Thursday, September 5, 2013

hivi kosa ni la nani?



Wakitamka bahali, hudhani Java natua,

Hushindwa tamka ghali, gari ukalisikia,

Hukambia kalili, kumbe kariri wambiwa,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Hukutajia fahali, ng'ombe ukamdhania,

Kumbe umulimuli, na kung'ara kwa tabia,

Kiswahili dhofu hali,  wahariri waugua?

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Wakitamka ya hali, ulivyo huidhania,

Kumbe joto dalili, ndo wanalofikiria,

Wasemapo ya mahari, ndipo huchanganyikiwa,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Mahali ndiyo mahari, hivi lini imekuwa,

Na kwanini mhariri, haya anayaridhia ?

Au hanayo habari, kwa yanayoripotiwa?

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Lini ikawa ni shali, hali ya kuwa ni shari,

Piri haijawa pili, hilo naona dosari,

Bado kwetu ni ajali, na ajari si sanjari,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Kabuli huwa ukweli, haijawa ni kaburi,

Na ishara ni dalili, si hariri si dariri.

Na johari si johali, hilo kwa kweli athari,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Kalili sio kariri, ni kidogo kitakuwa,

Wala reri sio reli, na wala haitakuwa,

Stairi si staili, mushkeli inakuwa,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Ajira kama ajali, nasamehe wahariri,

Dampo la mwenye mali, huna ila ya hiari,

Ila wateja muhali, inataka ujibari,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

 

huwa kimya kimya


Mlipe vyema mlipa, siri atawafichia,

Chochote weza amua, haki yenu kujakuwa,

Na ataye wasumbua, haki yenu  huambiwa,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Kuna kazi  za kupewa, na kanuni kujengewa,

Kama  unashateuliwa, sheria za kutetea,

Mifuko utajaziwa, na ziada kuchukua,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Oisi hufunguliwa, na funguo kufungua,

Kila kitu wazi kuwa, waweza kujichukulia,

Nani wa kuangalia, cha mtu kisichokuwa?

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Sinema nazo sanaa, kuchota wabarikiwa,

Akili wakatwambia, wenzetu wanatumia,

Sisi tusiojaliwa, twabakia kufulia,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Watunzi wazuzuliwa, waimbaji nao pia,

Bulungutu kugawiwa, kwa kazi zisizokaa,

Haziachi kufubaa, pesa weshazichukua,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Wakala watuanzishia, wakawajaza jamaa,

Kufumba na kfuumbua, matajiri wanakuwa,

Kila ukiangalia, huoni tulilojaliwa,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Ukuu wanagawiwa, na vilembe kufungiwa,

Majoho nayo kupewa, na senti zanye mkia,

Kila ukifuatilia, huoni unachoambua,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Tume wanazizindua, mamilioni wakapewa,

Sasa nao watumbua, wafurahi Tanzania,

Kukumbukwa radhia, nini tena watalia?

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Ila ukiangalia, uwiano unavia,

Vijijini kwenye njaa, neema kutoijua,

Laana wamekamia, ubani kujichomea,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Kiasi isipokuwa, amani huifagia,

Kiasi kikipotea, umoja hujibangua,

Kiasi isipokuwa, husuda huja kuua,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

njaa aina mbili



Walio na njaa huwa, chakula wakimbilia,

Kukila tumbo kujaa, na maji wakajazia,

Wala sio kuchezea, mchanga wakakitia,

Wapo wenye nja'ya kula, na njaa ya kuharibu!

 

Wenye ya ajabu njaa, israfu wanatia,

Chakula hukichezea, kwani si ya kweli njaa,

Sana walikililia, ili sheri kufanzia,

Wapo wenye nja'ya kula, na njaa ya kuharibu!

 

 

Matumbo yamewajaa, wazito utadhania,

Bado wakakililia, hali kuishatkia,

Pindi wanapopatiwa, huanza kukichezea,

Wapo wenye nja'ya kula, na njaa ya kuharibu!

 

 

U D I K T E T A



Ndani ukijichimbia, ukaanza kuamua,

Kupe waliotulia, huzidi kujichimbia,

Hawana la kulijua, zaidi ya kuambiwa,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Amri huwa silaha, toka  juu wakipewa,

Kugeuka si ridhaa, lazima kuitikia,

Hata likiwa ni baya, kwao zuri huambiwa,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Aidha roboti huwa, chama kimeshafyatua,

Si wa kufikiria, kujua wasilojua,

Gea ilishaingia, yote ndiyo kwitikia,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Hoja zote hufulia, na umma kunyanyapaa,

Wao wakajidhania, wajua wasiyojua,

Hadi machweo yakawa, shuka wanakimbilia,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Hutweta na kutetua, na vingama kupitia,

Ibura zikakimbia, na miujiza kupaa,

Majani mtu hutwaa, kama nguo akavaa,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Yaja tusiyoyajua, tena ya kutuumbua,

Wenzangu nawashtua, mmeacha kujitambua,

Na hakuna mkubwa udhia, kama mtu kutojijua,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Watu wanawahofia, huko mnakoelekea,

Njia mmeshapotea, kugeuka mwakataa ?

Na pori wanalijua, salama halijakuwa ?

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

FIKRA


 

Hucheka nikisikia,  yasiyokuwa najua,

Vivumishi kuvizua, utadhani wanapaa,

Ila ninavyoyajua, kutua yamekwishatua,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Hadithi imebakia, na nyingi zao tamaa,

Mioyo yanunuliwa, na akili nazo pia,

Hawana la kuamua, ila la  kutarajiwa,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Nani amekuambia, finyu, pana litazaa,

Na chanya haitazaliwa,  na hasi kinachokuwa,

Nyimbo wanajiimbia, kweli sintoitarajia,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Wanapenda kusikiwa, japo hewa wanatoa,

Aalli kisichokuwa, zaidi kukwepa njaa,

Wengine wanaugua, kukariri wasojua,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Wamezivaa kofia, matundu zilizojaa,

Zawavujia mvua, na hoja zisizokuwa,

Watu wanawashangaa, wao wanajisifia?

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Hoja wainshauflia, na wengine waogea,

Kazi ni kurejearea, utadani mbovu pleya,

Wapenda kujisikia, hata kwa kisichonukia,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Juu waweza paua, na msingi hujatia,

Watu mnawakimbia, ushirikishi mwavua,

Kisha mnajisema, yakuwa na yasokuwa?

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Chini mngejichimbia, na mizizi kuitia,

Ndipo mngeyafikia, ya matokeo kujua,

Kasi ipi ingekuwa, hilo noma twaawambia,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

 

 

takataka


Angalia takataka, zazidi kuimarika,
Tunu hii ya hakika, kwake yeye Mwafrika,
Hajafa haujaumbika kabla hajawa taka,
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Ndivyo alivyoumbika, kihuru au mateka ?
Au analogeka, na juu waliioshika,
Akili zikakunjika, jipya kutokufanzika?
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Makwao wanapotoka, na kwa vimada kufika,
Kila kona kwapambika, kwa wingi wa takataka,
Haya yanakubalika, wala hawana mashaka,
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Kwa wageni kwarembeka, kwa Mwafrika ni mahoka,
Nchi ukiizunguka, hili sasa lajengeka,
Hata kulikosifika, sasa kunaharibika,
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Kila kttu wakishika, sasa chageuka taka,
Ila wao wapambika, na majoho kubebeka,
Huu nchi yanyongeka, vipi tutayaepuka?
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Akili za takataka, usafi hazitotaka,
Maana kunawirika, ni lazima kuchafuka,
Ndiyo wanayoyataka, hawawezi kugeuka,
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Ahadi ilishawekwa, muda unasubirika,
Siku yao kuja fika, wavune waliyotaka,
Na si mkosa Rabuka, mamboye ni ya hakika,
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !

Wednesday, September 4, 2013

huwa kimya kimya...

 
Mlipe vyema mlipa, siri atawafichia,
Chochote weza amua, haki yenu kujakuwa,
Na ataye wasumbua, haki yenu  huambiwa,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
 
Kuna kazi  za kupewa, na kanuni kujengewa,
Kama  unashateuliwa, sheria za kutetea,
Mifuko utajaziwa, na ziada kuchukua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
 
Oisi hufunguliwa, na funguo kufungua,
Kila kitu wazi kuwa, waweza kujichukulia,
Nani wa kuangalia, cha mtu kisichokuwa?
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
 
Sinema nazo sanaa, kuchota wabarikiwa,
Akili wakatwambia, wenzetu wanatumia,
Sisi tusiojaliwa, twabakia kufulia,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
 
Watunzi wazuzuliwa, waimbaji nao pia,
Bulungutu kugawiwa, kwa kazi zisizokaa,
Haziachi kufubaa, pesa weshazichukua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
 
Wakala watuanzishia, wakawajaza jamaa,
Kufumba na kfuumbua, matajiri wanakuwa,
Kila ukiangalia, huoni tulilojaliwa,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
 
Ukuu wanagawiwa, na vilembe kufungiwa,
Majoho nayo kupewa, na senti zanye mkia,
Kila ukifuatilia, huoni unachoambua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
 
Tume wanazizindua, mamilioni wakapewa,
Sasa nao watumbua, wafurahi Tanzania,
Kukumbukwa radhia, nini tena watalia?
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
 
Ila ukiangalia, uwiano unavia,
Vijijini kwenye njaa, neema kutoijua,
Laana wamekamia, ubani kujichomea,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
 
Kiasi isipokuwa, amani huifagia,
Kiasi kikipotea, umoja hujibangua,
Kiasi isipokuwa, husuda huja kuua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!