Thursday, June 21, 2012
Nikipendacho si mwili
Nikipendacho mpenzi, ni roho na moyo wako,
Sio mwili wala ngozi, huisha kwenye maziko,
Viwili hivyo vya enzi, hata huko niendako,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Ni roho na moyo wako, nikipendacho si mwili,
Na katika uhai wako, hivyo kwangu ndio mali,
Na mimi kila niliko, njema hutakia hali,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Nikipendacho ulimi, usiokuwa muhali,
Daima unaojihami, kutotia idhilali,
Ukataao rasmi, umbeye kuuhimili,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Nipendacho adili, maovu haufumi,
Ukawa kwangu kandili, na ndia yangu ya lami,
Mitego kuikabili, kwangu ukawa ami,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Na roho niipendayo, makuu isiyokuwa,
Heshima ujengayo, bila ya kulaumiwa,
Tamaa isiyo nayo, haliye unaridhia,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Roho isiyo kinyaa, na matapishi kujaa,
Ndani inayotulia, yangu kunihudumia,
Mola inayomhofia, mabaya ikakimbia,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Mema ilodhamiria, kwa mchana na usiku,
Machozi inayotoa, uchamungu na shauku,
Inayowasaidia, walo kule, walo huku,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Moyo ninaoutaka, ovyo usiotamani,
Ujajuayo mashaka, ya uchu wa duniani,
Kila siku huridhika, kipatacho mkononi,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Kwa mwili tunaponzeka, usizo nazo akili,
Watu tukadangayika, wengi tukawa anzali,
Mitihani kuanguka, tuwe daima twafeli,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Mwili mkubwa ajali, bure unathaminiwa,
Hata usio akili, na udhaifu kujaa,
Wenye giza si kandili, mushiriki ulokuwa,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Rijali na wanawali, mwishowe wakaanguka,
Zidhoofu zao hali, yakawafika mashaka,
Pasiwe na afadhali, iwe vuta na chanika,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Waweza upenda mwili, mtu akose akili,
Na rijali na wanawali, kizazio bilkuli,
Kikawa chote muhali, kujaliwa ya akili,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Nenda kaoe akili, nakushauri bilali,
Mwili ni kitu muhali, uitakapo akili,
Ni mkubwa ubahili, bongo kwake ni ajali,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment