Monday, June 18, 2012
Tanganyika, tanganyika
Pacha alishatoweka, mmoja amebakia,
Wapi alipofichika, watu wataka kujua,
Mpotevu asemeka, raia kumfichua,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Tanzania twaitaka, izidi kuendelea,
Pia yetu Tanganyika upya ikazaliwa,
Tuweze yetu kushika, ikawa twajitambua,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Usawa haukufanzika, Tanganyika kuondoa,
Laana ikatufika, mpaka leo balaa,
Yao wanaoyataka, ndio visa wanazua,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Zanzibar na Tanganyika, ndiyo huwa Tanzania,
Mmoja akitoweka, ni kingine kitakuwa,
Msingi hautojengeka, chini utatumbukia,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Hakunao ushirika, upande ukaumia,
Na ubia huponzeka, upande kupendelea,
Ikifika kuhongeka, taabu kubwa inakuwa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Upofu umetufika, ukweli twaukataa,
Mbali sana itafika, Zanzibar itapaa,
Mamboye ikiachiwa, huru ikajifanzia,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Kadhalika bara pia, miko huru ikiwa,
Waziri mkuu akawa, n dio anaangalia,
Mbali sana itapaa, ngazi ya juu ikawa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Ni wanasiasa njaa, ukale waliosalia,
Zama wayang'ang'ania, kwa tija yasiyokuwa,
Kwenye juzi wabakia, utandawazi wakataa ?
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Mawaziri watajaa, pamwe na wabunge pia,
Bara na Zzanzibar, na kisha wale wa mkoa,
Ni shule tutajaliwa, viongozi kusomea,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Ushindani utazaa, mazuri yaliyokuwa,
Na watu bora kuibua, mikoani kuwajua,
Taifani kuingia, na ujuzi waliokuwa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Wakati umefikia, Tanzania kuchagua,
Na kama kuendelea, Tanganyika kurejea,
Mola atatujalia, tuyatakayo yakawa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment