Tuesday, February 26, 2013

Atampa mlo gani

 
 
Sijaiona yakini, ninayo shaka moyoni,
Jini kuwa wetu mgeni, sijawa nayo imani,
Naugua ndanindani, wa kumwambia ni nani?
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Ijapo si Selemani, hubaini hadharani,
Namjua huyu nani, na kwenu haonekani,
Naye hajiamini, akinitia machoni,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Kuna mambo ya uani, hayawekwi barazani,
Huwa huyo afkani, kinyume anayeghani,
Hayawi ya msalani, kuyaleta sebuleni,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Mshairi mtu gani, kichwani hana maoni,
Ndivyo wanavyoamini, njia wasiobaini,
Kumbe wanajizaini, hatima yao shakani,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Mtu huyu mtu gani, humuoni kivulini,
Na tonge kwenda kinywani, kwake huwa hayumkini,
Wala kiu haioni, hata akiwa juani,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Ameniacha pembeni, simo mwake shaurini,
Hakunitaka maoni, wala mie najuani,
Yeye yuko kilingeni, hana asicho baini,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Kwa heshima ububuni, nimeingia mwandani,
Kofuli iko kinywani, jipya sintolibaini,
Ila nangaoja mwakani, yarudi ya ughaibuni,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Wengine walibaini, kwa shetani kumuamini,
Watakuwa nayo imani, na dunia kuiwini,
Hivi leo wa shakani, mbele nyuma hawaoni,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Wamebaki kujilani,  wenyewe kujizaini,
Yakawa kama utani, hawaoni tumaini,
Nchi iko nje ndani, na uchi wajibaini,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 

No comments: