Wednesday, October 31, 2012

SIMAMA NA WEWE UHESABIWE


Mkono sasa tumia, juu ukaunyanyua,
Wito ukaitikia,  taifa kutumikia,
Uongofu lalia, ni nani wa kulifaa,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Wakati ni huu hawa, wapaswa kuhesabiwa,
Kwa upande kuchagua, kusimama kutetea,
Heri ukiichagua, shari hutolichukua,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Bahari yachafuliwa, na wengi maharamia,
Meli wameidandia, wahofu mabaharia,
Ya heri tukiamua, nahodha tutamfaa,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Nahodha tukimfaa, akili zitatulia,
Meli kujiongozea, hadi nanga tukatia,
Na wengine kuachia, wasoitaka balaa,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Na salama Tanzania, ikazidi kubakia,
Ghasia kuziondoa, za wasya hasiria,
Mabomu kutochimbua, viazi tukidhania,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Rushwa imeshatapakaa, kama panya tumekua,
Paka tunamuhofia, mafichoni twaingia,
Kila anayeisikia sikio ajifumbia,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Nani mwenye ushujaa, mhanga kujitolea,
Kama babu wa India, uzee kajipambua,
Kitalini kaingia, bure wakamzuia,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Kila mtu ashangaa, wakubwa kando kulia,
Ngoma kati imekaa, pembeni waugulia,
Nani aliyetakiwa, ujemadari kuuvaa ?
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Uongo ukitumiwa, mwisho ukweli ukawa,
Nani atatuelewa, timamu waliokuwa,
Guu limetangulia, kule tusikotakiwa,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Musuli waliopewa, kwa kuwatunza hidaya,
Leo wafanya mabaya, hila wanaitumia,
Nyara watu wote kuwa, wapendavyo ndivyo huwa?
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Haitojenga hadaa, nchi safi ilokuwa,
Viinimacho vikiwa, maruerue hujaa,
Turudi nyuma raia, na msokuwa raia,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Kioo tumekikimbia, twezacho jiangalia,
Taasisi zazaliwa, bure hela kutumiwa,
Na kazi zilizopewa, rukusa zakataliwa ?
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Sasa kihoro watia, wakubwa waugulia,
Kucheka najizuia, kila nikiwasikia,
Au yaweza ikawa, tuna 'bosi' tusomjua ?
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Mwenzi ngao augua, kilemba kukikazia,
Kinamama ni bidhaa, leo wananunuliwa ?
Nini kilichobakia, nchi bado kupotea?
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Wazee kwa yao njaa, waukubali udhia,
Nani wa kuwaangalia, wasiende nunuliwa,
Hali ilivyo ni mbaya, kapuni wataingia,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Vijana tunawagawa, kwa fefha kuwarushia.
Huku tunachekelea, wanavyozipigania,
Masalale naitoa, Mola kutuhurumia,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Wazazi gumba wakiwa, huko huko  twelekea,
Ndoano kuiachia, kazi kubwa itakuwa,
Yao yote wamefulia, nin kilichobakia ?
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Watu wanaulizia, hivi hii ndiyo njia,
Nyerere katuachia, sisi kuifatilia,
Au tumeshapotea, twanda tusikokujua ?
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Mishipa imetujaa, twazidi kung'ang'ania,
Twajua tumekosea, tayari twakoselewa,
Kukubali twaktaa, sawa tunajionea,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Sasa waliojaliwa, katikati waingia,
Samaki wanawavua, nchi kavu walokuwa,
Mipango tumefulia, baharini kwenda vua,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Mipesa waitumia, vijana kuwanunua,
Kisha pande tukagawa, hawa na wasiokuwa,
Kule macho twafumbia, huku twawakolea ?
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Dabo standadi mbaya, mbali hatutafikia,
Basi tulilodandia, tairi zajichimbua,
Bondeni twaelekea, na kingo kusikokuwa,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Mamlaka zatakiwa, haki kuisimamia,
Vingine inapokuwa, kadhia naihofia,
Utu waja kujifia, Tanzania italia,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Kiooni kujangalia, muda umeshawadia,
Tena bila kuchelewa, tusije kuadhiriwa,
Tutofautishe ubaya, na mazuri kuchagua,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Huu ni wangu usia, moyoni ninautoa,
Nchi hii kwangu ua, waridi lilotulia,
Kwa amani na umoya, bara linajipambia,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Watu wangu wema huwa, ila wanapoonewa,
Kisha wakabaguliwa, kufanzwa kisichokuwa,
Moyoni wakiumia, mateke wataachia,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Walojuu watakiwa, haki kuisimamia,
Kuna vyombo vyaingia, haki sasa zinaua,
Macho mkiyafungua, ukweli mtautambua,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Naasa kutoamua, pasina kweli kujua,
Daudi alitubia, kosa alipotambua,
Vingine ikijakuwa, ujibari ni nazaa,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Mola nakugeukia, Maulana ulokuwa,
Mtukufu na mjua, njia unazawadia,
Sahihi iliyokuwa, watuwe kutopotea,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!

Nasi twakuangukia, mustakimu kuijua,
Taifa kusaidia, salama likabakia,
Vizazi vikafatia, bila ya kuhujumiwa,
Simama uhesabiwe, nchi ilipokutaka!






Viongozi wa kidni


Msiwe sawa waumini, moyo uwe akilini,
Elimu mwaithamini, akili zitumieni,
Msibwabwaje kundini, ila palipo yakini,
Viongozi wa kidini, akili 'siwe moyoni!

Sera zenu zinahini, wengi kuwa masikini,
Na fukara ni pagani, au hili hamwamini?
Leeni kwenye imani, kwa kuzifata kanuni,
Viongozi wa kidini, akili 'siwe moyoni!

Msiambe ritadini, kukoma umaskini,
Amani nguo ya ndani, msiikwaze hadharani,
Kwa tendo na ulimini, ufanzeni ulaini,
Viongozi wa kidini, akili 'siwe moyoni!

Rugambwa mkumbukeni, na askofu uchaguni,
Moshi waliyobaini, wakaienzi amani,
Mkiingia kundini, nchi yenda mashakani,
Viongozi wa kidini, akili 'siwe moyoni!

Nyote tunawaenzini, kuwa ni watu makini,
Mwafikia kileleni, shahada mnaauni,
Yaingiyo kichwani, kwa watu yatumieni,
Viongozi wa kidini, akili 'siwe moyoni!

Nyuma katu msibakini, ingineni uongozini,
Sio kwa siasa zaini, ila kwa zenu imani,
Uongozi kubaini, si lazima siasani,
Viongozi wa kidini, akili 'siwe moyoni!

Hapo mlipo mjini, na mkaako vijijini,
Ni viongozi amini, ustawi  kubaini,
Watu wote muwapeni, ya hapa hapa duniani,
Viongozi wa kidini, akili 'siwe moyoni!

Isiwe tu ni amani, maendeleo leteni,
Kama mkate amani, na siagi  ipakeni,
Hapo ndipo hubaini, ustawi kuauni,
Viongozi wa kidini, akili 'siwe moyoni!

VITU HIVI SI MABOMU ?

NJAA naihofia, chanzo cha hizi ghasia,
Kuishi usiyejua, nini kesho wajiia,
Riziki kungojea, ya sadaka kugawiwa,
HIVI huu ni udini, au yatokota njaa ?

Kuishi usiyejua, mwana vipi wamlea,
Kwa karamu kungojea, tajiri kumpikia,
Makombo ukachukua, wana kuja walishia,
Hivi vitu si mabomu,  njaa na umaskini !

Kushi bila kujua, ni mtumwa wa majaa,
Ukafiri ukatiwa, kwa sharti za kupewa,
Utaikifu dunia, uchafu ukishajaa,
Hivi vitu si mabomu, ajira kukosekana?

Matambara utakuwa, na mitumba wa kuvaa,
Huku unajionea, yako yakipakuliwa,
Mtupu ukaachiwa, maganda umeshakuwa,
Hivi vitu si mabomu, ujinga na kununuliwa?

Dira huwa zakataa, njia kutojionea,
Na kila ukifikiria, mbaya utamdhania,
Juu anayekukalia, kama jiko na mkaa,
Hivi vitu si mabomu, wongo na udanganyifu?

Kisha hukusimuliwa, na ukweli yasokuwa,
Nawe akutarajia, hayo utamkubalia,
Kingine ukisikia, uongo wende kulia,
Zidini kutuibia, mola atatufidia!

Majira yakiwadia, joho hili hujivua,
Yako ukaangalia, si ya wengine kujua,
Pasiwe wa kukumbatiwa, ila haki mwanadawa,
Zidini kutuibia, mola atatufidia!

Umaskini asili

NITAKUWA ni bahau, tena kweli baradhuli,
Asili nikisahau, yangu na ya Kiswahili,
Babu sasa mjukuu, chabaki kitendawili,
Umaskini asili, katu siwezi 'sahau !

Nende milima na nguu, cha kwangu ni kiswahili,
Ni nusu yake juzuu, bilacho si mtu kamili,
Hujiona ni mafuu, mpungufu wa akili,
Umaskini asili, katu siwezi 'sahau !

Hili ni langu dau, kurudi kwenye asili,
Katu sintokisharau, kwa dhiki na udhalili,
Kama ni kupanda juu, bilacho sistahimili,
Umaskini asili, katu siwezi 'sahau !

Haunifai ukuu, bila asili akili,
Na mali za kijuujuu, mizizi kwao bahili,
Ila lililo mguu, kwenye badi na fasili,
Umaskini asili, katu siwezi 'sahau !

Sio jambo la malau, hii yetu stahili,
Lugha yetu kudharau, ufakiri twakubali,
Vigumu kuenga juu, itakuwa ni muhali,
Umaskini asili, katu siwezi 'sahau !

Ni watu wa chauchau, watufanzia batili,
Wakakataa nafuu, matumzi ya asili,
Wakaifanza juzuu, lugha isiyo awali,
Umaskini asili, katu siwezi 'sahau !

Wanaipiga dafrau, lugha yao ya asili,
Ukubwa wakakubuhu, yetu kufanza dhalili,
Kumbe wanajisahau, zaonyesha zote dalili,
Umaskini asili, katu siwezi 'sahau !

Japani si  mabahau,wajenga kwayo asili,
Na Uchina kwa nahau, sasa ni watu kamili,
Ila tuliojisahau, tusio watu kamili,
Umaskini asili, katu siwezi 'sahau !

Ila tuliojisahau, tusio watu kamili,
Kwa yetu kudharau, washindi ni Waswahili,
Ustawi ni malau, na vimbwanga ndo akili,
Umaskini asili, katu siwezi 'sahau !

Rais pia raia

KATIBA ya kutwokoa, pande zote kwangalia,
Juu huvunja sheria, kama chini nao pia,
Ovyo tukiachia, yaja kutugeukia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Sana ukiangalia, udhibiti watakiwa,
Nafasi ikichezewa, tunageuzwa majuha,
Nchi wakaichezea, tukabakia kulia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Kuwabana yatakiwa, baya kutotutendea,
Na kama tukilegea, wenyewe tunaumia,
Nchi huja kuigawa, vitani tukaingia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Madhambi ukichungua, si chini yaanzia,
Huwa kama ni mvua, juu inakotokea,
Ni wapambe haramia, njia humchanganyia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.
Katika hii dunia, watu wananunuliwa,
Nje wakajinunulia, nchi yao kujakuwa,
Na sisi tulio raia, ikawa twadharauliwa,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Tafakuri asokuwa, tajiri humnunua,
Wao akatumikia, sio nchi kuifaa,
Na hapo mkifikia, udikteta huzua,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Kuwa chini ya sheria, mahakama juu kuwa,
Hofu itawaingia, nafasi wakichukua,
Kuthubutu huhofia, mabaya kutufanzia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Mahakama chini kuwa, nchi ataichezea,
Fujo akatufanyia, kisha kutusingizia,
Haki ikajapotea, matatani kuingia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Jaji mkuu raia, wapaswa kumridhia,
Bunge wakalitumia, yeye likamteua,
Rais huyu ikiwa, huwa zavizwa sheria,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Kuna walionunuliwa, na wao wananunua,
Mfukoni akaitwia, Nyerere katuambia,
Aibu kuwa 'takuwa, nchi kama Tanzania,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Mama yetu ni sheria, na katiba juu yawa,
Kila hali yatakiwa, nyufa zote kuondoa,
Tusije tukajaliwa, kuja rais kichaa,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Ikawa yake sheria, yamlinda kwa udhia,
Dhambi akazizamia, huku twamuangalia,
Amin mnamjua, Uganda yaliyotokea,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Mali akazichukua, na ovyo kujifujia,
Hakuna la kumzuia, tukabaki twazubaa,
Na nyingine kuchukua, Uswizi akazitia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Mke, wana na jamaa, utajiri kuwagea,
Miradi akaiua, ili wao kuwafaa,
Nasi tukayaridhia, kwani hatunayo njia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Usultani kuzua, japo tuliukataa,
Watoto akatamia, cheo chake kuchukua,
Uarabuni twajua, mambo waliyoyazua,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Rais kushtakiwa, lazima kukubaliwa,
Kama akinunuliwa, hataka kumuondoa,
Watu akiwanunua, awe ameshaumia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Wananchi kuwaambia, si chini waliokuwa,
Ila juu wakalia, katiba wakiijua,
Wanaweza kumwondoa, madudu akifanzia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Budi hofu kumtia, nguvu yetu kuijua,
Kazi si kuichezaya. ila ya kuogopewa,
Ovyo tukiachia, midubwana waingia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Zama za kuwasifia, hivi sasa zajisia,
Kazi wamekusudiwa, mzigo kuuchukua,
Tena huru budi kuwa, bila wao kutumiwa,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Ahadi namuachia, hii ni yake dunia,
Naye analoamua, ndilo hasa linakuwa,
Na wasiojisadia, hawezi wasaidia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

T U N Z O H I Z I T U N A T O A

Tunzo tunawapatia, kwa sifa zilizopewa,
Hadharani twazitoa, kila mtu kuzijua,
Haki tumeangalia, na zote zahifadhiwa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo watu kununua, ukubwa kujipatia,
Hamsini ukitoa, huziganga zao njaa,
Vikundi ukinunua, ngazi za juu kupaa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo jilie nyamaza, yetu kutoyasikia,
Wakubwa tunawatunza, juu waliopitia,
Kisha wakaeneza, kesho yatakayotuua,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya ahadi hewa, nayo twawazawadia,
Kwa ahadi kuzitoa, ukweli zisizokuwa,
Tamaa ikabakia, maajabu kutokea,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo nyumba ni anasa, ustwai motokaa,
Na njaa ikitokea, ni chakula kitakuwa,
Karamu kuiandaa, wale raha Tanzania,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo fisadi ni ndugu, hauwezi mkataa,
Hii ni ya kichwa sugu, kinachong'aa kipaa,
Kutunza wetu undugu, kusahau inafaa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo umaskini dili, misaada kuinyakua,
Wazungu yao akili, burungutu kuachia,
Mtalalia ukili, dhahabu huku watwaa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo wazungu wa unga, kwa wote wanaojaa,
Wenetu wawachabanga, wao ukwasi wakwaa,
Vidagaa kuwafunga, mapapa huru raia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo chakula kibovu, pia na hiyo mbolea,
Kwa wale wote werevu, wapatao kwa kutuua,
Mungu awape wangavu, hadi roho kujitoa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo za kuteuliwa, akili kutoumia,
Sio wa kuchaguliwa, mkoa ukaulilia,
Pasiwe na kidedea, mkoa wahujumiwa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya kubaguliwa, wengine kupendelea,
Hata wasiotufaa, kazi wakaajiriwa,
Maeneo hufulia, yanangoja ogelea,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo fisadi kufaa, wala sio kumuachia,
Huyu mkweli shujaa, atakuja kuwafaa,
Vile tulivyojilia, 'usije jitapikia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo utumwa sheria, wapewe wanasheria,
Haki wanaojiuzia, dhulluma wakaitia,
Hata wasione haya, kungoja wanachopewa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo kilimo cha njaa, ni ujanja kutumia,
Mitumba kuinunua, trekta kama bandia,
Mfukoni ukatia, hela inayozidia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo geuza kibao, haki wanaozinunua,
Kisha wakajiuzia, kwa wakubwa walokuwa,
Tajiri kuwatumia, kama tambaa la mafua,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo rushwa tapakaa, kwa wanaoiachia,
Huku ndani wanalia, ipunguzeni jamaa,
Aibu mnatutia, kila mtu anajua?
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo mikopo hadaa, wapakue na pakua,
Kidogo ukishatoa, kingi ukakichukua,
Nchi yataka kuliwa, ipate kuendelea,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo urongo tumia, wajinga bado wajaa,
Ukweli ukazuia, hakuna watalojua,
Mkono ukishatia, mara moja ni kunawa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo udhibiti duni, mameneja wachukua
Wasiokuwa makini, vya kwao kuangalia,
Na pengine yumkini, watawala nao pia,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya kutofatilia, wengi hii wamepewa,
Yenyewe yajiendea, Mola anasaidia,
Utabiri kuutoa, vigumu haitakuwa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo nifae upate, wachache wazawadiwa,
Awali kupanga kete, zinduko kuzinduliwa,
Mwana ni simupopote, huwepo yasiyokuwa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya mwaga machozi, kuwapa waso hatia,
Akili wasioenzi, kwa nguvu kuzitumia,
Hawanzi mazoezi, mkosa kutambliwa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya maji upupu, mpita njia kumwagiwa,
Na kuachwa utupu, nguo unapozivua,
Ukavitupa vikapu, samaki kujiozea,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya hawa wenetu, wa kwanza kuangalia,
Halafu rafiki zetu, wale kinachobakia,
Asiyekuwa mwenetu, kesho kumfikiria,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya mlipa pigwa, kodi yako kutumiwa,
Wewe mwenyewe kupigwa, kwa silaha za kutungua,
Mgalagala kuagwa, fukweni mchanga hujaa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya maji tope, vijijini kujinywea,
Kisha wazuka mapepe, eti tumeendelea,
Na weusi si weupe, wakoloni weshakuwa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ua yafaayo, mfano kujitegemea,
Na michezo kufulia, pasiwe kuendelea,
Wote tunawapatia, hili waliochangia,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya mikopo njaa, watu wetu kuwafaa,
Hii ni ya ujamaa, kama vile kijamaa,
Tundu tunalitumia, cha kwetu  kupitishia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo mifuko ulaji, kuuza na kununua,
Kugawa kwetu mtaji, unene kupindukia,
Wahiji wanaohiji, sisi kazi kupakua,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo za kuwaibia, fukrara wasiojua,
Mifuko kuitumia, ya kwenu nyie kujaa,
Kila mkipungukiwa, ni kisima mwayazoa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo za simu iba, tafiru wanazotwaa,
Mianya wakaiziba, vyamani ilikojaa,
Mlalahoi kukabwa, kdiogo wakachukua,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya nchi gizani, umeme mtaji kuwa,
Tukiingia nuruni, neema itapotea,
Muhimu kuwa gizani, wafadhili kukamua,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo 'Baah' Ibrahimu, kama kondoo tukawa,
Hata yasiyo na hamu, tukaacha kukosoa,
Twapiga maktaimu, eti mbele twatembea?
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya mweupe bora, hotelini kuwatia,
Na weusi ni hasara, hawajui kutumiwa,
Tena wazidi ukora, na vifo kusingizia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya kula vya umma, kila wakijiuzia,
Wakaziziba tuhuma, na mengine kuhadaa,
Ubepari ni unyama, tumeanza jionea,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunza ya kifaurongo, sauti kuzisikia,
Katiba kupa mgongo, kelele amri ikawa,
Na mwana mlea zongo, haki hana, akapewa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo mipango sanaa, kipangwacho kutokuwa,
Ikawa waigizia, kama lililotokea,
Watu wabaki wakiwa, dhihaka wanafanziwa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo udhalililishaji, midude tunagawia,
Wapate la moto taji, zamu yao ikitua,
Karamu ubabaishaji, duniani huishia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo miradi Ulaji, cha mbele kikitolewa,
Utaifa uhitaji, tumbo linatangulia,
Ambayo sasa wahiji, hata wasio na njaa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya sahaulisha, madai kutojibiwa,
Watu wakakorofisha, la leo likachelewa,
Ila yao kuyapasha, usiku wakajilia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo yake potezea, nayo hapa yaingia,
Hoja inapoibuliwa, hewani kaishia,
Bengeni yanaanzia, ikulu ikadandia,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo la wala sinia, kisahani wakatoa,
Matumbo walojaliwa, na akiba kumegewa,
Nundu wanaozilea, kifuani zilojaa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo chama - baba mama, ukoo na familia,
Tamalaki wajituma, Jetwa wakamfikia,
Kuliokufa hekima, ikabakia udhia,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya kubebeshana, takataka kuchukua,
Kisha ukazilipia, aghali isivyokuwa,
Huku hali wafulia, chakula chakuishia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya njaa wanyama, hifadhini kuwatoa,
Uchumi ukakoroma, yasiyokuwa yakawa,
Wewe ukawa kiyama, cha wanyama Tanzania,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Yuraniamu uhai, tunzo inayotwimbia,
Ienziye maslahi, na ubinafsi kukua,
Hii wote watawahi, uhai wanaotania,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya dhahabu dili, awamu ya tatu yatwaa,
Walivyojaliwa akili, thamani bue kugawa,
Na mzuka kukabili, mwalimu nao alia,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya ng'ombe bure, aghali zinazokuwa,
Wamdhihaki Nyerere, na kujifanza wajua,
Na wenye kiherehere, nchi kuja kuiua,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !