Friday, June 1, 2012

D O D O M A


Mji mkuu umekwama, unashindwa kusimama,
Kimejikusuru chama, kubeba Darisalama,
Mshumaa unazima, kufikiria kuhama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Huko nyuma walisema, katikati na salama,
Nduli aliporindima, kila kitu kikagoma,
Miezi minane ngoma, wakaamba ni lazima,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Miezi minane ngoma, wakaamba ni lazima,
Hata ilipoyoyoma, meli ikazidi zama,
Mzee akanguruma, IMF akaitoma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Na wajanja wakachuma, uhunzi ulipokoma,
Babu alipotazama, cheche mwisho  akatema,
Kustaafu lazima, nchi  ibaki salama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Thelathini yatetema, mitatu ingali nyuma,
Toka wapya kuegema, na yao wakayafuma,
Bunge kweli limehama, na chuo kinasimama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Ila wizara zakwama, nani ataka kuhama,
Mizizi Darisalama, chini imeshajitoma,
Na bahari waipema, upepo mkavu Dodoma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Sokoine alihama, wao wakarudi nyuma,
Ndwele bado zarindima, zinafichwa ndarahima,
Yapo tusiyoyasema, kuelekea Kigoma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?
Wagogo washika tama, haijafika neema,
Ila nyama ya kuchoma, na shingoni zinakwama,
Maji yazidi yoyoma, kuiga Darisalama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?
Tabora kwenda lazima, na konani ni Kahama,
Reli yaota mtima, wananchi wanazizima,
Na sasa kwao tuhuma, kuyabeba mataruma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Nazi kaziye kugema, mnazi ukiufuma,
Kama hauna mtama, na maziwa yasimama,
Bongo zetu ziko nyuma, kuiunda zimekwama ?
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Au suti wazipima, na reli inaroroma ?
Vijana wakijituma, na mtaji wakauchuma,
Kutengeza watakwa, au sisi tunagoma ?
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Uamuzi ni lazima, kitu gani ni Dodoma,
Kuhama au kutohama, sasa wimbo unakwama,
Nchi isiyo azma, kwneda mbele ni gharama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Miaka inayoyoma, labaki vumbi Dodoma,
Twangonja mwenye huruma, ya kwetu kwnenda yakama ?
Uhandisi wansoma, au vitabu wachoma ?
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Karne hii kiama, kuyafanza tukikwama,
Intaneti kujitoma, vitendo tukavisoma,
Wenyewe tuna lazima, miundombinu kuchuma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au ni Dar es Salaam ?

No comments: