Monday, May 27, 2013

Kulinda uhuru


Siandiki wa leo, watu wasiojijua,

Nawaandikia wajao, macho wataofungua,

Dhahiri wakaijua, na giza kuliondoa,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Havitakiwi kupungua, mizani ikitumiwa,

Kwa kadiri vyatakiwa, pasipo kufililia,

Wala ya kuongezewa, kwa kisichokusudiwa,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Haki watu kutendewa, ni dhuluma kuondoa,

Aliyeishapunguziwa, kiasi akafidiwa,

Mizani kati kukaa, kila mtu akajua,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Inapozidi hadaa, mambo itayapindua,

Kichwa chini kuja kaa, na miguu juu kwelea,

Kinyamkela kikaa, vitu juu kusombea,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Ukweli ukiuliwa, jamii yatima huwa,

Mengi yakahasiriwa, na imani kupotea,

Na mwisho wa siku ikawa, amani imeuawa,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Hakuna aliye njia, mlango wa kupitia,

Hadi mtu kujitia, ndiyo yeye kaizaa,

Amani mama tabia, kama mbaya hupotea,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

Hutoweka na  kwishia, ukiwa ikawaachia,

Mkawa wa kujijua, na vijembe kufifia,

Jibari walojitia, haraka wakasinyaa,

Haki, kweli na usawa, budi kulinda  uhuru !

 

 

No comments: