia,
Uliona wapi ndwele, ikaja ikawa dawa?
Mbinuze ni zilezile, ya kichwa kuwa mkia!
Wasemele walewale, kila kitu kujitia,
Wasiokuwa simile, na wakubwa kuwajua,
Wao wakajidhanile, vinara wameachiwa?
Mbinuze ni zilezile, ya juu kuwa ya chini!
Hawakujua upole, ya shujaa tabia,
Na uoga anogile, hadi akadharauliwa,
Na walii si mkwale, neema alijaliwa,
Mbinuze ni zilezile, kushoto kuwa kulia!
Maisha ni kuvukile, madaraja kupitia,
E, mwanangu Chaupele, budi hili kuridhia,
Nalo tulitafutile, halibaki ila dua,
Mbinuze ni zilezile, janibu kuwa ghaibu!
Mchangani liishile, dunia 'kaendelea,
Palepale ubakile, au nawe kufagiwa,
Ina wake wateule, nasi si tunaojua,
Mbinuze ni zilezile, rafiki kuwa adawa!
Waache na kimbelembele, yatakuja kutokea,
Hadharani wapandile, wakicheza kidedea,
Hapo hapo washukile, kwenye vumbi kwogelea,
Mbinuze ni zilezile, halali kuwa batili!
UKifikia kilele, ngwee hautopandia,
Hubakia kushukile, chini kwenda kurudia,
Ukajua lipandile, kushuka ni yake ndia,
Mbinuze ni zilezile, ukweli kuwa hadaa!
Mja hanayo milele, muumbwa kifo kapewa,
Na wakati ufikile, ndiyo ya mwisho hidaya,
Lazima uchukulile, na weye kuchukuliwa,
Mbinuze ni zilezile, mwele kutibu mganga!
Nyie sio wajuvile, haya mambo mwaelewa,
Na wao si waanzile, kitu kuwashtukia,
Zege letu polepole, na haliachi kolea,
Mbinuze ni zilezile, mwele kutibu mganga!
Na lengo ni lile lile, shabaha yenye kujua,
Wateule wenye ndwele, dawa yao kuijua,
Hakika ni wapitile, kuwasindikiza tabia,
Mbinuze ni zilezile, mwele kutibu mganga!
Adili namtanguzile, yanyooka yake njia,
Wala si wa kupindile, na kona kujikatia,
Vya kesho agawalile, mauti visivyojua,
Mbinuze ni zilezile, mwele kutibu mganga!
No comments:
Post a Comment