Mwana cheo amepewa, na ubaba kachukua,
Sasa ataka amua, na ye akaabudiwa,
Ubaba kumnyanyua, kusiko akafikia,
Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?
Baba aliposinzia, kakuta kahujumiwa,
Mwana kitini kakaa, na ukubwa kujitia,
Subira inatakiwa, sio baba kumwambia,
Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?
Haki hajatutendea, ya kwetu kuyavamia,
Cheo alichopewa, ubaba hakijamwachia,
Ubaba unabakia, wananchi wa Tanzania,
Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?
Kawaida inakuwa, mwana kazi kulelewa,
Akishapiga hatua, hekima akaijua,
Ndipo anapoachiwa, mengine kushughulikia,
Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?
Mwana ndio anakuwa, ukubwa ang'ang'ania,
Nchi chini juu yawa, na mengi kuhujumiwa,
Kisa kinachotokea, mwana nchi keshapewa,
Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?
Uttoo bado wanukia, vipi atayoamua,
Sana hujipendelea, chote akajimegea,
Chakula tukaishiwa, tubaki kupigania,
Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?
Nidhamu ataka pewa, na utu kuutambua,
Dunia hii ni njia, si pahala pa kukaa,
Katika kujipitia, wote wakaangaliwa,
Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?
Heshima inatakiwa, kwa wa juu na chini
pia,
Kule unakopuuzia, ndiko nyufa hutukia,
Birika tundu kitiwa, kamwe haiwezi jaa,
Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?
Majidi twamwachia, macho akawafungua,
Ukweli wakatambua, na kujirudi tabia,
Wakiivunja ubia, na hisani hupotea,
Mwana akiwa ni baba, baba atakuwa mwana ?
No comments:
Post a Comment