Monday, May 27, 2013

MWANA AKIJIFANZA BABA


Mwana cheo amepewa, na ubaba kachukua,

Sasa ataka amua, na ye akaabudiwa,

Ubaba kumnyanyua, kusiko akafikia,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Baba aliposinzia, kakuta kahujumiwa,

Mwana kitini kakaa, na ukubwa kujitia,

Subira inatakiwa, sio baba kumwambia,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Haki hajatutendea, ya kwetu kuyavamia,

Cheo alichopewa, ubaba hakijamwachia,

Ubaba unabakia, wananchi wa Tanzania,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

Kawaida inakuwa, mwana kazi kulelewa,

Akishapiga hatua, hekima akaijua,

Ndipo anapoachiwa, mengine kushughulikia,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Mwana ndio anakuwa, ukubwa ang'ang'ania,

Nchi chini juu yawa, na mengi kuhujumiwa,

Kisa kinachotokea, mwana nchi keshapewa,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Uttoo bado wanukia, vipi atayoamua,

Sana hujipendelea, chote akajimegea,

Chakula tukaishiwa, tubaki kupigania,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Nidhamu ataka pewa, na utu kuutambua,

Dunia hii ni njia, si pahala pa kukaa,

Katika kujipitia, wote wakaangaliwa,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Heshima inatakiwa, kwa wa juu na chini pia,

Kule unakopuuzia, ndiko nyufa hutukia,

Birika tundu kitiwa, kamwe haiwezi jaa,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

Majidi twamwachia, macho akawafungua,

Ukweli wakatambua, na kujirudi tabia,

Wakiivunja ubia, na hisani hupotea,

Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?

 

 

No comments: