Monday, April 29, 2013

Sunday, April 21, 2013

Nyumba isiyo na haki


Nyumba ikosayo haki, baba huwa mnafiki,

Limbwata ikimwashiki, ya wana hatoafiki,

Akaachia mikiki, rabsha na taharuki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!

 

Biblia hutaliki, na Daudi hasemeki,

Qurani haifunguki, ya Selemani kucheki,

Akili zao riziki, na kisha umamuluki,

Nyumba isiyo na haki, maisha haijengeki!

 

Wangeata unafiki, mistari ina haki,

Wasingejaribu hiki, hofu ingetamalaki,

Ujinga wauafiki, dunia haisomeki,

Nyumba isiyo na haki, milele haisimamiki!

 

Nyumba ikosayo haki, baba huwa mnafiki,

Limbwata ikimwashiki, ya wana hatoafiki,

Akaachia mikiki, rabsha na taharuki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!

 

Nuru haimpeleki, na aendako haafiki,

Katikati huafiki, akakwaza ushtaki,

Akawa haaminiki, na leke halithaminiki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!

 

Huzaa huambiliki, na mkubwa unafiki,

Ya usawa na ya haki, yawe kwake hayasikiki,

Wakasepa washtaki, yawe hayaeleweki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!

 

Ya haki akataliki, na kuikwaza milki,

Baraka ikahamaki, na hekima kuishtaki,

Ukazuka umamluki, pia nao uzandiki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!

 

Nyumba isiyo na haki, wevi wataibariki,

La kweli halitamkwi, na uongo huafiki,

Wema ukawa kisiki, waovu hawautaki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!

 

Umma huudhhaki, yeye ndio mwenye haki,

Kusema wasidiriki, wanaihofia dhiki,

Ila wakitaharuki, nao huja kuhamaki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!

 

Huukataa uzandiki,  na kubwaga unafiki,

Wakaililia haki, kila kona kutamalaki,

Ukaisha umamluki, kwa kumhofu Maliki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!

 

Nyumba yetu ibariki, ewe bwana mtoa haki,

Hakikisha hawafiki, wote wenye unafiki,

Kiwatibue kisiki, wawe juu hawaamki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina amani!

 

Huzaa huambiliki, na mkubwa unafiki,

Ya usawa na ya haki, yawe kwake hayasikiki,

Wakasepa washtaki, yawe hayaeleweki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!

 

Madaraka  huwanoki, injini haziamki,

Ya mwana hawashtuki, ila yao huhamaki,

Usanaa huulaki, sera wakaiafiki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina amani!

 

Umma huudhhaki, yeye ndio mwenye haki,

Kusema wasidiriki, wanaihofia dhiki,

Ila wakitaharuki, nao huja kuhamaki,

Nyumba isiyo na haki, huwa haina imani!

 

 

Tuesday, April 9, 2013

SHETANI WA NA MIMI NICHINJE !


 

Shetani wa na mimi nichinje

 

ASILI tunaijua, itokako Tanzania,

Mababu waliamua, nani wa kutuchinjia,

Mwaikana historia, na utu kuuchezea?

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Tuliungana jamii, nasara na islamiya,

Ndugu tukawaachia, kazi ya kutuchinjia,

Mbegu tukiitambua, Ibrahimu kuanzia,

Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na alegee!

 

Yaliyoishaamuliwa, vipi twaja yafukua,

Makaburi kuyazua, walo hai kuwatia,

Au mnalololijua, sisi bado kulijua?

Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na alegee!

 

Yapo ya kuzungumzia, nchi ikaendelea,

Barabara zatakiwa, vijijini kuingia,

Na madaraja kuzua, watu wakajivukia,

Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na alegee!

 

Mashamba yanatakiwa, kulima kulisha Tanzania,

Na kiasi kuongezea, dunia kuiuzia,

Kuchinja twapigania, hivi kweli twajijua?

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Hivi kweli twajijua, kwa tunayojisemea,

Au wehu watuingia, ya ovyo kujiamlia,

Dunia kutushangaa, mfano  tuliokuwa?

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Mengi tungelifikiria, ubora kujiongezea,

Afrika kutambua, ni darasa tumekua,

Sisi tukatangulia, na wengine kufatia,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Ya wa Kongo twaamua, sasa kwenda kurejea,

Kwanza tungejichungua, kama wazima raia,

Au tumeingiliwa, na walio ni vichaa,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Burma ukiangalia, kichaa kajizukia,

Ndugu anawachukia, na uadui kuwatia,

Hivi sasa awaua, na nyumba kuwaunguzia,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Iraqi na Syria, dini zinahujumiwa,

Wauana raia, kwa hata wasiyojua,

Ni vichaa wamekuwa, nchi zinateketea,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Amiri anatakiwa, katikati akakaa,

Mstari kuutia,  hakuna wa kuuchezea,

Maaamuzi yatakiwa, sio lawama kutoa,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Maji yanatusumbua, lazima kujivunia,

Majumbani kuingia, na mashambani kumwaa,

Kuchinja wito likiwa, naona tunafulia,

Shetani 'nami' nichinje, ashindwe na alegee!

 

Kongo wanatungojea, kwenda kuwahubiria,

Nchi ya kati nayo pia, uamsho yangojea,

Kimataifa tukiwa, thumni hatutapigania,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Masoko kujitafutia, nyie mngetangulia,

Wafuasi kufatia, sadaka wakajipatia,

Michango yao ikawa, na nchi kwenda chanua,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

Nchi ninaiombea, kuvuka hii balaa,

Kwa uongo kukataa, na ukweli kulilia,

Salama ya Tanzania, sote yatutegemea,

Shetani 'nami' nichinje, adhindwe na alegee!

 

ISIWE MIAKA HII NUHUSI !!!

 
Wakuu twawaambia, juu walioshikilia,
Macho yao kufungua, kujua kinachoendelea,
Wapunguze kusinzia, hali watu wauawa,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Awamu iloanzia, ndiyo inaendelea,
Urafiki ilizua, hadi mitano kwishia,
Kipindi kilofatia, ajabu zikazuliwa,
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
 
Kubenea kuanzia, asidi akamwagiwa,
Hadi leo analia, mbaya hajamjua,
Na wala hatujasikia, kama kapewa fidia,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Mwangosi akafatia, mchana akauawa,
Wakubwa wafatilia, hadithi hatujaijua,
Na bado hatujajua, wana kulipwa fidia,
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
 
Absalom kafatia, hadi uchongo kutiwa,
Uchunguzi waendelea, mwisho tutajionea,
Hekaya itayokuwa, ni rahisi kung'amua,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Umoja unatakiwa, mafia wameshaingia,
Waliko kuwafichua, na kubwa ni yao nia,
Nini wanaitakia, hii yetu Tanzania?
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
 
Waandishi mwatakiwa, ya kwengu kufatilia,
Ukweli mkaujua, ili kinga kuitwaa,
Mkiwa mwaangalia, kulia huwa tabia,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Haraka mnatakiwa, mitandao kuizua,
Nchi mkaichungua, na wabaya kuwajua,
Kama ni hongo wapewa, na nyie si mnayajua?
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
 
Huenda ndani kakaa, mbaya msiyemjua,
Au mahala katulia, kimulimuli akawa,
Mbele anatangulia, mumiani kufatia,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Ili nchi kuokoa, wamulikeni mafia,
Nchini walioingia, kuharibu Tanznia,
Mhanga kujitolea, salama wana kukaa,
Isiwe miaka hii, ni ya umwagaji damu!
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Huhalalisha kuua, ili cheo kupatiwa,
Au fedha kuzikwaa, kisha wakazichezea,
Yafaa kujiokoa, kwa wao kuwatambua,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
 
Mungu hawakujaliwa, shetani waabudia,
Ndivyo inavyokuwa, na roho wasiojaliwa,
Fisadi huabudia, ukuu sio raia,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
Twawaomba waheshimiwa, doa hili kulitoa,
Nchi inahujumiwa, kwa kuwa na sifa mbaya,
Tujali demokrasia, na uhai kwangalia,
Isiwe miaka hii, ya  historia nyeusi!
 
 

Tuesday, February 26, 2013

Mbinuze ni zilezile


Hilo nilitangazile, wa kujua akajua,

Silo linalonogile, mabichwa wakijitia,

Ngoma hii tuchezele, waalikwa twawajua?

Mbinuze ni zilezile, mwele kutibu mganga!


Majini na misukule, huko yalikotokea,

Zumari na vibwagile, mila havijaridhia,

Uliona wapi ndwele, ikaja ikawa dawa?

Mbinuze ni zilezile, ya kichwa kuwa mkia!


Wasemele walewale, kila kitu kujitia,

Wasiokuwa simile, na wakubwa kuwajua,

Wao wakajidhanile, vinara wameachiwa?

Mbinuze ni zilezile, ya juu kuwa ya chini!


Hawakujua upole, ya shujaa tabia,

Na uoga anogile, hadi akadharauliwa,

Na walii si mkwale, neema alijaliwa,

Mbinuze ni zilezile, kushoto kuwa kulia!


Maisha ni kuvukile, madaraja kupitia,

E, mwanangu Chaupele, budi hili kuridhia,

Nalo tulitafutile, halibaki ila dua,

Mbinuze ni zilezile, janibu kuwa ghaibu!


Mchangani liishile, dunia 'kaendelea,

Palepale ubakile, au nawe kufagiwa,

Ina wake wateule, nasi si tunaojua,

Mbinuze ni zilezile, rafiki kuwa adawa!


Waache na kimbelembele, yatakuja kutokea,

Hadharani wapandile, wakicheza kidedea,

Hapo hapo washukile, kwenye vumbi kwogelea,

Mbinuze ni zilezile, halali kuwa batili!


UKifikia kilele, ngwee hautopandia,

Hubakia kushukile, chini kwenda kurudia,

Ukajua lipandile, kushuka ni yake ndia,

Mbinuze ni zilezile, ukweli kuwa hadaa!


Mja hanayo milele, muumbwa kifo kapewa,

Na wakati ufikile, ndiyo ya mwisho hidaya,

Lazima uchukulile, na weye kuchukuliwa,

Mbinuze ni zilezile, mwele kutibu mganga!


Nyie sio wajuvile, haya mambo mwaelewa,

Na wao si waanzile, kitu kuwashtukia,

Zege letu polepole, na haliachi kolea,

Mbinuze ni zilezile, mwele kutibu mganga!


Na lengo ni lile lile, shabaha yenye kujua,

Wateule wenye ndwele, dawa yao kuijua,

Hakika ni wapitile, kuwasindikiza tabia,

Mbinuze ni zilezile, mwele kutibu mganga!


Adili namtanguzile, yanyooka yake njia,

Wala si wa kupindile, na kona kujikatia,

Vya kesho agawalile, mauti visivyojua,

Mbinuze ni zilezile, mwele kutibu mganga!




Atampa mlo gani

 
 
Sijaiona yakini, ninayo shaka moyoni,
Jini kuwa wetu mgeni, sijawa nayo imani,
Naugua ndanindani, wa kumwambia ni nani?
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Ijapo si Selemani, hubaini hadharani,
Namjua huyu nani, na kwenu haonekani,
Naye hajiamini, akinitia machoni,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Kuna mambo ya uani, hayawekwi barazani,
Huwa huyo afkani, kinyume anayeghani,
Hayawi ya msalani, kuyaleta sebuleni,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Mshairi mtu gani, kichwani hana maoni,
Ndivyo wanavyoamini, njia wasiobaini,
Kumbe wanajizaini, hatima yao shakani,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Mtu huyu mtu gani, humuoni kivulini,
Na tonge kwenda kinywani, kwake huwa hayumkini,
Wala kiu haioni, hata akiwa juani,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Ameniacha pembeni, simo mwake shaurini,
Hakunitaka maoni, wala mie najuani,
Yeye yuko kilingeni, hana asicho baini,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Kwa heshima ububuni, nimeingia mwandani,
Kofuli iko kinywani, jipya sintolibaini,
Ila nangaoja mwakani, yarudi ya ughaibuni,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Wengine walibaini, kwa shetani kumuamini,
Watakuwa nayo imani, na dunia kuiwini,
Hivi leo wa shakani, mbele nyuma hawaoni,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?
 
Wamebaki kujilani,  wenyewe kujizaini,
Yakawa kama utani, hawaoni tumaini,
Nchi iko nje ndani, na uchi wajibaini,
Baba kamleta jini, atampa mlo gani?