Thursday, December 13, 2012

Z I M A M O T O


PAPO kwa papo kuamua, pasi kuwa na bajeti,
Sifa za kuserubukia, shukrani kuambua,
Watu wakasujudia, na viatu kurambia,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Hayo ya kujinyanyua, walipokwishagukia,
Wakaondoa udhia, matope kwenda ondoa,
Huruma wakajiuzia, kwenye njaa na ukiwa,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Mamlaka kuyazoa, mtu ukajilimbikia,
Ukabaki kuamua, na wengine kushangaa,
Haiwi kushangilia, ubaya ukitiokea,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Nchi inayo mikoa, kama nchi ilokuwa,
Uhuru isipopewa, nchi tutaichezea,
Mbali hatuafikia, tutaanza kupagawa,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Inatakiwa mikoa, mipango yao kuzua,
Na uongozi ridhaa, wenyewe kujichagua,
Hatua wakajipangia, wapi wataka fikia,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Dar  wakingojea, yao kuja kuamua,
Mikoa itafubaa, na riadha kufulia,
Mbali hawatafikia, kuchekwa iwe tabia,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Uchumi kuunyanyua, wakazi wanatakiwa,
Yao wakayamua, na ulua kuutia,
Kadiri wakaagua, wawezavo jinasua,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Nasaha nimeitoa, naomba hoja kutoa,
Manani akajalia, upevu kuufikia,
Nchi ni kubwa gunia, sio rahisi kujaa,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Si mshairi wa chama


UCHAMA naukataa, haki nazingatia,
Ni mwana demokrasia, pembeni aliyekaa,
Haki kuilingania, itulie mizania,
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Nateta demokrasia, izagae Tanzania,
Udikteta uchwara, chembe kutobakia,
Yale ya chama kimoya, yatoke yasiyofaa,
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Usawa naupigania, fakiri kusaidia,
Vijijii wlaiokuwa, huko kusikoangaliwa,
Hali juu kuinua, makwao kujivunia,
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Ukinitaka ubia, na wew weza ingia,
Vijijini kuingia, ya kwao tukayanoa,
Bongo tukiwapatia, kufikiri wanajua,
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Mipango ukiandaa, kusoma wanaelewa,
Mita ukiwaambia, ni kipimo wakijua,
Umbali ukiongea, wnaaweza kufikia,
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Wazo ukilichimbua, lulu wataigundua,
Haba na haba ikawa, mbele weza endelea,
Mzawa asipojifaa, hivi nani kumfaa?
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Kwenu ukiwajengea

 Kwenu ukiangalia, na kwingine saidia,
Haki kuianglaia, usawa ukatimia,
Sio huku kuchukua, kule tu ukawafa,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Mizani kusimamia, usawa kuangalia,
Haki ukashadidia, bila kitu kupungua,
Rehema mkatunukiwa, kwa dhuluma kuiondoa,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Katiba ninavyojua, ulinganifu sheria,
Pasiwe wa kuonewa, wala wa kupendelewa,
Sasa kinachotokea, mashaka kinatutia,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Kwa wapinzani huvia, tawala wakachanua,
Au swahiba pakiwa, mambo yatazinduliwa,
Kwa wengine kunapwaya, nani wa kuangalia ?
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Kwa wakubwa nasikia, ridhaa wakajengewa,
Wengine wakililia, hiyo ndoto waambiwa,
Mizani naihofia, pande inaegemea,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Wanakokupachagua, kwa wakubwa walokuwa,
Wadogo yarukwa njia, hadi mbali kuendea,
Mkubwa palipokuwa, sasa ndio huangaliwa,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Hili sijaliridhia, wala sintolliridhia,
Hofu yangu nawambia, ila ninaidhania,
Jema halitajaliwa, mabaya laja kuzua,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!


Hakuna mkamilifu


WAJA hatukujaliwa, ukamilifu kupewa,
Kiasi tunapungua, na wengi tunajijua,
Kadari hatukupewa, ya kuweza kutimia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!


Mjua mwenye kujua, sababu zake ajua,
Upungufu kutegea, kisa chake akijua,
Ukamili kabakia, kuhodhi mwenye kutoa,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Tusije kujihadaa, vingine tukadhania,
Wapambe waliokuwa, miungu kutuumbia,
Wasifu anatakiwa, Mola asiyezaliwa,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Viumbe  hatukupewa, ruhusa kujiumbua,
Kwa kelele na kuzua, yale tusiyojaliwa,
Kuridhika ndiyo njia, na kikomo kukijua,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Mwanzo wetu twaujua, ila mwisho twaotea,
Uchamungu kiingia, nalo tutakadiria,
Hapa si watu wa kukaa, hii njia  twatumia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Kwa kitambo kulijua, tutaiacha dunia,
Visa tungevipangua, na hoja kujijengea,
Hakuna wa kubakia, usawa tungenuia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Haki tungeangalia, tusende mbele kulia,
Na dhuluma kupungua, moto kutokuumbua,
Na adili kutufaa, mizani ikatimia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Fukara tungewafaa, na wala si kuulea,
Tungepiga vita njaa, na sio kuitumia,
Watu tukawanua, na mfukoni kutia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Tungelijua masaa, huwa ni yetu dunia,
Na fumba na kufumbua, hapa tunaezuliwa,
Isingekuwa ridhaa, uongo kupalilia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Umma tusingeuubia, na ufukara kuutia,
Udhibiti tungetia, haramu kuikataa,
Halali tukailea, h adi mwisho wa dunia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!


T H A W A B U

Thawabu utagawiwa, mema ukijifanyia,
Watu ukasaidia, kwa huruma kuwalea,
Bali bado sijajua, dhambi haitonizidia,
Thawabu utazipata, je, zitazidi madhambi ?

Ya nje tunayajua, ya ndani twakadiria,
Milima ukipangua, mabonde yatabakia ?
Safari naihofia, hatari nyingi zajaa,
Thawabu utazipata, je, zitazidi madhambi ?

Umbali nashuhudia, kamili sijaujua,
Na siku ya kufikia, ni hadithi imekuwa,
Mitihani imejaa, kufaulu ninagwaya,
Thawabu utazipata, je, zitazidi madhambi ?

Mitego imesambaa, unaweza kushitua,
Vipini kukuingia, na miiba usiyotoa,
Miguu ikalemaa, mbele usende tembea,
Thawabu utazipata, je, zitazidi madhambi ?

Dharau naihofia, yaweza kuniingia,
Thawabu zikatwaliwa, na mwingine kwenda pewa,
Udhaifu nikijua, waweza kuniokoa,
Thawabu utazipata, je, zitazidi madhambi ?

Wahaka waniingia, ujibari kutokea,
Utukufu nikavaa, kwa joho la kushonewa,
Na rangi nikapambiwa, kiumbe kwenye dunia,
Thawabu utazipata, je, zitazidi madhambi ?

Uovu nauhofia, usije kuniingia,
Ubaya kukusudia, kwa kisasi kujitia,
Milima hukwanguliwa, vichuguu kubakia,
Thawabu utazipata, je, zitazidi madhambi ?

Hofu inaniingia, kila  ninapowazia,
Shetani kunihadaa, rafiki nikamdhania,
Kwaye kuniongopea, mkenge nikaingia,
Thawabu utazipata, je, zitazidi madhambi ?

Kilio chako chamkera

Mgumu kuvumilia, na subira humpaa,
Kilio ukiangua, huku unaugulia,
Atauona udhia, hataki kukisikia,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Mgonjwa ukitambua, ni mgumu kujijua,
Yeye anaugulia, sio mbwembwe anatia,
Wewe ukimatania, ndugu yangu wakosea,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Waweza kumdhania, ni sanaa anatia,
Uchungu yeye ajua, vipi wewe kuujua,
Hali ungelijaliwa, hapo usingelikaa,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Mwenye njaa hugugumia, mwenye shibe kafakamia,
Vipi atamuelewa, mkosa asojaliwa,
Tumbo humngurumia, kama ndege ya Ulaya,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Chakula ajionea, ashindwa kukinunua,
Kabaki kukiangalia, kwake sasa ni sanaa,
Wamsimanga raia, mikono atanyanyua,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Palikuwa Malkia, Ufaransa nasikia,
Watu wakamwendea, mikate wanalilia,
Yeye akawashangaa, keki kutokununua,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Shilingi asiyekuwa, vipi maji 'tanunua,
Kiu humashambulia, akatamani kulia,
Mengine ukimwambia, vipi atakuelewa?
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Hatuishi kuzubaa, wnezetu kuporomoa,
Majumba yazidi ng'aa, na shani za motokaa,
Ila mfukoni balaa, senti zinatukimbia,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Haruna Kilewo mbia, zamani aliyekuwa,
Kilio akiangua, hivi sasa kafulia,
Auni aililia, wapi  pa kuingilia,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Mola tunawaombea, mliokuwa mughni,
Mkijatufikiria, tutapata afueni,
Mioyo ikatulia, tudhani tuna thamani,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Kilio chako chamkera

Mgumu kuvumilia, na subira humpaa,
Kilio ukiangua, huku unaugulia,
Atauona udhia, hataki kukisikia,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Mgonjwa ukitambua, ni mgumu kujijua,
Yeye anaugulia, sio mbwembwe anatia,
Wewe ukimatania, ndugu yangu wakosea,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Waweza kumdhania, ni sanaa anatia,
Uchungu yeye ajua, vipi wewe kuujua,
Hali ungelijaliwa, hapo usingelikaa,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Mwenye njaa hugugumia, mwenye shibe kafakamia,
Vipi atamuelewa, mkosa asojaliwa,
Tumbo humngurumia, kama ndege ya Ulaya,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Chakula ajionea, ashindwa kukinunua,
Kabaki kukiangalia, kwake sasa ni sanaa,
Wamsimanga raia, mikono atanyanyua,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Palikuwa Malkia, Ufaransa nasikia,
Watu wakamwendea, mikate wanalilia,
Yeye akawashangaa, keki kutokununua,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Shilingi asiyekuwa, vipi maji 'tanunua,
Kiu humashambulia, akatamani kulia,
Mengine ukimwambia, vipi atakuelewa?
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Hatuishi kuzubaa, wnezetu kuporomoa,
Majumba yazidi ng'aa, na shani za motokaa,
Ila mfukoni balaa, senti zinatukimbia,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Haruna Kilewo mbia, zamani aliyekuwa,
Kilio akiangua, hivi sasa kafulia,
Auni aililia, wapi  pa kuingilia,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !

Mola tunawaombea, mliokuwa mughni,
Mkijatufikiria, tutapata afueni,
Mioyo ikatulia, tudhani tuna thamani,
Kukerwa yake tabia, 'gonjwa asiyelijua !