Friday, June 28, 2013

YALIYOTOKEA PARIS


Wale waliojaliwa, kila kitu walitwaa,

Wakawa wang'ang'ania, kidunchu kutoachia,

Hoja wakazikataa, ndani kujitomelea,

Paris yalitokea, someni historia!

 

Tofauti zilokuwa, ni bomu waliambiwa,

Wao wakajitetea, ubepari ndio dawa,

Nusura hawakuamua, kilichobaki balaa,

Paris yalitokea, someni historia!

 

Bepari wakaamua,  vya dola kuvitumia,

Nchi ikagugumia, kwa kilio kuzuiwa,

Hadi yalipotokea, yale yasiyotarajiwa,

Paris yalitokea, someni historia!

 

Wasio nacho walia, mwneye nacho agomea,

Wingi wakautumia, ya kwao kujipatia,

Nani angewazuia, kadari kuiondoa?

Paris yalitokea, someni historia!

 

Wote walisanzulia, tena pasina silaha,

Unyongaji kuenea, Ufaransa ilokuwa,

Waloshiba kuwaniwa, kila walipokikaa,

Paris yalitokea, someni historia!

 

Paris ikajillia, hatima iliyozua,

Bepari kuondolewa, ukaingia ujamaa,

Haki ikapiganiwa, mwishowe kujisimamia,

Paris yalitokea, someni historia!

 

Muafaka nawambia, somo hili kutumia,

Huko tunakoelekea, giza ninajionea,

Kama hamtanisikia, itajaza historia,

Paris yalitokea, someni historia!

No comments: