Monday, June 18, 2012

Ghorofa haina msingi



VIJANA wanaondoka, wazee wamewachoka,
Kisa wanahamanika, ukale unatukuka,
Na nchi wanaoshika, hawataki badilika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Msingi umeng'oleka, wa vijana watukuka,
Vibabu vyahangaika, upepo kuzuilika,
Kwao makubwa mashaka, hawana lenye hakika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Mafuriko yamezuka, maji yazidi mwaika,
Msingi unachimbuka, wazee wameridhika,
Utaifa unatoweka, kwa uchama kuushika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Babu ameshatoweka, wamebaki vibabuka,
Kwa yao kughafilika, na ya watu kubweteka,
Kaniki zimahamanika, vikoi pia na shuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Waizima Tanganyika, kama sio kunyongeka,
Wahofu ikifufuka, itakuja na mizuka,
Kukumbatia wataka, yao wanaoyataka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Tuteni inafanzika, na mabomu kupigika,
Wao wanayoyataka, kuyafosi kufanzika,
Watuzulia mashaka, kutugharimu viraka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Dunia sasa yataka, madogo ya kushikika,
Makubwa wanaepuka, huwezi kuimarika,
Vivuko hautovuka, mtoni utaanguka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Ushirika wanataka, si'noa iso talaka,
Ukitaka kuachika, pasiwe wa kukuteka,
Hili lisipofanyika, utata hatutaepuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Watu sasa wamechoka, ndani kuwa wawekeka,
Wataka yao kuzuka, hadhi yao kupangika,
Na mambo kunyooka, sio yazidi pindika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Katiba kama  kibaka, katu haitapendekea,
Ikizua ya kutaka, nani atasalimika ?
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Zabzibar wanaotaka, kura huru kupigika,
Kadhalika Tanganyika, Tanzania ikazuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Tatu ndizo tunataka, serikali za hakika,
Ya umoja kuiweka, kcuhangia ushirika,
Ndogo itayojengeka, na watu wenye hakika,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Na uchama kupunguka, utaifa kujengeka,
Na kisha ikajazuka, mikoa ya madaraka,
Mfano ukaushika, nchi hii kujengeka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Hili halina mashaka, ajira zitafufuka,
Mikoa ikichemka, ushindani ukazuka,
Uchumi utanyanyuka, na wakazi kuridhika,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Mikoa itajengeka, Unguja na Tanganyika,
Na Pemba kuerevuka, ukawaisha wahaka,
Kote nchi kujengeka, kwa ushindani kuzuka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Chama kisichoitaka, hiyo  yetu Tanganyika,
Sio cha Watanganyika, wajua walikotoka,
Sasa kumepambazuka, na ujinga watoweka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Utumwa tulivuka, leo ya nguvu mwataka ?
Weusi mmegeuka, wakoloni wa kuteka ?
Uhuru nusu yafika, nusu nyingine twataka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

No comments: