Friday, June 28, 2013

kujibu si kujibu tu


Mtu mzima akiwa,  utoto huukimbia,

Hafanzi la kuambiwa, pasina kufikiria,

Kisha akafuatilia, kila analoambiwa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji akili!

 

Tafakari huzua, jambo akafikiria,

Na akisha jipimia, mizaniye humwambia,

Lipi la kuliachia, na lipi kung'ang'ania,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji busara!

 

Malau kwenye dunia, kila kona yaelea,

Ukiamua kuvua, itapinduka mashua,

Na wote mlokuwa, ndaniye kuumbuliwa,

Kuibu si kujibu tu, inahitaji hekima!

 

Hekima tunaiua, sasa kujirpokea,

Hutomjua kichaa, nani mzima akawa,

Wote sasa mnakuwa, dharau mwapalilia,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Chema walichokijua, inakuwa ni sanaa,

Watu wakajichekea, na mizaha kuidhua,

Hadhari ikififia, hatari huzidi kua,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji akili!

 

Kila mjifanya kujua, hili angeling'amua,

Daraja kujipatia, na heshima kuipewa,

Ubabe anayetitia, kiyama atutakia,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji busara!

 

Wa leo Watanzania, haki zao wazijua,

Maguvu mkitumia, hivi kimya watakaa ?

Sasa demokrasia, vingine haitakuwa,

Kuibu si kujibu tu, inahitaji hekima!

 

Nchi inahujumiwa, watu watayaridhia,

Kauli wasipotumia, ipi iwe yao silaha ?

Mwapaswa kufikiria, kwa hali zao kujua,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Kuandamana ni njia, yaitumia dunia,

Watu wanapozuiwa,  bwawa lao litajaa,

La hasira lilokuwa, hadi kingoze kung'oa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Valvu kifunguliwa, maji huweza pungua,

Tambarae kuingia, salama bwawa likawa,

Vingine haitakuwa, mnatafuta balaa,
Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!
 

Jalali namlilia, kizazi kukiokoa,

Nyota zazusha udhia, giza laanza ingia,

Tuepushe na nazaa, usanii na balaa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

piga ikijibu piga



Laiti tungelijua, sikuzote hufatia,

Ndicho kinachoendelea, hapa kwetu Tanzania,

Haambiliki kakua, nani atamsikia ?

Piga ikijibu piga, hivi nini hufwatia ?

 

Mtu mzima akiwa,  utoto huukimbia,

Hafanzi la kuambiwa, pasina kufikiria,

Kisha akafuatilia, kila analoambiwa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji akili!

 

Tafakari huzua, jambo akafikiria,

Na akisha jipimia, mizaniye humwambia,

Lipi la kuliachia, na lipi kung'ang'ania,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji busara!

 

Malau kwenye dunia, kila kona yaelea,

Ukiamua kuvua, itapinduka mashua,

Na wote mlokuwa, ndaniye kuumbuliwa,

Kuibu si kujibu tu, inahitaji hekima!

 

Hekima tunaiua, sasa kujirpokea,

Hutomjua kichaa, nani mzima akawa,

Wote sasa mnakuwa, dharau mwapalilia,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Chema walichokijua, inakuwa ni sanaa,

Watu wakajichekea, na mizaha kuidhua,

Hadhari ikififia, hatari huzidi kua,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji akili!

 

Kila mjifanya kujua, hili angeling'amua,

Daraja kujipatia, na heshima kuipewa,

Ubabe anayetitia, kiyama atutakia,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji busara!

 

Wa leo Watanzania, haki zao wazijua,

Maguvu mkitumia, hivi kimya watakaa ?

Sasa demokrasia, vingine haitakuwa,

Kuibu si kujibu tu, inahitaji hekima!

 

Nchi inahujumiwa, watu watayaridhia,

Kauli wasipotumia, ipi iwe yao silaha ?

Mwapaswa kufikiria, kwa hali zao kujua,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Kuandamana ni njia, yaitumia dunia,

Watu wanapozuiwa,  bwawa lao litajaa,

La hasira lilokuwa, hadi kingoze kung'oa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

Valvu kifunguliwa, maji huweza pungua,

Tambarae kuingia, salama bwawa likawa,

Vingine haitakuwa, mnatafuta balaa,

 

Jalali namlilia, kizazi kukiokoa,

Nyota zazusha udhia, giza laanza ingia,

Tuepushe na nazaa, usanii na balaa,

Kujibu si kujibu tu, inahitaji nadhari!

 

 

Sunday, June 2, 2013

Sauti inapozimwa

 Ubabe ukitumika, na haki ikawa nyuma,
Hata wasipolalamika, lao kwa sana huvuma,
Hadi mbali kusikika, na kuongeza tuhuma,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Wingi usiobebeka, hauwezi kunguruma,
Sautiye hukatika, zisifike kwenye ngoma,
Masikio kuzibika, pasiwe kitu kuchuma,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Asiyetaka baraka, hatoipat hekima,
Ya kwake yatafanyika, yakaongeza hasama,
Na mbali hawataruka, balaa kuwaandama,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Ya mola yakikwazika, ya nani kuwa salama ?
Amzuiaye Rabuka, ataka yeye nguruma ?
Au anadanganyika, aipoteze neema ?
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Waoga waweweseka, wanaikosa kalima,
Wameshindwa kutamka, wakaondoa dhuluma,
Wanatutia wahaka, kama kweli twenda pema,
Sauti inapozimwa, kilio chake ngurumo!
 
Wingi uliobebeka, kesho isiwe lawama,
Mwenyewe umeyataka, twafumua unafuma,
Kwa shari anayeezeka, akilala huwa wima,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Ninalojua hakika, haki huwa inasema,
KImya kikaondoka, na hoja zake kuvuma,
Kiumbe yote ponzeka, ila si kukosa rehema,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!
 
Waasi usiye wahaka, ninaziomba huruma,
Dunia imewateka, hawajui wanazama,
Muqtadiri eleka, utakalo likapema,
Sauti inapozimwa, kilio chake huzidi!

Thursday, May 30, 2013

Kila muabudu mtu


Wakizuka nakwambia, waabuduji wakawa,

Watu wawatangulia, na ibada kuwafanyia,

Tambua bado wazua, trela wameanzia,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

 

 

Kichuguu wachukua, wao mlima walilia,

Mlango wa kupitia, lazima pa kuanzia,

Budi mtu  kuchezewa, kttu asiyetambua,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

 

Wao wakajiandaa, uungu kuununua,

Wafanye ya kushtua, wakatingisha dunia,

Na uliyewaachia, ukaja kuyajutia,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

 

Milango yafunguliwa, muda haujaishia,

Toba kuikimbilia, maghufira kiuyajua,

Ibilisi kumkataa, na mbali ukamlania,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

 

Mtu wa kuabudiwa, apaswa awe raia,

Kwa shidaye kuijua, na  tatizo kutatua,

Hakika ninawaambia, Mola hapo mtamjua,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

 

Vingine mwamchezea, hasiraye ikakua,

Kidogo kilichokuwa, mlima kugeuziwa,

Viumeb mwachanganyikiwa, si miaka mna saa,

Kila muabudu mtu, hutaka naye uungu!

Kila mkweza ukubwa



Ukimuona raia, debe anajipigia,

Mkubwa kumnyanyua, hadi awe nazo mbawa,

Huyo ukimchungua, siriye utaijua,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Yazusha yetu dunia, mitume wa kuamua,

Cheo wakajitwalia, na karama kununua,

Kisha wakaja chipua, mithili yake maua,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Huyo ukimuangalia, ukubwa aulilia,

Na njiaye ya kupitia,  mkubwa kwanza kupewa,

Kisha aje kufatia, apewe alichopewa,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Hawa watu wa tamaa, waidanganya dunia,

Ndivyo wanavyofikiria, kumbe la hasha waugua,

Yumkini ukichaa, tena wa kuchanganyikiwa,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Waishi kwa kupagawa, na ushindani kuzua,

Wa ovyo ulokuwa, kufuru unaotia,

Hakika nawaambia, washindwe na kulegea,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Fakiri wetu walia, makubwa twende vamia,

Gari ukijitolea, mafutaye pia lipia,

Tana karne ikiwa, vyema zaidi itakuwa,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Na ndege nayo pia, kwa papo hapo ingia,

Kwingine kutotokea, hili ukalitambua,

Zusha ya kuhurumia, usizushe ya kuonea,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Wahurumie izaya, Muumba wetu radhia,

Dhambi wanaopalilia, kwa pepo kuwaingia,

Kama kipepeo kuwa, kula bila cha kuzaa,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

Umenipata ukiwa, wangu nawafikiria,

Dhehebu nalikimbia, masoni weshaingia,

Salama nawaambia, ya kwao kuwaachia,

Kila mkweza ukubwa, na yeye autamani!

 

 

Maji yakizidi unga


Mafundi wakizidisha, leseni wakazitoa,

Cheti wenzi kupandisha, na unafiki kuvaa,

Huja panako mkesha, chungu chote kufuaa,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

 

Vyeo wanavyovikosha, kwa hisani kuzitia,

Kiasi wakazidisha, hadi wakakanyagia,

Huyatatiza maisha, na kuongeza nazaa,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Ya ovyo watayazusha, hadi vyumba vikajaa,

Kila ukikitingisha, kibiriti kinapwaya,

Huja sasa yakuwasha, kujikuna kukakua,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Mwanziishi wa rabsha, si anayekataliwa,

Ila anayetoa rushwa, ziada akajaziwa,

Siasa zikaharisha, na kwacha harufu mbaya,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Mengine ya kuchekesha, kiumbe anayozua,

Ajitikwa ya kutisha, kama kubeba dunia,

Kumbe muosha hukoshwa, bado hajayaelewa,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Angazieni maisha, haya yangu kuyajua,

Kuna mikasa yachosha, na vitendo vya udhia,

Watu vinawewesesha, haki yao kutojua,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Mirija waiboresha, wachache kuyakamia,

Maji wakayapitisha, ya malaki sio mia,

Hali haijawawezesha, mpito utapasua,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Mita waziviringisha, maudhui kurejewa,

Hii yaanza yavusha, na nyingine zafatia,

Hilo hilo likijsaa, watu watajiepusha,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Makundi yatutingisha, yao yakikataliwa,

Nani wa kuwawezesha, ikiwa watindikiwa,

Kauli zingine zachosha, humpa mtu kuugua,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Hukuambia maisha, na lingine halijawa,

Nakataa ni kuzusha, mtakuja changanyikiwa,

Vitendo vya kubabaisha, sumu yake kuchukiwa,

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

Tamaa lakukatisha, patupu kuambulia,

Hata kama umekesha, usambe  na ya jana njaa,

Na wala hukuendesha, ila umetumikia ?

Maji yakizidi unga, ugali hugeuka uji!

 

 

 

Monday, May 27, 2013

MTAKUJA ENDA NA MAJI


Ujinga ukisikia, ni wengine kuachia,

Wao wakajifanyia, wanayoyakusudia,

Wenyewe yakawafaa, patupu ukaambulia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

mtakuja kwenda na maji !

 

Fakiri ukiambiwa, tambua walanguliwa,

Wengne kujichumia, na weye ukajikwaa,

Wao wakaendelea, nyuma wenye kubakia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Chini wa kukanyagiwa, hadhi mngeliijua,

Ndio juu mlokuwa, iwapo mnajijua,

Ila msipojitambua, mtazidi kuonewa,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

Kuongoza ni hidaya, watu wakatumikiwa,

Haijawa, haitakuwa, ubaba kuuchukua,

Kisha kujiamlia, jinsi mnavyojisikia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Hili mkilitambua, maswali mtayazua,

Katibani kuingia, cheo mkajilindia,

Ila mkipuuzia, mwauzwa kwenye gunia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

KIswahili mkitumia, kila kitu mtajua,

Hata na hizo sheria, hakuna wa kupindua,

Machale  huwaambia, stopu mkendaitoa,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Mijini mkiyajua, wenyewe mtaamua,

Huko mikoani pia, na kwenye hizo wilaya,

Uongozi mtatia, muwezao kuuchaagua,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

Njia ya demokrasia, ni ya wengi kuamua,

Wachache wakiamua, huwa wavunja sheria,

Ni budi kuwaodnoa, wenye haki kuwatia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !

 

Muda itatuchukua, ila huko twafikia,

Hata wanaozuia, patupu wataambulia,

Mkiamka Tanzania, Afrika itakuwa,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Mnakuja enda na maji !

 

Na  lugha hii rupia, yafaa kiuitumia,

Kanuni tukazitia, na mifumo kuizua,

Juu juu kutembea, ikatuona dunia,

Nchi hii nchi yenu, wengine mkiachia:

Itakuja enda na maji !