Friday, February 17, 2012

Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

BATI waweza kutia, uwanja ukaanua,
Mipaka ukaitia, kujenga wadhamiria,
Ila hili majaliwa, hata ukitia nia,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Ujenzi ni majaliwa, na mtu kuandikiwa,
Msingi wanaoitia, hadi wakamalizia,
Ni wachache walokuwa, wengi wao hupwelea,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Hushidnwa kuendelea, katikati kuishia,
Bado ipo yao nia, ila uwezo wapwaya,
Mahitaji yazidia, kuliko kinachoingia,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Na hili jema kujua, mtu unapojaliwa,
Muumba ukamjua, na dhamira kumwachia,
Hubariki yalokuwa, hadi yaje kutimia,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Msingi ukanyanyua, imara uliokuwa,
Kisha kuta ukatia, na lenta kuimwagia,
Na boriti kufungia, paa ukalipaua,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Milango ukafungia, madirisha nayo pia,
Fenicha ukazitia, makabati yalokuwa,
Na vyumba kujipmbia, kadri unavyojua,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Neru ukamiminia, na kumwaiya chokaa,
Na rangi kuziwania, zote zinazovutia,
Nje ukamalizia, na bustani kukua,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Ukuta kuzungushia, ulinzi ukiamua,
Na kuondoa udhia, jirani waliokuwa,
Na geti kujiwekea, tena la kujifungua,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Na kengele ukatia, hodi ukazikataa,
Na taa kumulikiwa, hata usiku ukiwa,
Na ving'ora vikajaa, wevi wapate kimbia,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Siku ikajafikia, ya wewe kujahamia,
Ziraili akatua, na roho kuichukua,
Wengine wataingia, wewe hautaingia,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

Yako haiwezi kuwa, huwa ya atayenunua,
Au mrithi akiwa, ataka kuitumia,
Wewe kwana kuhamia, ulikoishandaliwa,
Mtu kuzungusha bati, si hakika ya ujenzi!

No comments: