Monday, February 20, 2012

WIZI KAMA NGAZI CHINI LAZIMA KUSHUKA

ASILI ilivyokuwa, na huwezi kuzuia,
Juu wezi wakikaa, chini nao hufatia,
Uoza ukaenea, kila mahali ukawa,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Nchi zataka ulua, watu wasio tamaa,
Wajuao kutulia, na mambo kufatia,
Sio wanaosinzia, na wengine kuachia,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Hao wanaoachiwa, hugeukia ubaya,
Mengi wakajifanyia, nchi isiyoyafaa,
Na dhuluma kuitia, kila katika hatua,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Ndipo tulipofikia, na dunia inajua,
Yaona twaikosea, utawala tunapwaya,
Mambo tunayaachia, yenyewe yajiendea,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Na wengine washania, ushirika tumekua,
Na wahuni watuvaa, na mfukoni kututia,
Na kila tukiamua, ni wao yanayowafaa,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Kila mwana ajisemea, hilo analolijua,
Ukweli hatujajua, maana hatujaambiwa,
Uongo tumezoea, ukweli tunauchelea ?
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Kila wizara yalia, na idara nazo pia,
Salama imepotea, kwa watu na mali pia,
Ulinzi ajizi yawa, kubaya twaelekea,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Nchi sasa yaibiwa, kushoto pia kulia,
Na ndani wametulia, haya wanaojifanyia,
Ulemavu twajitia, na upofu nao pia,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Amkeni mwasinzia, kuwa macho mwatakiwa,
Arijojo Tanzania, ndege sasa inapaa,
Mlima kuuvamia, ni rahisi itakuwa,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Hatari inatujia, kuamka tunatakiwa,
Rubani kwenda mshtua, apime wanaomsaidia,
Yaelekea jamaa, hawajui yalokuwa,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Ushahidi nimetoa, nami kuja shuhudiwa,
Niliona, nikajua, na wengine kuwaambia,
Hakuna alonisikia, hadi shari kutokea,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Na kizazi kitajua, mkweli aliyekuwa,
Iandike historia,waliofanza sanaa,
Wakajitia kujua, hata wale wasojua,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Yafaa kumgeukia, Mola kutuhurumia,
Majaribu katutia, tunashindwa kujitoa,
Kila mtu aumia, na sifa zinapungua,
Wa juu wakiwa wezi, wa chini wa'che kuiba?

Jeneza nalingojea

Mwenyewe nimesikia, kwangu hautorejea,
Na mtu sikuambiwa, maneno umeyatoa,
Na kiapo kuapia, hadi maiti ukiwa,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Maiti naikataa, haiwezi yangu kuwa,
Ila unayemfaa, sasa ulikotulia,
Yabadilika dunia, wakati umechelewa,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Hasira nazo ukiwa, waupata ukichaa,
Mwenzi nakusikitia, mumunye umeshakua,
Ukubwani yakupwaya, na kichekesho kwendakua,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Jeuri umezidia, na dharau kujitia,
Na hicho ulichokuwa, wengine wamejaliwa,
Tena wamezidishiwa, na kila mtu anajua,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Nani wa kukuhurumia, kiumbe usiyesikia,
Ubishi umekujaa, na vya watu kudokoa,
Urushi umeingia, na watu kusingizia,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Mikopo unachukua, biashara hujajua,
Hela zinakoendea, hakuna anayejua,
Mwanamke wapotea, au umeshachezewa,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Marafiki wachagua, mazuri wasokutakia,
Wajianya unajua, na sisi twakuachia,
Salama twajitakia, sio kuja kunadiwa,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Mwanamme kakuzuzua, hili hatujalijua,
Tabia twakushangaa, fedha zinavyopotea,
Mashimbo unatoboa, hata mitaji ikiwa,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Hakika weye balaa, sasa tumeshakujua,
Mbali na wewe kukaa, yabidi hivyo ikawa,
Vinginevyo kutulia, wazee wakikuombea,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Na laana kuitoa, uliyokwishajiwekea,
Jeneza kuaguliwa, mwingine kutochukua,
Ulimi hakika baa, waweza kuteketeya,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Waganga wakutambua, ATM umeshakua,
Wazidi kukufukua, tena na kukuchimbua,
Kiumbe unalaaniwa, kwa hayo unayozua,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Huruma nawaonea, wenye wake kama hawa,
Akili hukupasua, mengi ukamdhania,
Kumbe ameshalaniwa, huko anakotokea,
Jeneza nalingojea, ambalo wanitumia.

Friday, February 17, 2012

Mnafiki hubomoa

Mnafiki hutumiwa, na wa ndani na nje pia,
Ya kwao yakachanua, kwa malengo kuwafaa,
Na yeye ni kitambaa, makamasi huachiwa,
Mnafiki hubomoa, sikuzote si mjenzi,
Na hasa anapokuwa, ni wa watu kiongozi,
Ni kiraka cha mikogo,
Hutumiwa na vigogo,
Ni karatasi ya choo,
Hutumiwa na vizito!

Udogoni huanzia, sio tu anapokuwa,
Utashi humuishia, wengine kuwangojea,
Hutumwa akakimbia, hata asikokujua,
Mnafiki hubomoa, sikuzote si mjenzi,
Na hasa anapokuwa, ni wa watu kiongozi,
Ni kiraka cha mikogo,
Hutumiwa na vigogo,
Ni karatasi ya choo,
Hutumiwa na vizito!

Uzuzi kwake huvia, hana analochambua,
Sembuse kuja ng'amua, au baya kuligundua,
Huishi kwa majaliwa, kaburini kumtia,
Mnafiki hubomoa, sikuzote si mjenzi,
Na hasa anapokuwa, ni wa watu kiongozi,
Ni kiraka cha mikogo,
Hutumiwa na vigogo,
Ni karatasi ya choo,
Hutumiwa na vizito!

Sio wa kutegmewa, sembuse kujaaminiwa,
Yake ukimsikia, jua wenda kupotea,
Analolifikiria, ni wewe kununuliwa,
Mnafiki hubomoa, sikuzote si mjenzi,
Na hasa anapokuwa, ni wa watu kiongozi,
Ni kiraka cha mikogo,
Hutumiwa na vigogo,
Ni karatasi ya choo,
Hutumiwa na vizito!

Utumwani atawatia, hata macho walokua,
Wakijakushtukia, minyororo wamevaa,
Wakawa waning'inia, wasijue pakwachia,
Mnafiki hubomoa, sikuzote si mjenzi,
Na hasa anapokuwa, ni wa watu kiongozi,
Ni kiraka cha mikogo,
Hutumiwa na vigogo,
Ni karatasi ya choo,
Hutumiwa na vizito!

Hata wakubwa wakiwa, ni watu wa kutumiwa,
Ninawasikitikia, watu wasiojitambua,
Na kizazi kilokuwa, huruma kuwaonea,
Mnafiki hubomoa, sikuzote si mjenzi,
Na hasa anapokuwa, ni wa watu kiongozi,
Ni kiraka cha mikogo,
Hutumiwa na vigogo,
Ni karatasi ya choo,
Hutumiwa na vizito!

Yarabi nakulilia, utumwa kutonitia,
Kwa juu waliokuwa, hali ninajitambua,
Ni heri kunichukua, kuliko hivyo ikawa,
Mnafiki hubomoa, sikuzote si mjenzi,
Na hasa anapokuwa, ni wa watu kiongozi,
Ni kiraka cha mikogo,
Hutumiwa na vigogo,
Ni karatasi ya choo,
Hutumiwa na vizito!

Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

BATI waweza kutia, uwanja ukaanua,
Mipaka ukaitia, kujenga wadhamiria,
Ila hili majaliwa, hata ukitia nia,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Ujenzi ni majaliwa, na mtu kuandikiwa,
Msingi wanaoitia, hadi wakamalizia,
Ni wachache walokuwa, wengi wao hupwelea,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Hushidnwa kuendelea, katikati kuishia,
Bado ipo yao nia, ila uwezo wapwaya,
Mahitaji yazidia, kuliko kinachoingia,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Na hili jema kujua, mtu unapojaliwa,
Muumba ukamjua, na dhamira kumwachia,
Hubariki yalokuwa, hadi yaje kutimia,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Msingi ukanyanyua, imara uliokuwa,
Kisha kuta ukatia, na lenta kuimwagia,
Na boriti kufungia, paa ukalipaua,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Milango ukafungia, madirisha nayo pia,
Fenicha ukazitia, makabati yalokuwa,
Na vyumba kujipmbia, kadri unavyojua,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Neru ukamiminia, na kumwaiya chokaa,
Na rangi kuziwania, zote zinazovutia,
Nje ukamalizia, na bustani kukua,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Ukuta kuzungushia, ulinzi ukiamua,
Na kuondoa udhia, jirani waliokuwa,
Na geti kujiwekea, tena la kujifungua,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Na kengele ukatia, hodi ukazikataa,
Na taa kumulikiwa, hata usiku ukiwa,
Na ving'ora vikajaa, wevi wapate kimbia,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Siku ikajafikia, ya wewe kujahamia,
Ziraili akatua, na roho kuichukua,
Wengine wataingia, wewe hautaingia,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Yako haiwezi kuwa, huwa ya atayenunua,
Au mrithi akiwa, ataka kuitumia,
Wewe kwana kuhamia, ulikoishandaliwa,
Mtu kuweka msingi, si hakika ya kujenga!

Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

BATI waweza kutia, uwanja ukaanua,
Mipaka ukaitia, kujenga wadhamiria,
Ila hili majaliwa, hata ukitia nia,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Ujenzi ni majaliwa, na mtu kuandikiwa,
Msingi wanaoitia, hadi wakamalizia,
Ni wachache walokuwa, wengi wao hupwelea,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Hushidnwa kuendelea, katikati kuishia,
Bado ipo yao nia, ila uwezo wapwaya,
Mahitaji yazidia, kuliko kinachoingia,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Na hili jema kujua, mtu unapojaliwa,
Muumba ukamjua, na dhamira kumwachia,
Hubariki yalokuwa, hadi yaje kutimia,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Msingi ukanyanyua, imara uliokuwa,
Kisha kuta ukatia, na lenta kuimwagia,
Na boriti kufungia, paa ukalipaua,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Milango ukafungia, madirisha nayo pia,
Fenicha ukazitia, makabati yalokuwa,
Na vyumba kujipmbia, kadri unavyojua,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Neru ukamiminia, na kumwaiya chokaa,
Na rangi kuziwania, zote zinazovutia,
Nje ukamalizia, na bustani kukua,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Ukuta kuzungushia, ulinzi ukiamua,
Na kuondoa udhia, jirani waliokuwa,
Na geti kujiwekea, tena la kujifungua,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Na kengele ukatia, hodi ukazikataa,
Na taa kumulikiwa, hata usiku ukiwa,
Na ving'ora vikajaa, wevi wapate kimbia,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Siku ikajafikia, ya wewe kujahamia,
Ziraili akatua, na roho kuichukua,
Wengine wataingia, wewe hautaingia,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Yako haiwezi kuwa, huwa ya atayenunua,
Au mrithi akiwa, ataka kuitumia,
Wewe kwana kuhamia, ulikoishandaliwa,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Haiwezi kuwa hoja, kuzaliwa tumbo moja,

Katika miaka hii, ya nazi kufanywa tui,
Adui kuwa akhii, na mlinzi Mmasai,
Na watu wengi laghai, kweli waliokinai,
Haiwezi kuwa hoja, kuzaliwa tumbo moja!

Hai wasokuwa hai, na mui waso na rai,
Wafanyao baibui, kugeuzwa buibui,
Na sinia makarai, wafaao hawafai,
Haiwezi kuwa hoja, kuzaliwa tumbo moja!

Mdaiwa kuwa mdai, na mwenye njaa hajui,
Wajanja magoigoi, na mbumbumbu wasanii,
Uhai ukawa hoi, taabani tandabui,
Haiwezi kuwa hoja, kuzaliwa tumbo moja!

Janibu kuwa jinai, na ghaibu maslahi,
Huzuni ikafurahi, na furaha kuzirai,
Hayaishi majidai, na mafao hayafai,
Haiwezi kuwa hoja, kuzaliwa tumbo moja!

Sijawa mpiga nai, na midundo sitambui,
Ila hili ninarai, wajuao kujiwahi,
Mazazi mengi nishai, upweke siukinai,
Haiwezi kuwa hoja, kuzaliwa tumbo moja!

Mwapiga ngoma ya kifo

Uroho utatuumbua, na tamaa kutuua,
Wamiliki watakiwa, kujenga kisha kukaa,
Madini wanakochimbua, wao na zao jamaa,
Mwapiga ngoma ya kifo, kucheza acheze nani?
Walemavu tukizaa,
Na kojale umauti?
Haiwezi kuwa hoja

Viongozi nao pia, haya wanaoridhia,
Si wajinga kuwavaa, na kisha mkawahadaa,
Njaa inayowasumbua, kitu wasiokijua,
Mwapiga ngoma ya kifo, kucheza acheze nani?
Walemavu tukizaa,
Na kojale umauti?
Haiwezi kuwa hoja

Nchi haijajiandaa, maafa mwatuletea,
Ya kawaida mwazubaa, makubwa yasiwe baa,
Mbona twawaajabia, ovyo kukeungikiwa,
Mwapiga ngoma ya kifo, kucheza acheze nani?
Walemavu tukizaa,
Na kojale umauti?
Haiwezi kuwa hoja

Njaa mnailea, utajiri mwawania?
Umauti mkitia, wenzetu Watanzania,
Haya mtafurahia, mkala na kutanua?
Mwapiga ngoma ya kifo, kucheza acheze nani?
Walemavu tukizaa,
Na kojale umauti?
Haiwezi kuwa hoja

Macho mnayazuia, ukweli kuangalia,
Nyani mnamuua, kwa kinyume kumjia?
Laana mnaifungua, na kwenu haitaishia,
Mwapiga ngoma ya kifo, kucheza acheze nani?
Walemavu tukizaa,
Na kojale umauti?
Haiwezi kuwa hoja


Subira inatakiwa,siotunavyoingia,
Hujayakatupalia,puazijekuumia,
Pasiwewa kumlilia, nuksi tukizizaa,
Mwapiga ngoma ya kifo, kucheza acheze nani?
Walemavu tukizaa,
Na kojale umauti?
Haiwezi kuwa hoja

Pwani wanaotamia, nakovisiwani pia,
Hawawezi kuumia, haya watayasikia,
Bara waliochimbiwa, mizizi ikafukuliwa,
Mwapiga ngoma ya kifo, kucheza acheze nani?
Walemavu tukizaa,
Na kojale umauti?
Haiwezi kuwa hoja

Ngoma hii kuiondoa, tunaiomba dunia,
Waweze kusaidia, vingine kuganga njaa,
Wakati haujawadia, mabomu kuyachezea,
Mwapiga ngoma ya kifo, kucheza acheze nani?
Walemavu tukizaa,
Na kojale umauti?
Haiwezi kuwa hoja

Sumu haina radhia, wala wa kumuachia,
Pale inapoingia, damu zote zitalia,
Na vizazi kufatia, kama ilivyo India,
Mwapiga ngoma ya kifo, kucheza acheze nani?
Walemavu tukizaa,
Na kojale umauti?
Haiwezi kuwa hoja

Mshairi naachia, wengine kuendelea,
Sio vita ya mmoya, wanaharakati wajua,
Na wajinga wasojua, budi ukweli kujua,
Mwapiga ngoma ya kifo, kucheza acheze nani?
Walemavu tukizaa,
Na kojale umauti?
Haiwezi kuwa hoja