Friday, June 28, 2013

Raia si watoto




Wanalosema wajua, sio wa kutamkiwa,
Watendalo waelewa, sio wa kuelezewa,
Vingine ikitokea, lawama mwajitakia,
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Hawajaugua kichaa, na kamwe sio majuha,
Wana lao wakilia, kusikizwa watakiwa,
Vingine inapokuwa, mwaendeleza udhia,
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Hata wasiobukua, na elimu kuzivaa,
Majoho kuning'inia, na kupambwa na kofia,
Kichwa tupu walokuwa, haki zao wazijua,
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Wafaragua sanaa, na vitendo maridhia,
Visivyoleta ukiwa, na jeraha kuwatia,
Adili ikisinyaa, kimya wategemea?
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Hali wanajionea, ghali bure kusifiwa,
Lao wanalolijua, gharama zawalemea,
Hivi waache kulia, sawa mtajionea?
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Tofauti zinakua, hakuna la kuzuiwa,
Wa juu waogelea, chini wazama dhiraa,
Sera zimetibuliwa, nani kuwasaidia ?
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Kila aliyejaliwa, azidi kuongezewa,
Na yule asiyekuwa, alichonacho mwataa,
Wapi pa kuegemea, ikasikia dunia?
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Utundu mwawazuliwa, na ukaidi kuwatia,
Ya kwenu mpate zua, kuezuka na kuezua,
Nani wa kuangalia, ya kwao yaliyokuwa?
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Hamaki mnajitia, na vitisho kuvitoa,
Ndimi zinawalemea, madhambi yawachefua,
Nani ni wa kutubia, wakuu au raia?
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Vitabu mngefungua, adili mkaijua,
Ukweli mlioua, uanze tena chanua,
Haki mlojizikia, muanze kuzifufua,
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Muikomeshe hadaa, na wengine kuonea,
Kwa kuwa mmejaliwa, si wengine kushindiliwa,
Dhuluma huja umbua, haki ikijifungua!
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Kila mwenye kujua, ishara huziagua,
Za wakati zilokuwa, ya kale akaachia,
La, hasha akiendelea, yake huja muumbua,
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Ninachowaambia, wakati umewadia,
Mseto kufikiria, mkaepusha balaa,
Imla mkidandia, mtashuka kati ya njia,
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

Vyote mnang'ang'ania, wenzenu wataridhia?
Kidorik uwaachia, hata kidunchu kikiwa,
Hili msipotambua, uchawi mwaununua,
Raia sio watoto, ni watu na heshima zao!

YALIYOTOKEA PARIS


Wale waliojaliwa, kila kitu walitwaa,

Wakawa wang'ang'ania, kidunchu kutoachia,

Hoja wakazikataa, ndani kujitomelea,

Paris yalitokea, someni historia!

 

Tofauti zilokuwa, ni bomu waliambiwa,

Wao wakajitetea, ubepari ndio dawa,

Nusura hawakuamua, kilichobaki balaa,

Paris yalitokea, someni historia!

 

Bepari wakaamua,  vya dola kuvitumia,

Nchi ikagugumia, kwa kilio kuzuiwa,

Hadi yalipotokea, yale yasiyotarajiwa,

Paris yalitokea, someni historia!

 

Wasio nacho walia, mwneye nacho agomea,

Wingi wakautumia, ya kwao kujipatia,

Nani angewazuia, kadari kuiondoa?

Paris yalitokea, someni historia!

 

Wote walisanzulia, tena pasina silaha,

Unyongaji kuenea, Ufaransa ilokuwa,

Waloshiba kuwaniwa, kila walipokikaa,

Paris yalitokea, someni historia!

 

Paris ikajillia, hatima iliyozua,

Bepari kuondolewa, ukaingia ujamaa,

Haki ikapiganiwa, mwishowe kujisimamia,

Paris yalitokea, someni historia!

 

Muafaka nawambia, somo hili kutumia,

Huko tunakoelekea, giza ninajionea,

Kama hamtanisikia, itajaza historia,

Paris yalitokea, someni historia!

TUTUMIENI NADHARI



Wa dini pia siasa, tujifunzeni hadhari,

Ya jana si ya sasa, yameingia shubiri,

Na kwetu kubwa fursa, ni kuepusha hatari,

Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!

 

Tujipigeni msasa, kuziepusha hatari,

Na kukosa sio kosa, kosa ni kulikariri,

Maisha yasiwe mkasa, tuitumie nadhari,

Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!

 

Hakuna wa kumsusa, na kujitia kiburi,

Lazima kujitakasa, kwa wabaya na wazuri,

Vingine tukijinesa, ya heri huwa ya shari,

Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!

 

Hili adhimu darasa, maisha kutafakari,

Tukateta na kunasa, wapi tunakoabiri,

Ikiwa tunajitosa, kubaya tukahadhari,

Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!

 

Wa Yesu au Issa, wote tujenge hadhari,

Nchi isiwe ni tasa, kwenye kuzua ya kheri,

Hii ni njema fursa, kingine tusisubiri,

Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!

 

Tuufungue kurasa, wa nchi yenye hadhari,

Kujua iwe yapasa, njia yetu kukariri,

Tukaikuza hamasa, kwenye bora ushauri,

Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!

 

Msikiti na kanisa, wkaawa ni washauri,

Kila jema tukinusa, kugawa iwe ni kheri,

Ubinafsi kuususa, unazo kubwa hatari,

Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!

 

Mola hawezi kutosa, mkusanyiko wa kheri,

Kati yetu atadesa, huyo mwingi wa Saburi,

Utaifa ukanasa, nasi kuvuna mazuri,

Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!

 

kujibu si kujibu tu


Mtu mzima akiwa,  utoto huukimbia,

Hafanzi la kuambiwa, pasina kufikiria,

Kisha akafuatilia, kila analoambiwa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji akili!

 

Tafakari huzua, jambo akafikiria,

Na akisha jipimia, mizaniye humwambia,

Lipi la kuliachia, na lipi kung'ang'ania,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji busara!

 

Malau kwenye dunia, kila kona yaelea,

Ukiamua kuvua, itapinduka mashua,

Na wote mlokuwa, ndaniye kuumbuliwa,

Kuibu si kujibu tu, inahitaji hekima!

 

Hekima tunaiua, sasa kujirpokea,

Hutomjua kichaa, nani mzima akawa,

Wote sasa mnakuwa, dharau mwapalilia,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Chema walichokijua, inakuwa ni sanaa,

Watu wakajichekea, na mizaha kuidhua,

Hadhari ikififia, hatari huzidi kua,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji akili!

 

Kila mjifanya kujua, hili angeling'amua,

Daraja kujipatia, na heshima kuipewa,

Ubabe anayetitia, kiyama atutakia,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji busara!

 

Wa leo Watanzania, haki zao wazijua,

Maguvu mkitumia, hivi kimya watakaa ?

Sasa demokrasia, vingine haitakuwa,

Kuibu si kujibu tu, inahitaji hekima!

 

Nchi inahujumiwa, watu watayaridhia,

Kauli wasipotumia, ipi iwe yao silaha ?

Mwapaswa kufikiria, kwa hali zao kujua,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Kuandamana ni njia, yaitumia dunia,

Watu wanapozuiwa,  bwawa lao litajaa,

La hasira lilokuwa, hadi kingoze kung'oa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Valvu kifunguliwa, maji huweza pungua,

Tambarae kuingia, salama bwawa likawa,

Vingine haitakuwa, mnatafuta balaa,
Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!
 

Jalali namlilia, kizazi kukiokoa,

Nyota zazusha udhia, giza laanza ingia,

Tuepushe na nazaa, usanii na balaa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

piga ikijibu piga



Laiti tungelijua, sikuzote hufatia,

Ndicho kinachoendelea, hapa kwetu Tanzania,

Haambiliki kakua, nani atamsikia ?

Piga ikijibu piga, hivi nini hufwatia ?

 

Mtu mzima akiwa,  utoto huukimbia,

Hafanzi la kuambiwa, pasina kufikiria,

Kisha akafuatilia, kila analoambiwa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji akili!

 

Tafakari huzua, jambo akafikiria,

Na akisha jipimia, mizaniye humwambia,

Lipi la kuliachia, na lipi kung'ang'ania,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji busara!

 

Malau kwenye dunia, kila kona yaelea,

Ukiamua kuvua, itapinduka mashua,

Na wote mlokuwa, ndaniye kuumbuliwa,

Kuibu si kujibu tu, inahitaji hekima!

 

Hekima tunaiua, sasa kujirpokea,

Hutomjua kichaa, nani mzima akawa,

Wote sasa mnakuwa, dharau mwapalilia,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Chema walichokijua, inakuwa ni sanaa,

Watu wakajichekea, na mizaha kuidhua,

Hadhari ikififia, hatari huzidi kua,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji akili!

 

Kila mjifanya kujua, hili angeling'amua,

Daraja kujipatia, na heshima kuipewa,

Ubabe anayetitia, kiyama atutakia,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji busara!

 

Wa leo Watanzania, haki zao wazijua,

Maguvu mkitumia, hivi kimya watakaa ?

Sasa demokrasia, vingine haitakuwa,

Kuibu si kujibu tu, inahitaji hekima!

 

Nchi inahujumiwa, watu watayaridhia,

Kauli wasipotumia, ipi iwe yao silaha ?

Mwapaswa kufikiria, kwa hali zao kujua,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Kuandamana ni njia, yaitumia dunia,

Watu wanapozuiwa,  bwawa lao litajaa,

La hasira lilokuwa, hadi kingoze kung'oa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Valvu kifunguliwa, maji huweza pungua,

Tambarae kuingia, salama bwawa likawa,

Vingine haitakuwa, mnatafuta balaa,

 

Jalali namlilia, kizazi kukiokoa,

Nyota zazusha udhia, giza laanza ingia,

Tuepushe na nazaa, usanii na balaa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

 

Sunday, June 2, 2013

Sauti inapozimwa

 Ubabe ukitumika, na haki ikawa nyuma,
Hata wasipolalamika, lao kwa sana huvuma,
Hadi mbali kusikika, na kuongeza tuhuma,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Wingi usiobebeka, hauwezi kunguruma,
Sautiye hukatika, zisifike kwenye ngoma,
Masikio kuzibika, pasiwe kitu kuchuma,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Asiyetaka baraka, hatoipat hekima,
Ya kwake yatafanyika, yakaongeza hasama,
Na mbali hawataruka, balaa kuwaandama,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Ya mola yakikwazika, ya nani kuwa salama ?
Amzuiaye Rabuka, ataka yeye nguruma ?
Au anadanganyika, aipoteze neema ?
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Waoga waweweseka, wanaikosa kalima,
Wameshindwa kutamka, wakaondoa dhuluma,
Wanatutia wahaka, kama kweli twenda pema,
Sauti inapozimwa, kilio chake ngurumo!
 
Wingi uliobebeka, kesho isiwe lawama,
Mwenyewe umeyataka, twafumua unafuma,
Kwa shari anayeezeka, akilala huwa wima,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Ninalojua hakika, haki huwa inasema,
KImya kikaondoka, na hoja zake kuvuma,
Kiumbe yote ponzeka, ila si kukosa rehema,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Waasi usiye wahaka, ninaziomba huruma,
Dunia imewateka, hawajui wanazama,
Muqtadiri eleka, utakalo likapema,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!