Wa dini pia siasa, tujifunzeni hadhari,
Ya jana si ya sasa, yameingia shubiri,
Na kwetu kubwa fursa, ni kuepusha hatari,
Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!
Tujipigeni msasa, kuziepusha hatari,
Na kukosa sio kosa, kosa ni kulikariri,
Maisha yasiwe mkasa, tuitumie nadhari,
Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!
Hakuna wa kumsusa, na kujitia kiburi,
Lazima kujitakasa, kwa wabaya na wazuri,
Vingine tukijinesa, ya heri huwa ya shari,
Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!
Hili adhimu darasa, maisha kutafakari,
Tukateta na kunasa, wapi tunakoabiri,
Ikiwa tunajitosa, kubaya tukahadhari,
Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!
Wa Yesu au Issa, wote tujenge hadhari,
Nchi isiwe ni tasa, kwenye kuzua ya kheri,
Hii ni njema fursa, kingine tusisubiri,
Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!
Tuufungue kurasa, wa nchi yenye hadhari,
Kujua iwe yapasa, njia yetu kukariri,
Tukaikuza hamasa, kwenye bora ushauri,
Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!
Msikiti na kanisa, wkaawa ni washauri,
Kila jema tukinusa, kugawa iwe ni kheri,
Ubinafsi kuususa, unazo kubwa hatari,
Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!
Mola hawezi kutosa, mkusanyiko wa kheri,
Kati yetu atadesa, huyo mwingi wa Saburi,
Utaifa ukanasa, nasi kuvuna mazuri,
Tujifunzeni nadhari, viongozi Tanzania!
No comments:
Post a Comment