Saturday, November 30, 2013

KUNA VICHAA WA FEDHA...


 

HABARI nimesikia, kuwa wa fedha vichaa,

Wameishajilimbikia, eti sasa wazimwaa,

Kusudi na yao nia, hakuna anayejua,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Kwa wingi zilivyojaa, kila mtu agawiwa,

Hakuna wa kuchagua, wote kwao abiria,

Lengo sijalitambua, nabakia kushangaa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Punda ingelikuwa, ngejuwa wamelemewa,

Mwenye punda achezewa, na dhihaka kufanyiwa,

Mtoni akajitia, chumvi  maji kwenda kuwa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Na wanaokusudiwa, kura wanaoshikilia,

Vyamani walimokuwa, waziwazi ni bidhaa,

Bei imeshaamuliwa, taslimu wanatoa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Karuni ninayemjua, japo wingi ulimzidia,

Bure kitu hakutoa, hadi alipofukiwa,

Hawa sijawaelewa, gia gani watumia?

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Nyumbani wazichukua, ugenini kufukia,

Kisha wanajichengua, na mikwara kujitia,

Ukiona yaelea, juwa wameazimia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Matofali wachukua, dhahabu yaliyokuwa,

Kaziye si kujengea, ila kuji9nyeshea,

Ukubwa uliokuwa, hasara kwenye dunia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Wanywa hadi kujinywea, ibilisi kakolea,

Hio waalofurahia, Mola hajafurahia,

Kicheko kilichokuwa, kilio kakitohoa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Milma waelemea, bondeni kulikouwa,

Huku juu umejaa, chini wazidi kupyway,

Na bado twatarajia,  kisiwa tutabakia ?

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Kama pombe ingekuwa, sababu ningeijua,

Wataka watu kulewa, ovyo wakajisemea,

Kisha lao wakalitwaa, pasina wao kujua,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Keki ingelikuwa, kwenye basi imekuwa,

Kisha dawa imetiwa, shabaha ningegundua,

Wanuia abiria, kwenda mbele waibia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Mimi hili sijajua, la tajiri kuwa na njaa,

Ikawa yamelvyaa, hadi chini twamzoa,

Kuna kitu sijajua, bado nakiangalia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Si wa bure ukichaa, ovyoovyo kuzigawa,

Kuna sababu na nia, ila sijaigundua,

Kofia nitaivua, kija mtu kunambia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Semeni Watanzania, haya mnayoyajua,

Vimbgwanga vyakaribia, mengi tutashuhdia,

Watu nguo watavua, sapoti kwenda kutoa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Ni wakati wa maridhia, watu kuyafikiria,

Akili wakatumiwa, si kwa moyo kuzainiwa,

Kisha wakaja kuyajutia, siku wasioitambua,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

Monday, October 14, 2013

N Y E R E R E DEI 2013


Bismillahi Jalia, mmiliki wa dunia,
Mbingu na sayari pia, tujuazo, tusojua,
Yahillahi mtambua, msafi pasipungukiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Peke wa kuabudiwa, aidha wa kutegemewa,
Mshiriki usiyekuwa, japo wakusingizia,
Daraja unayejua, waja za kuwapatia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Laiti ungelikuwa, haya ningekushtakia,
Nchini yanayoingia, na macho twayafungia,
Nchi uliowaachia, weye ungewashangaa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ibilisi katuvaa, twaiabudu dunia,
Watu miungu wakawa, na ibada kufanziwa,
Wa kutusamehea, hawezi mwingine kuwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ufahari wamejaa, nchi uliowachia,
Matumizi watumia, tajiri utadhania,
Washindwa kuvipangia, fakiri kutunasua,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Hekalu wajijengea, matembe tunakalia,
Na manyatta ndio njia, Umasaini sikia,
Ila kuna walojaliwa, vya milioni kuvaa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Nyumba wanatuvunjia, wala si kutujengea,
Mali aisli yatumiwa, ughali kutwongezea,
Nusura h atuaijua, japo tumeahidiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ibada wasiojua, migongano wanazua,
Kuchinja ulichinjiwa, na Islamu alokuwa,
Vipi wawakatalia, au visa wanavizua ?
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Udini unaingia, manabii twajaliwa,
Cheo wanajinyanyua, na njia kufaragua,
Wakuu wakawaambia,  kifalme kujiishia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Elimu twaichezea, kifaurongo ikawa,
Watasi wanakamia, wa kwao kupendelewa,
Hatarini kuigawa, nchi ulotuachia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Maji yazidi potea, na tenda zinaongea,
Masikini wafulia, walonacho kwogelea,
Shilingi yazidi kupaa, mwezini itafikia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Umeme sasa nazaa, tayari imeshakuwa,
Mashamba wajilimia, Kwa ya Mtera kumwaa,
Mengi tusiyoyajua, nani aatatuambia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Amoeba imekua, tatizo linalojizaa,
Ngomba inavyozidi kulia, viraka twaongezewa,
Nafuu inatukimbia, kilio kimebakia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Udugu wajifufua, macho tunaufumbia,
Wakubwa inapokuwa, hatuna la kuongea,
Kisirani inakuwa, wazidi kujichimbia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Vyama vimeingiliwa, na hasidi na nazaa,
Vyao wanajifanzia, wapendalo huamua,
Waviza demokrasia, ya kwao kufanikiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !
makundi

Yabanwa demokrasia, na ndondocha walokuwa,
Vyumbani waliotiwa, misumari kupigiliwa,
Kisha kwa kukosa hewa, weupe hugeukia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ukabila wa siasa, nchini umeshaingia,
Wachache wajiteua,  ya wengi wakafukia,
Anayejifaragua, uhaini atatiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ukubwa twauchukua, ila maendo yavia,
Nyuma vile twarejea,  kilichopo kupotea,
Upya tunayaanzia, hata yaliyotangulia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ufisadi umetua, nani aje kuung'oa,
Manake una wafaa, wajuao wanajua,
Kulalama sijajua, mabomu nayahofia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Twatakiwa kunyamaa, ukweli kuufukia,
Kulaumu si sheria, hakiye yachukuliwa,
Twatakiwa vumilia, lolote tukitendewa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Maguvu sasa ni njia, wenye nayo watumia,
Fedha nayo sasa pia,  imeshapewa sheria,
Kama nayo sipokuwa,  haki inanunuliwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Madini yachimbuliwa, hata na gesi nayo pia,
Swali lisilojibiwa, hivi nani kumfaa,
Ni wengi itajakuwa, au ndugu na jamaa?
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Twahofia kutokea, kama kule Nigeria,
Na JIneikwatoria,  ambako zabanjuliwa,
Wakuu wakaogelea, hadi wa chini wafulia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Wazawa wasimuliwa, thamani yaondolewa,
Maisha juu yapaa, hali chini wadumaa,
Wataipataje furaha, inashangaa dunia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Imani zimeachiwa, mikingamo kuingia,
Wa chini juu akawa, ya wengine kuamua,
Ndio wakajisemea, ya wakuu wasokuwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Mengi waliahidiwa, dirishani yatokea,
Mlangoni yazuiwa, ngangari yanashupaa,
Musuli zikishakuwa, za akili kutanua,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Mipango twaihofia, kinyume yakaakaa,
Ya mbele yanakosewa, ya nyuma yakafatia,
Kipaumbele chavia, shamba na mjini pia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Si vyema haijawa, mikakati Tanzania,
Mifumo tunafumua, badala kujishonea,
Watu wajiamlia, jinsi wanavyosikia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Uimla twauzua, utakuja tuumbua,
Na kwenye hii dunia, tuishio kwa kupaa,
Yallahi twakulilia, baa kutuepushia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Vijiji vinadumaa, vile ulivyotuachia,
Laiti ungerejea, Mwalimu ungeshangaa,
Maktaimu vinatia, na watu washangilia ?
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Kinamama wanalia, shamba wanasahauliwa,
Wateta wawanyapaa, wa mjini wanabebwa,
Wataacha nyong'onyea, na uzee kuingia ?
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Mshairi achukiwa, kwenye  yako Tanzania,
Sasa wamnyanyapaa, kwa uongo kukataa,
Kweli akapigania, watu macho kufungua,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Maisha yetu ya jaa, uleo yamechelewa,
Wanayoyafikiria, sio yanayotakiwa,
Na wanayoyaamua, tafiti zake ukiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Arijojo imekuwa, mengi yanajiendea,
Ila inapokuwa, maandamano kung'oa,
Na machinga kusanzuliwa, na vyao  vikaharibiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Hoi demokrasia, dripu imeekewa,
Spitali yatibiwa, unyafuzi wazidia,
Katibani kuingia, mengi sana yapunguwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Katiba twaililia, mbali ikatuchukua,
Tusiwe wa kudumaa, kwa uoga kutwingia,
Mola tunokusudia, yote ungeyajalia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Wachache wapigania, ya kwao kufanikiwa,
Ya wengine kutibua, kwa nguvu au ridhaa,
Hatari twajionea, ujanja ukizidia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Latifu mhimidiwa, ipokee yangu dua,
Batili kuiondoa, ya haki yakabakia,
Haramu kuicheua, halali ikasalia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Tamati nimefikia, mbele sintoendelea,
Miye kusahauliwa, ni haki nimeridhia,
Ila ninayowambia, haya mngeyachukua,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

makillla
Nyerere Dei, 2013.

UKIZIDISHA UCHOYO


Angalia historia, toka utoto wakiwa,
Shuleni tulipokuwa, dishi walilivamia,
Kingi wakajimegea, kidunchu kikabakia,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Chuoni tumeingia, sasa ninakumbukia,
Shimoni kulimokuwa, chakula tukigombea,
Mara mbili warejea, ngwini tulipokaangiwa,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Yaendelea tabia, ukubwani kuingia,
Nchi wanajimegea, wengine kutogeea,
Nafsi yawachezea, kumg'ang'ania dunia,,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Ila ninayahofia, walivyochoka raia,
Furaha yawakimbia, na hasira kuwajaa,
Kulipuka ndio njia, nalilia Tanzania,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Tuidhibiti tabia, yenye wingi wa tamaa,
Ovyo kujilimbikia, hata kwa yasiyotufaa,
Yataja tutumbukia, tukabaki tunalia,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Mmoja tungeanzia, mitaani kuingia,
Makubwa hayajakuwa, matatizo Tanzania,
Madogo yanayokuwa, tusiache kutatua,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Upofu tukijitia, twampa shoka kichaa,
Wana na wanaofatia, salama hawatakuwa,
Mbegu tutajipandia, ya hasama na adawa,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Uchoyo ukizidia, kupendwa haitakuwa,
Watu watakuchukiya, na unafiki kutia,
Ilhali wazomewa, udhani washangiliwa,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Rafiki watakimbia, mwenyewe ukabakia,
Ikawa wao umbeya,  tadi kuiongelea,
Mengi wakakupakia, weye usiyechukua,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Kama kuna majaliwa,  hili nisingejaliwa,
Riziki ningeachia, kila mtu kujaliwa,
Yangu nikawagawia, tunu kwenda zawadiwa,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

MNAPOKUWA SHULENI, VYUONI


WENGI nimeuliziwa, waliokuwa vipenzi,
Rafiki wa kutulia, tusofendana ajizi,
Habari nikaambiwa, dongo halikuwaenzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Najua wa chekekechea, wamerdi kwa Mwenyezi,
Jichoni sikuwatia, nilipoianza kazi,
Taarifa sikupewa, si za jana si za juzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Msingi na huko pia, tumepishana kwa ngazi,
Peter alishapotea, na Ummy naye ni wa juzi,
Sasa ninasimuliwa, na hata wangu wanafunzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Sekondari tulijaa, pasina ya kizuizi,
Milango tulotumia, ya shule ile Mawenzi,
Wameondoka mamia, na kujua si wajuzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Chuo kikuu najua, kwa hesabu siiwezi,
Waliojiondokea, kina kazi kikotezi,
Sammy analialia, ya Freddy, Mboya vipenzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Rafiki aliyekuwa, na pili ni mkufunzi,
Dunia yatuhadaa, ila yake hatuwezi,
Lati tungelijua, mambo yepi ya kuenzi ?
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Ukaribu tusokuwa, tumuachia Mwenyezi,
Siri zake azijua, mapenzi hatuyawezi,
Huenda kwa kuandikiwa, zikabaki simulizi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Mola namwangukia, aliye wetu mlinzi,
Hao walotangulia, kuwapa njema hifadhi,
Viwango anavijua, hilo kwangu mwanafunzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

KIKULACHO


Kwanza 'ngejiangalia, vizuri kujichungua,
Wa nje kutosingizia, masahibu wakutia,
Pengine hujatambua, ndaniyo aweka kuwa,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

Labda keshakuingia,  kwa mithili yake chawa,
Kwenye nywele kaingia, pango keshalilipia,
Anasa ajifanzia, rusha roho azizua,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

Stihizai hutia, wengine ukadhania,
Shere akautezea, jirani kusingizia,
Ila yatakustua, kung'atwa ukigundua,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

Damu anajinyonyea, kuwanda akazidia,
Wewe unapalilia, yeye anajivunia,
Au ng'ombe umekuwa, kaziye kukukamua,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

Yako unaharibikiwa, yake yanasimuliwa,
Kichinichini ikawa, kitu hautosikia,
Husema amepatia, mahala kashikilia,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

Utamu kashikilia, hawezi kupungukiwa,
Ila niavyotambua, kuna siku yaingia,
Nywele ukijakunyoa, atakosa pa kukaa,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

USIMSOGELEE


HATA dadayo akiwa,  simsogelee mnafiki,
Stara hajajaliwa, rohoye ni mamluki,
Ndarahima adhania, Mola wake wadhihaki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Kiumbe ninakataa, hajawa naye rafiki,
Kazi yake kfukua, udhaifu kuulaki,
Kisha akakufanzia, ya kuja kutaharuki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Kifo atakuombea,  ami wa kindakindaki,
Huku anakutekea, nawe wampa malaki,
Au unalomfaa, pasina nayo mikki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Dhiki atakuombea, njiani ije kulaki,
Kadri unavyofulia, furaha haimtoki,
Yake yakiogelea, kuzama  yako huafiki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Usoni hukuchekea, hali moyoni ni chuki,
Hutaka kumalizia, ya uimbeya kuafiki,
Kisasi akakitia, msingi kisichonaki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Pagani ninakwambia, bora yake mnafiki,
Kisomo hajakijua, nafsi ingeafiki,
Dua ukimuombea, hudumu kwa urafiki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Dini hukurubia, mwisho akaiafiki,
Ashaduu akatia, akapendezwa Mulki,
Ila ninalikataa, hayawezi mnafiki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

P U L I Z O



Upepo ukilitia, kwa kiasi hufumuka,
Hupanuka likajaa, na viungo kuitika,
Usipolishikilia, juu laweza chomoka,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Arijojo hukimbia, kwenda lisikokutaka,
Wahaka ukakujaa, hali unaweweseka,
Huwezi likimbilia, si kiumbe wa kupaa,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Jua litaliachia, hali mahala kufika,
Hari ikishazidia, kawaida kufumuka,
Na viumbe wanajua, jambo hili la hakika,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Hawataki kusikia, ukawatia mashaka,
Ya kwao yakasinyaa, waendako kutofika,
Wanaipenda hadaa, kwa kuzua na kuzuka,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Juu wanaidhania, furaha imefichika,
Nini utawaambia, wasiache kuteseka,
Ukichaa inakuwa, eti ni shani kuzuka,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Mbio wanazitimua, haraka wapate fika,
Ushindani kuutia, hata pasipotakika,
Malaika wavizia, nani wataoanguka,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Kamba wameshazitia, na viuzi kuviweka,
Kuruka asiyejua, huenda akateguka,
Pumzi wanaoishiwa, hao mabli kutofika,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Hii halina ngekewa, kadara yahitajika,
Kila asiyeijua, haiwezi nunulika,
Bure unajisumbua, akiba ungeiweka,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Kalamu naiachia, hapa ninapumizka,
Siwezi ya kukimbia, kutembea natosheka,
Umri nikiongezewa, ukweli kudhihirika,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !