Thursday, December 13, 2012

Dharau siichukii

 JUU walishanzia, thamani wakanitoa,
Wageni wakiingia, sithaminiwi wajua,
Wao kinachafia, aitivii inakuwa,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Hadhi sijathaminiwa, na hali waichimbua,
Heri wamejigawia, makiwa kunigawia,
Hawapo kuninyanyua, ila kunishindilia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Yao wanafatilia, kwa karibu kwangalia,
Doti wanaitambua, hadi nukta kulea,
Hawawezi kuachia, cha kwao kikapotea,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Vya wengine hubeua, udhalili kuvitia,
Kisha wakavitifua, kama wasipotumia,
Yatima kumuibia, kisha utumwa kumtia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Jadi yangu kufulia, wengine kusaidia,
Ni jiwe kukanyagia, ng'ambo kwenda kuvukia,
Heshimake naijua, kingine sintolilia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Sawa wote tungekuwa, isingekalika dunia,
Kipawa ukijaliwa, si wote watapewa,
Wewe unayoyajua, vipi wao kuyajua,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Leo hii waijua, ghaibu wameshafulia,
Hapa ndipo hudhania, huwa mwanzo kuishia,
Wewe unalielewa, maisha yaendelea,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Ni hatua kupitia, mwisho hatujafikia,
Wengi inawazudua, wakadhani wametua,
Kisha wakajifanyia, ya dhuluma na izaya,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Yarabi nakusifia, mjua mwenye kujua,
Macho umenifungua, kuiona yangu njia,
Zaidi sintolilia, ila kuniangalia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Dharau siichukii

 JUU walishanzia, thamani wakanitoa,
Wageni wakiingia, sithaminiwi wajua,
Wao kinachafia, aitivii inakuwa,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Hadhi sijathaminiwa, na hali waichimbua,
Heri wamejigawia, makiwa kunigawia,
Hawapo kuninyanyua, ila kunishindilia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Yao wanafatilia, kwa karibu kwangalia,
Doti wanaitambua, hadi nukta kulea,
Hawawezi kuachia, cha kwao kikapotea,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Vya wengine hubeua, udhalili kuvitia,
Kisha wakavitifua, kama wasipotumia,
Yatima kumuibia, kisha utumwa kumtia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Jadi yangu kufulia, wengine kusaidia,
Ni jiwe kukanyagia, ng'ambo kwenda kuvukia,
Heshimake naijua, kingine sintolilia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Sawa wote tungekuwa, isingekalika dunia,
Kipawa ukijaliwa, si wote watapewa,
Wewe unayoyajua, vipi wao kuyajua,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Leo hii waijua, ghaibu wameshafulia,
Hapa ndipo hudhania, huwa mwanzo kuishia,
Wewe unalielewa, maisha yaendelea,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Ni hatua kupitia, mwisho hatujafikia,
Wengi inawazudua, wakadhani wametua,
Kisha wakajifanyia, ya dhuluma na izaya,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Yarabi nakusifia, mjua mwenye kujua,
Macho umenifungua, kuiona yangu njia,
Zaidi sintolilia, ila kuniangalia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

k u p a l i l i a


ZA dini zilizokuwa, na ukabila kutia,
Kwao kupalilia, magugu kwetu kwotea,
Tunashindwa kwelewa, nini chapaliliwa ?
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Siri hatujaijua, sinema twajionea,
Wahariri wakatia, kurasa isotakiwa,
Na tivii kutumia, na haja pasipokuwa,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Papi pasipougua, kwetu hapa Tanzania,
Kumoja kukatibiwa, na kwingine kuchiwa,
Kadari kama ikiwa, hilo basi naridhia,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Ila ninayoyajua, cheo si kupendelea,
Kwenu ukawajengea, wengine wakafulia,
Neema ukaigawa, jinsi unavyojisikia,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Imani ukazigawa, hawa ukasaidia,
Wengine ukawaambaa, na ya kwao kupuuzia,
Mioyo hufa hisia, na upendo kupotea,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Mbegu mlizochukua, ardhi yazikataa,
Mkilazamisha wakiwa, wanawenu kuja kuwa,
Hili msipolijua, mtakuja kushangaa,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Hadithi zasimuliwa, wanafiki kuwajua,
Ahadi zao nazaa, kweli haitatokea,
Naye akiaminiwa, usadiki hatojua,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Na mijini wamejaa, sasa wayaogelea,
Kawaida kufulia, pasi wakaingojea,
Bila ya maji kutia, na moto umekolea,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Kijijini natulia, moyo wangu kuufua,
Kwaniridhi, naridhia, nakuona maridhia,
Hakika hii ni njia, pepo katika dunia,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!


KUNG'ARA KWENYE TIVII

 BIASHARA wamezua, sura kuziangazia,
Tivii wazinunua, ya kwao kutangaziwa,
Hata ushuzi ukiwa, mradi una rupia,
Kung'ara kwenye tivii, siri ya mafanikio?

Bishara zinatukia, hadhi sasa zinapewa,
Ukubwa kutangaziwa, pasina ya kusinzia,
Kama hukutangaziwa, kujitangaza amua,
Kung'ara kwenye jarida, siri ya mafanikio?

Kwenye habari kivia, na lako huwa lavia,
Wapaswa twaa hatua, usikose angaziwa,
Hata kama kulipia, utaja kurejeshewa,
Kung'ara kwenye tovuti, siri ya mafanikio?

Cheo ukikichukua, gharama ndogo ikawa,
Kwingi utakukwambua, hata mawe nayo pia,
Hubinywa damu kutoa, kwa dawa ukatumia,
Kung'ara kwenye tivii, siri ya mafanikio?

Shani imetufikia, ya mazuri kutononoa,
Na sauti kusikiwa, hata na wenye mafua,
Vigugumizi wakawa, kwenye vyombo ni fasaha,
Kung'ara kwenye jarida, siri ya mafanikio?

Uchumi wa zawadiwa, bila ya kutumikia,
Enzie zimefikia, wajuao watambua,
Jasho wanaolitoa, papo hapo hubakia,
Kung'ara kwenye tovuti, siri ya mafanikio?

Kizungumkuti kikawa, dhihaka kupaliliwa,
Nami hilo nimeng'amua, ang'arae atumiwa,
Mishipi washilkilia, mwanasesere akawa,
Kung'ara kwenye tivii, siri ya mafanikio?

Itihari hatakuwa, kaziye kutumikia,
Hufanza la kuambiwa, hutumwa kutumikia,
Nchi atawauzia, bila ya kuulizia,
Kung'ara kwenye jarida, siri ya mafanikio?

Ni nani asiyejua, hadhihi ya kuambiwa,
Huyo wa kukimbilia, kitu gani afatia,
Nini aenda fichua, au ulinzi kutoa ?
Kung'ara kwenye tovuti, siri ya mafanikio?

U R I T H I


BABA anamhofia, ataiaga dunia,
Naye anajiandaa, urithi kuuchukua,
Fursa azichambua, pahali pema kukaa,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Kisa nimehadithiwa, mizungu kilichotiwa,
Ngano ya kuenguliwa, toka tambo za dunia,
Inayotia fadhaa, na  hamasa kupungua,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Kumbe nilivyoyajua, sivyo yalivyotokea,
Kielelezo si dawa, zaidi walichengua,
Ndani wakayafikia, mimi nisiyoyajua,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Fadhaa yawaumbua, neno hili kusikia,
Uraibu umekuwa, pombe waisiyoelewa,
Mlevi sasa kichaa, kila mtu abambua,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Kumbe laini kikiwa, ugumu ndani hulea,
KIla kinachong'aa, hakiachi kufubaa,
Navyo vinavyovutia, mvuto huja kwiishiwa,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Rai niliitengua, haikuwa ya raia,
Mwenzi aliyezidiwa, wala hakuwa mzawa,
Mwana aliyejitia, hakuwa Mtanzania?
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Watumwa waliokuwa, danguroni wamekaa,
Nta sasa wazaa, na mnato kuutia,
Mzinga kupalilia, kuvuna ya ushujaa?
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Hatua wasiotwaa, aibu wanatutia,
Umma wahofu ubia, walikwishauandaa,
Wafanzao wayahua, na kwetu sisi hadaa,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?


Lenu langu litakuwa


Wanyonge wanapokuwa, na mimi nitaingia,
Lao nikalichukua, mpka langu likawa,
Ndicho nilichoumbiwa, musrati kufwatia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Sikuumbiwa dunia, njii hii napitia,
Lengo nimejiwekea, uangavu kufikia,
Kuona msiyojua, wala kuyafikiria,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Hili si la kuombewa, ni tunu ikijaliwa,
Mimi nalifurahia, kuishi naaazimia,
Msongo kwangu likawa, shinikizo kunitia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Maisha nakadiria, taishi kutumikia,
Vingine naviachia, hili kwake nahamaia,
Nikaanzisha ubia, milele kuendela,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Inshallah naitia, siachi kukumbukia,
Neema najiombea, na kinga nikapatiwa,
Akitacho Jalia, na hakika ndilo huwa,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Hili ninalielewa, vingine sijafikiria,
Nafuai nimeitoa, ruksa sijajaliwa,
Yeye ndiye huamua, mimi wa kufatilia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Nia akibarikia, lake ndilo hutimia,
Mimi atanitumia, abdi niliyekuwa,
Lake nikaitikia, na kazi kumfanzia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Muhula akinigea, vyema kutumikia,
Hadi nitapofikia, wengine wakachukua,
Yake akaniridhia, na mimi kumridhia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Akhiri amesikia, yangu atayaridhia,
Nakili lililokuwa, uwakili sijapewa,
Ila kushuhudia, kwa lile ninalojua,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Makombora yanarudi

 YATUPWA kuhilikia, safu wakazipangua,
Asubhi kiingia, mipango wanajipangia,
Jioni ikiishia, tathmini hutolewa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hadithi kuendelea, hurushwa yakarejea,
Mwamvuli wahofia, mlengwa anatumia,
Uyahudi wangejua, huyo wangemnunua,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Wabaki kusingizia, adui kawarushia,
Kumbe ilivyokuwa, yenyewe yajirudia,
Siri hawajaijua, wanazidi kuumia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Aliko hawajajua, nasibu waitumia,
Kapelekewa hidaya, wala hazikupokelewa,
Wadhani ana  kinaya, hayajali ya dunia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Ganzi limeshaingia, ovoovyo yarushiwa,
Lengo sijalitambua, wala pia yake nia,
Hadhira inashangaa, kitali kinavyokuwa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Na mimi najiachia, mlinzi atanifaa,
Kadari sijaijua, pengine hii ndo njia,
Wito nilishaitikia, hutoweza kunitoa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hili sikuigilizia, starehe naijua,
Tena ninafurahia, kulikosa si ridhaa,
Wanyonge ni yangu bia, hunywa hadi nikalewa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hayanipiti masaa, bila kuwaulizia,
Hali zao kuzijua, na nini wapungukiwa,
Sinacho nitakitoa, kukopa nilichopwa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Mkononi huachia, mtupu nikabakia,
Hali nikiangalia, h aziwezi fanania,
Ila raha naijua, wala siwezi kulia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Nderemo inapokuwa, peponi hujisikia,
Na kilio wakilia, ninauvaa ukiwa,
Yao niemshakusudia, ya kwangu budi yakawa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Laiti mngelijua, kusita isingekuwa,
katika hii dunia, uongozi ni kufaa,
Uongozi wa kubwia, na starehe karaha,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hesabu nishahisabia, wa sikio, kusikia,
Ulimi sikuachia, ila kwa kujizuia,
Lengo nalitarajia, Mwenyezi atajalia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !