Monday, May 13, 2013

Upofu wa roho na moyo

WENGI hutatizika, upofu kiwaingia,
Roho ikadahaika, kwa upofu kuivaa,
Mengi sana kutamka, kwa ulimi kupotoa,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Moyo unaghilibika, kwa kutafuna tamaa,
Joho silo kujivika, lifaalo kuvaliwa,
Nafsi kutaabika, lawama inayojua,
Kitu ki'kupa upofu, udhibiti moyo wako !

Kimali nafilisika, ila roho yanambia,
Ukwasi umeishika, yanitaka kutulia,
Tena kutohangaika, lijalo kulingojea,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Vipofu wakiiongoka, na viziwi kusikia,
Taharuki wakataka, na hatua kuchukua,
Na ngao zikatumika, kama kinga kuzuia,
Kitu kitia upofu, udhibiti moyo wako !

Yawezayo kuwafika, mbali wakafukuzia,
Wenye tamaa  kuzika, sahau ikaingia,
Na wanaostahika, umma wakaangalia,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Hofuni wenye shirika, yao wanayoyazua,
Uchu unapowashika, hadi watume wakawa,
Na vyeti wakavipoka, na utu kuuhadaa,
Kitu kitia upofu, udhibiti moyo wako !


Kwa nyuma wakiwapoka, na mbele kuwagawia,
Wanafiki wastahika, kuangalia yafaa,
Wana yao wayashika, sio yenu kuyajua,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Watu hawa wa mashaka, ndio waliosambaa,
Njia zote wazifika, wapitao kuwavaa,
Lao halijagungulika, na wengi wapopolewa,
Kitu kitia upofu, udhibiti moyo wako !

Zao zinasambazika, mifuko yafunguliwa,
Ili mpate tatizika, na wehu mkaingia,
Ikawa mnaotamka, lile msilolojua,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Ikawa mwahamanika, kimakosa kuamua,
Ibilisi kumshika,Mola mkamuachia,
Kisha aje kuwazika, ilhali mwapumua,
Mtu kipata upofu, irejee roho yako !

Yangu kuja kutajika, hali mmeishapotea,
Na nchi kuhairibika, na watu wakalaniwa,
Usiya asiyeushika, hedaya yake balaa,
Kitu ki'kupa upofu, udhibiti moyo wako !




No comments: