Monday, May 27, 2013

MTAKUJA ENDA NA MAJI


Ujinga ukisikia, ni wengine kuachia,

Wao wakajifanyia, wanayoyakusudia,

Wenyewe yakawafaa, patupu ukaambulia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

mtakuja kwenda na maji !

 

Fakiri ukiambiwa, tambua walanguliwa,

Wengne kujichumia, na weye ukajikwaa,

Wao wakaendelea, nyuma wenye kubakia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Chini wa kukanyagiwa, hadhi mngeliijua,

Ndio juu mlokuwa, iwapo mnajijua,

Ila msipojitambua, mtazidi kuonewa,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

Kuongoza ni hidaya, watu wakatumikiwa,

Haijawa, haitakuwa, ubaba kuuchukua,

Kisha kujiamlia, jinsi mnavyojisikia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Hili mkilitambua, maswali mtayazua,

Katibani kuingia, cheo mkajilindia,

Ila mkipuuzia, mwauzwa kwenye gunia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

KIswahili mkitumia, kila kitu mtajua,

Hata na hizo sheria, hakuna wa kupindua,

Machale  huwaambia, stopu mkendaitoa,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Mijini mkiyajua, wenyewe mtaamua,

Huko mikoani pia, na kwenye hizo wilaya,

Uongozi mtatia, muwezao kuuchaagua,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

Njia ya demokrasia, ni ya wengi kuamua,

Wachache wakiamua, huwa wavunja sheria,

Ni budi kuwaodnoa, wenye haki kuwatia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Muda itatuchukua, ila huko twafikia,

Hata wanaozuia, patupu wataambulia,

Mkiamka Tanzania, Afrika itakuwa,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

Na  lugha hii rupia, yafaa kiuitumia,

Kanuni tukazitia, na mifumo kuizua,

Juu juu kutembea, ikatuona dunia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

 

No comments: