Monday, February 18, 2013

BARAZA LA KISWAHILI TANZANIA

 
KIZIBAO kimekua, baraza ilivyokuwa,
Wizara limekivaa, au limeshavuliwa,
Lugha yatima ikawa, hakuna kuendelea,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Linazidi kudumaa, na wakati unapaa,
Mengi lingeyaamua, kama huru lingekuwa,
Miradi likaizua, trilioni kuingia,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Kawaida imekua, kaaburini limetiwa,
Nani alikumbukia, au hazina kujua,
Tukilichangamkia, mengi laweza kuzaa,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Tumejenga mazoea, kukazwa nazo sheria,
Ndimo tunamoishia, hatutaki kujitoa,
Watazuka wakujua, lugha mtaji ikawa,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
Mtaji twauachia, ujasiriamali kuvia,
Kwa elimu na sanaa, nchi vingelichangia,
Hata kibiashara pia, masoko yangesambaa,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Tipu tipu alijua, biashara kaanzia,
Tanganyika ikakua, hadi Kongo kuingia,
Leo ninayojionea, nje tunakuhofia,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Tunabaki kurejea, ndani tuking'ang'ania,
Mwee zabanana kuwa, si moja moja kumea,
Jopo hatujajaliwa, uchumi kufikiria,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Laiti ningelikuwa, kuna mengi ya kuzua,
Redio zinalilia, na tivii nazo pia,
Ila ninayosikia, uwezo wanafulia,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Uwezo ningelipewa, ngwee ningejikatia,
Kwa kuenzi teknolojia, na programu kuzua,
Vijana wakatulia, na vichwa kuvifungua,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Uzuzi ungelikuwa, ujasiriamali kwenea,
Kwa maabara kuanzia, ya lugha za Tanzania,
Makao makuu ya mkoa, mradi ungeanzia,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Wadau ningewambia, lugha tumeipania,
Kila njia kutumia, na vyuoni kuingia,
Na kituo cha kwanzia, cha Baraza kingekuwa,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Nimeishawaelezea, hapa ninamalizia,
Akili tukitumia, tupate la kuamua,
Lugha isipotumiwa, kwoza haitachelewa,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!
 
Manani twakulilia, lugha yetu kujalia,
Tupate kuitumia, kwa imani na dunia,
Juu tukajipandia, na kilele kufikia,
Baraza la Kiswahili, bora liwe mamlaka!

No comments: