Thursday, May 30, 2013

Kila muabudu mtu


Wakizuka nakwambia, waabuduji wakawa,

Watu wawatangulia, na ibada kuwafanyia,

Tambua bado wazua, trela wameanzia,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

 

 

Kichuguu wachukua, wao mlima walilia,

Mlango wa kupitia, lazima pa kuanzia,

Budi mtu  kuchezewa, kttu asiyetambua,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

 

Wao wakajiandaa, uungu kuununua,

Wafanye ya kushtua, wakatingisha dunia,

Na uliyewaachia, ukaja kuyajutia,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

 

Milango yafunguliwa, muda haujaishia,

Toba kuikimbilia, maghufira kiuyajua,

Ibilisi kumkataa, na mbali ukamlania,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

 

Mtu wa kuabudiwa, apaswa awe raia,

Kwa shidaye kuijua, na  tatizo kutatua,

Hakika ninawaambia, Mola hapo mtamjua,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

 

Vingine mwamchezea, hasiraye ikakua,

Kidogo kilichokuwa, mlima kugeuziwa,

Viumeb mwachanganyikiwa, si miaka mna saa,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

Kila mkweza ukubwa



Ukimuona raia, debe anajipigia,

Mkubwa kumnyanyua, hadi awe nazo mbawa,

Huyo ukimchungua, siriye utaijua,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Yazusha yetu dunia, mitume wa kuamua,

Cheo wakajitwalia, na karama kununua,

Kisha wakaja chipua, mithili yake maua,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Huyo ukimuangalia, ukubwa aulilia,

Na njiaye ya kupitia,  mkubwa kwanza kupewa,

Kisha aje kufatia, apewe alichopewa,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Hawa watu wa tamaa, waidanganya dunia,

Ndivyo wanavyofikiria, kumbe la hasha waugua,

Yumkini ukichaa, tena wa kuchanganyikiwa,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Waishi kwa kupagawa, na ushindani kuzua,

Wa ovyo ulokuwa, kufuru unaotia,

Hakika nawaambia, washindwe na kulegea,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Fakiri wetu walia, makubwa twende vamia,

Gari ukijitolea, mafutaye pia lipia,

Tana karne ikiwa, vyema zaidi itakuwa,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Na ndege nayo pia, kwa papo hapo ingia,

Kwingine kutotokea, hili ukalitambua,

Zusha ya kuhurumia, usizushe ya kuonea,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Wahurumie izaya, Muumba wetu radhia,

Dhambi wanaopalilia, kwa pepo kuwaingia,

Kama kipepeo kuwa, kula bila cha kuzaa,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Umenipata ukiwa, wangu nawafikiria,

Dhehebu nalikimbia, masoni weshaingia,

Salama nawaambia, ya kwao kuwaachia,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

 

Maji yakizidi unga


Mafundi wakizidisha, leseni wakazitoa,

Cheti wenzi kupandisha, na unafiki kuvaa,

Huja panako mkesha, chungu chote kufuaa,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

 

Vyeo wanavyovikosha, kwa hisani kuzitia,

Kiasi wakazidisha, hadi wakakanyagia,

Huyatatiza maisha, na kuongeza nazaa,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Ya ovyo watayazusha, hadi vyumba vikajaa,

Kila ukikitingisha, kibiriti kinapwaya,

Huja sasa yakuwasha, kujikuna kukakua,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Mwanziishi wa rabsha, si anayekataliwa,

Ila anayetoa rushwa, ziada akajaziwa,

Siasa zikaharisha, na kwacha harufu mbaya,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Mengine ya kuchekesha, kiumbe anayozua,

Ajitikwa ya kutisha, kama kubeba dunia,

Kumbe muosha hukoshwa, bado hajayaelewa,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Angazieni maisha, haya yangu kuyajua,

Kuna mikasa yachosha, na vitendo vya udhia,

Watu vinawewesesha, haki yao kutojua,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Mirija waiboresha, wachache kuyakamia,

Maji wakayapitisha, ya malaki sio mia,

Hali haijawawezesha, mpito utapasua,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Mita waziviringisha, maudhui kurejewa,

Hii yaanza yavusha, na nyingine zafatia,

Hilo hilo likijsaa, watu watajiepusha,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Makundi yatutingisha, yao yakikataliwa,

Nani wa kuwawezesha, ikiwa watindikiwa,

Kauli zingine zachosha, humpa mtu kuugua,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Hukuambia maisha, na lingine halijawa,

Nakataa ni kuzusha, mtakuja changanyikiwa,

Vitendo vya kubabaisha, sumu yake kuchukiwa,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Tamaa lakukatisha, patupu kuambulia,

Hata kama umekesha, usambe  na ya jana njaa,

Na wala hukuendesha, ila umetumikia ?

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

 

 

Monday, May 27, 2013

MTAKUJA ENDA NA MAJI


Ujinga ukisikia, ni wengine kuachia,

Wao wakajifanyia, wanayoyakusudia,

Wenyewe yakawafaa, patupu ukaambulia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

mtakuja kwenda na maji !

 

Fakiri ukiambiwa, tambua walanguliwa,

Wengne kujichumia, na weye ukajikwaa,

Wao wakaendelea, nyuma wenye kubakia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Chini wa kukanyagiwa, hadhi mngeliijua,

Ndio juu mlokuwa, iwapo mnajijua,

Ila msipojitambua, mtazidi kuonewa,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

Kuongoza ni hidaya, watu wakatumikiwa,

Haijawa, haitakuwa, ubaba kuuchukua,

Kisha kujiamlia, jinsi mnavyojisikia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Hili mkilitambua, maswali mtayazua,

Katibani kuingia, cheo mkajilindia,

Ila mkipuuzia, mwauzwa kwenye gunia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

KIswahili mkitumia, kila kitu mtajua,

Hata na hizo sheria, hakuna wa kupindua,

Machale  huwaambia, stopu mkendaitoa,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Mijini mkiyajua, wenyewe mtaamua,

Huko mikoani pia, na kwenye hizo wilaya,

Uongozi mtatia, muwezao kuuchaagua,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

Njia ya demokrasia, ni ya wengi kuamua,

Wachache wakiamua, huwa wavunja sheria,

Ni budi kuwaodnoa, wenye haki kuwatia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Muda itatuchukua, ila huko twafikia,

Hata wanaozuia, patupu wataambulia,

Mkiamka Tanzania, Afrika itakuwa,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

Na  lugha hii rupia, yafaa kiuitumia,

Kanuni tukazitia, na mifumo kuizua,

Juu juu kutembea, ikatuona dunia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

 

MWANA AKIJIFANZA BABA


Mwana cheo amepewa, na ubaba kachukua,

Sasa ataka amua, na ye akaabudiwa,

Ubaba kumnyanyua, kusiko akafikia,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Baba aliposinzia, kakuta kahujumiwa,

Mwana kitini kakaa, na ukubwa kujitia,

Subira inatakiwa, sio baba kumwambia,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Haki hajatutendea, ya kwetu kuyavamia,

Cheo alichopewa, ubaba hakijamwachia,

Ubaba unabakia, wananchi wa Tanzania,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

Kawaida inakuwa, mwana kazi kulelewa,

Akishapiga hatua, hekima akaijua,

Ndipo anapoachiwa, mengine kushughulikia,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Mwana ndio anakuwa, ukubwa ang'ang'ania,

Nchi chini juu yawa, na mengi kuhujumiwa,

Kisa kinachotokea, mwana nchi keshapewa,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Uttoo bado wanukia, vipi atayoamua,

Sana hujipendelea, chote akajimegea,

Chakula tukaishiwa, tubaki kupigania,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Nidhamu ataka pewa, na utu kuutambua,

Dunia hii ni njia, si pahala pa kukaa,

Katika kujipitia, wote wakaangaliwa,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Heshima inatakiwa, kwa wa juu na chini pia,

Kule unakopuuzia, ndiko nyufa hutukia,

Birika tundu kitiwa, kamwe haiwezi jaa,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Majidi twamwachia, macho akawafungua,

Ukweli wakatambua, na kujirudi tabia,

Wakiivunja ubia, na hisani hupotea,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

 

Kulinda uhuru


Siandiki wa leo, watu wasiojijua,

Nawaandikia wajao, macho wataofungua,

Dhahiri wakaijua, na giza kuliondoa,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Havitakiwi kupungua, mizani ikitumiwa,

Kwa kadiri vyatakiwa, pasipo kufililia,

Wala ya kuongezewa, kwa kisichokusudiwa,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Haki watu kutendewa, ni dhuluma kuondoa,

Aliyeishapunguziwa, kiasi akafidiwa,

Mizani kati kukaa, kila mtu akajua,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Inapozidi hadaa, mambo itayapindua,

Kichwa chini kuja kaa, na miguu juu kwelea,

Kinyamkela kikaa, vitu juu kusombea,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Ukweli ukiuliwa, jamii yatima huwa,

Mengi yakahasiriwa, na imani kupotea,

Na mwisho wa siku ikawa, amani imeuawa,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Hakuna aliye njia, mlango wa kupitia,

Hadi mtu kujitia, ndiyo yeye kaizaa,

Amani mama tabia, kama mbaya hupotea,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Hutoweka na  kwishia, ukiwa ikawaachia,

Mkawa wa kujijua, na vijembe kufifia,

Jibari walojitia, haraka wakasinyaa,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

 

Monday, May 13, 2013

Upofu wa roho na moyo

WENGI hutatizika, upofu kiwaingia,
Roho ikadahaika, kwa upofu kuivaa,
Mengi sana kutamka, kwa ulimi kupotoa,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Moyo unaghilibika, kwa kutafuna tamaa,
Joho silo kujivika, lifaalo kuvaliwa,
Nafsi kutaabika, lawama inayojua,
Kitu ki'kupa upofu, udhibiti moyo wako !

Kimali nafilisika, ila roho yanambia,
Ukwasi umeishika, yanitaka kutulia,
Tena kutohangaika, lijalo kulingojea,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Vipofu wakiiongoka, na viziwi kusikia,
Taharuki wakataka, na hatua kuchukua,
Na ngao zikatumika, kama kinga kuzuia,
Kitu kitia upofu, udhibiti moyo wako !

Yawezayo kuwafika, mbali wakafukuzia,
Wenye tamaa  kuzika, sahau ikaingia,
Na wanaostahika, umma wakaangalia,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Hofuni wenye shirika, yao wanayoyazua,
Uchu unapowashika, hadi watume wakawa,
Na vyeti wakavipoka, na utu kuuhadaa,
Kitu kitia upofu, udhibiti moyo wako !


Kwa nyuma wakiwapoka, na mbele kuwagawia,
Wanafiki wastahika, kuangalia yafaa,
Wana yao wayashika, sio yenu kuyajua,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Watu hawa wa mashaka, ndio waliosambaa,
Njia zote wazifika, wapitao kuwavaa,
Lao halijagungulika, na wengi wapopolewa,
Kitu kitia upofu, udhibiti moyo wako !

Zao zinasambazika, mifuko yafunguliwa,
Ili mpate tatizika, na wehu mkaingia,
Ikawa mnaotamka, lile msilolojua,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Ikawa mwahamanika, kimakosa kuamua,
Ibilisi kumshika,Mola mkamuachia,
Kisha aje kuwazika, ilhali mwapumua,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Yangu kuja kutajika, hali mmeishapotea,
Na nchi kuhairibika, na watu wakalaniwa,
Usiya asiyeushika, hedaya yake balaa,
Kitu ki'kupa upofu, udhibiti moyo wako !