Thursday, September 5, 2013

U D I K T E T A



Ndani ukijichimbia, ukaanza kuamua,

Kupe waliotulia, huzidi kujichimbia,

Hawana la kulijua, zaidi ya kuambiwa,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Amri huwa silaha, toka  juu wakipewa,

Kugeuka si ridhaa, lazima kuitikia,

Hata likiwa ni baya, kwao zuri huambiwa,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Aidha roboti huwa, chama kimeshafyatua,

Si wa kufikiria, kujua wasilojua,

Gea ilishaingia, yote ndiyo kwitikia,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Hoja zote hufulia, na umma kunyanyapaa,

Wao wakajidhania, wajua wasiyojua,

Hadi machweo yakawa, shuka wanakimbilia,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Hutweta na kutetua, na vingama kupitia,

Ibura zikakimbia, na miujiza kupaa,

Majani mtu hutwaa, kama nguo akavaa,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Yaja tusiyoyajua, tena ya kutuumbua,

Wenzangu nawashtua, mmeacha kujitambua,

Na hakuna mkubwa udhia, kama mtu kutojijua,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Watu wanawahofia, huko mnakoelekea,

Njia mmeshapotea, kugeuka mwakataa ?

Na pori wanalijua, salama halijakuwa ?

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

No comments: