Mswahili, mswahili, atumia Kiswahili,
Lugha yake ya asili, kwalo hilo si bahili,
Ajivuna kwa halali, si haramu kunakili,
Uswahili ni asili, lugha na utamaduni!
Wala sio udhalili, au kukosa akili,
Hiyo dhana baradhuli, watoa dhoofu hali,
Waliokosa akili, kwa utumwa kuwa mali,
Uswahili ni asili, lugha na utamaduni!
Ni yangu ardhilhali, iwafikie bilkuli,
Neno hili kulhali, zama zake zawasili,
Umma umeshakubali, vizuizi ni makuli,
Uswahili ni asili, lugha na utamaduni!
Katiba itafasili, na kukipandisha hali,
Vya wengine si batili, ila nafsi ya pili,
Hili lisipowasili, kuendelea muhali,
Uswahili ni asili, lugha na utamaduni!
Nilsema ni muhali, watumwa kustahili,
Historia kuwajali, kwa kutnza kiswahili,
Zama zao zimefeli, jalalani zao feli,
Uswahili ni asili, lugha na utamaduni!
Heshima ya Uswahili, kupata mzawa asili,
Lugha aisyekejeli, heshima kuwa wakili,
Cheo akikidahili, likawa hilo halali,
Uswahili ni asili, lugha na utamaduni!
Nishani kustahili, dunia kumsabili,
Halihitaji akili, linataka uhalali,
Zama hizi Kiswahili, cheo kinastahili,
Uswahili ni asili, lugha na utamaduni!
Iwe Mchina mithili, ukiitwa Mswahili,
Na uzazi ni wa mbali, si nchi kustahili,
Watatoka Rwanda kweli, na waitwe
Waswahili,
Uswahili ni asili, lugha na utamaduni!
Lugha atakayejali, ndiye awe Mswahili,
Astahili medali, japo kwao si asili,
Kina wetu bure ghali, waishie udhalili,
Uswahili ni asili, lugha na utamaduni!
Ninakuomba Jalali, tuongoze Waswahili,
Kwa lugha tuwe kamili, hadi kwenye uzamili,
Kitumike Kiswahili, kwa akheri na awali,
Uswahili ni asili, lugha na utamaduni!
No comments:
Post a Comment