LUGHA hii ni azizi, yenye kubwa manufaa,
Laiti tungemaizi, hazina tungetumia,
Ila wetu uongozi, Ukingali wasinzia,
Hasara ya Kiswahili, kaida ni kiada
hakuna.
Tipu tipu kamaizi, Kongo akenda kutua,
Biashara kwa kuenzi, Tanganyika ikapaa,
Tukayafanya majenzi,leo tunayochelea,
Hasara ya Kiswahili, Tipu tipu katushinda!
Nyumbani na pande hizi, lugha wangeitumia,
Kuuza na manunuzi, mabishano kuingia,
Vipya vizuke kwa jozi, hadi ziada ikawa,
Hasara ya Kiswahili, jirani kutozungumza.
MS watuenzi, lugha wameiandaa,
Iko katika ngamuzi, kama hujasimuliwa,
Ukiwa na vitowezi, waweza soma dunia,
Hasara ya Kiswahili, tovuti zetu
zinapwaya.
Ukafanza mamkuzi, na hali watu kujua,
Kunavyo vipeperuzi, waweza kuwarushia,
Dunia sasa pembuzi, ni kijiji imekuwa,
Hasara ya Kiswahili, unyani unatuzidi.
Twakosa maandalizi, nje kwenda palilia,
Yanazidi maongezi, vitendo vimepungua,
Bado iko kubwa kazi, ujasiriamali ikawa,
Hasara ya Kiswahili, kutotawala Afrika.
Wanangoja uwekezi, hili washindwa tambua,
Yakifanzwa ma'ndalizi, bilioni kuingia,
Kwa elimu nazo kazi, nchi kutokufulia,
Hasara ya Kiswahili, kaida ni kiada
hakuna.
Kiingereza chenye enzi, sasa chaachia
njia,
Dunia sio mjenzi, moja tu kuitumia,
Inataka mapinduzi, ndani na nje kutiwa,
Hasara ya Kiswahili, Tipu tipu katushinda!
Inataka mageuzi, asili kuichungua,
Pakawepo kikomezi, mazoea kuachia,
Ili tuipande ngazi, kule tunakotakiwa,
Hasara ya Kiswahili, jirani kutozungumza.
Lugha yataka malezi, na uwekezi kutiwa,
Kukusanya wajuuzi, mifumo kuifumua,
Tukifanza mapinduzi, vyungu viwe vimejaa,
Hasara ya Kiswahili, tovuti zetu
zinapwaya.
Tafsiri sio kazi, vikundi tukichangia,
Masomo yote asisi, tunaweza kutohoa,
Istilahi kimakuzi, mlima mkubwa ukawa,
Hasara ya Kiswahili, unyani unatuzidi.
Kwa kutumia ngamizi, vitu vyote vikatiwa,
Wakaanza mazoezi, wana shule kusomea,
Wanapopata tatizi, ufumbuzi kupatiwa,
Hasara ya Kiswahili, kutotawala Afrika.
Tukiyafanya malezi, kompyuta kutumia,
Lugha yetu tukaenzi, sana mbali kufikia,
Wenetu wana uzuzi, mengi watayagundua,
Hasara ya Kiswahili, kutotawala Afrika.
Jitihada hatufanzi, kompyuta kuwekewa,
Wakaanza mazoezi, hadi wakazizoea,
Kisha kwenye utumizi, mapya wakayavumbua,
Hasara ya Kiswahili, kutotawala Afrika.
Ukifanya uchunguzi, tofauti utajua,
Wasio na mazoezi, vijijini wamejaa,
Wao kwanza utambuzi, tivii huidhania,
Hasara ya Kiswahili, kutotawala Afrika.
Wa mjini wenye wenzi, zana wakawapatia,
Wayaweza matumizi, kila aina wajua,
Kuwatega huwa kazi, wao watakuchezea,
Hasara ya Kiswahili, kutotawala Afrika.
Tungeiacha ajizi, kompyuta kuenea,
Ili lugha kuienzi, Kiswahili kikakua,
MS ni wajuzi, hima watatufanzia,
Hasara ya Kiswahili, kutotawala Afrika.
Ninamuomba Mwenyezi, macho akatufungua,
Tukaulola na mwezi, kule unakoishia,
Ya kale tukiyaenzi, kama nyani twabakia,
Hasara ya Kiswahili, kutotawala Afrika.
No comments:
Post a Comment