Monday, June 18, 2012

Ghorofa haina msingi



VIJANA wanaondoka, wazee wamewachoka,
Kisa wanahamanika, ukale unatukuka,
Na nchi wanaoshika, hawataki badilika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Msingi umeng'oleka, wa vijana watukuka,
Vibabu vyahangaika, upepo kuzuilika,
Kwao makubwa mashaka, hawana lenye hakika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Mafuriko yamezuka, maji yazidi mwaika,
Msingi unachimbuka, wazee wameridhika,
Utaifa unatoweka, kwa uchama kuushika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Babu ameshatoweka, wamebaki vibabuka,
Kwa yao kughafilika, na ya watu kubweteka,
Kaniki zimahamanika, vikoi pia na shuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Waizima Tanganyika, kama sio kunyongeka,
Wahofu ikifufuka, itakuja na mizuka,
Kukumbatia wataka, yao wanaoyataka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Tuteni inafanzika, na mabomu kupigika,
Wao wanayoyataka, kuyafosi kufanzika,
Watuzulia mashaka, kutugharimu viraka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Dunia sasa yataka, madogo ya kushikika,
Makubwa wanaepuka, huwezi kuimarika,
Vivuko hautovuka, mtoni utaanguka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Ushirika wanataka, si'noa iso talaka,
Ukitaka kuachika, pasiwe wa kukuteka,
Hili lisipofanyika, utata hatutaepuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Watu sasa wamechoka, ndani kuwa wawekeka,
Wataka yao kuzuka, hadhi yao kupangika,
Na mambo kunyooka, sio yazidi pindika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Katiba kama  kibaka, katu haitapendekea,
Ikizua ya kutaka, nani atasalimika ?
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Zabzibar wanaotaka, kura huru kupigika,
Kadhalika Tanganyika, Tanzania ikazuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Tatu ndizo tunataka, serikali za hakika,
Ya umoja kuiweka, kcuhangia ushirika,
Ndogo itayojengeka, na watu wenye hakika,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Na uchama kupunguka, utaifa kujengeka,
Na kisha ikajazuka, mikoa ya madaraka,
Mfano ukaushika, nchi hii kujengeka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Hili halina mashaka, ajira zitafufuka,
Mikoa ikichemka, ushindani ukazuka,
Uchumi utanyanyuka, na wakazi kuridhika,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Mikoa itajengeka, Unguja na Tanganyika,
Na Pemba kuerevuka, ukawaisha wahaka,
Kote nchi kujengeka, kwa ushindani kuzuka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Chama kisichoitaka, hiyo  yetu Tanganyika,
Sio cha Watanganyika, wajua walikotoka,
Sasa kumepambazuka, na ujinga watoweka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Utumwa tulivuka, leo ya nguvu mwataka ?
Weusi mmegeuka, wakoloni wa kuteka ?
Uhuru nusu yafika, nusu nyingine twataka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Tanganyika, tanganyika




Pacha alishatoweka, mmoja amebakia,
Wapi alipofichika, watu wataka kujua,
Mpotevu asemeka, raia kumfichua,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?


Tanzania twaitaka, izidi kuendelea,
Pia yetu Tanganyika upya ikazaliwa,
Tuweze yetu kushika, ikawa twajitambua,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?


Usawa haukufanzika, Tanganyika kuondoa,
Laana ikatufika, mpaka leo balaa,
Yao wanaoyataka, ndio visa wanazua,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Zanzibar na Tanganyika, ndiyo huwa Tanzania,
Mmoja akitoweka, ni kingine kitakuwa,
Msingi hautojengeka, chini utatumbukia,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Hakunao ushirika, upande ukaumia,
Na ubia huponzeka, upande kupendelea,
Ikifika kuhongeka, taabu kubwa inakuwa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Upofu umetufika, ukweli twaukataa,
Mbali sana itafika, Zanzibar itapaa,
Mamboye ikiachiwa, huru ikajifanzia,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Kadhalika bara pia, miko huru ikiwa,
Waziri mkuu akawa, n dio anaangalia,
Mbali sana itapaa, ngazi ya juu ikawa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Ni wanasiasa njaa, ukale waliosalia,
Zama wayang'ang'ania, kwa tija yasiyokuwa,
Kwenye juzi wabakia, utandawazi wakataa ?
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Mawaziri watajaa, pamwe na wabunge pia,
Bara na Zzanzibar, na kisha wale wa mkoa,
Ni shule tutajaliwa, viongozi kusomea,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Ushindani utazaa, mazuri yaliyokuwa,
Na watu bora kuibua, mikoani kuwajua,
Taifani kuingia, na ujuzi waliokuwa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Wakati umefikia, Tanzania kuchagua,
Na kama kuendelea, Tanganyika kurejea,
Mola atatujalia, tuyatakayo yakawa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?


Friday, June 1, 2012

D O D O M A


Mji mkuu umekwama, unashindwa kusimama,
Kimejikusuru chama, kubeba Darisalama,
Mshumaa unazima, kufikiria kuhama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Huko nyuma walisema, katikati na salama,
Nduli aliporindima, kila kitu kikagoma,
Miezi minane ngoma, wakaamba ni lazima,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Miezi minane ngoma, wakaamba ni lazima,
Hata ilipoyoyoma, meli ikazidi zama,
Mzee akanguruma, IMF akaitoma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Na wajanja wakachuma, uhunzi ulipokoma,
Babu alipotazama, cheche mwisho  akatema,
Kustaafu lazima, nchi  ibaki salama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Thelathini yatetema, mitatu ingali nyuma,
Toka wapya kuegema, na yao wakayafuma,
Bunge kweli limehama, na chuo kinasimama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Ila wizara zakwama, nani ataka kuhama,
Mizizi Darisalama, chini imeshajitoma,
Na bahari waipema, upepo mkavu Dodoma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Sokoine alihama, wao wakarudi nyuma,
Ndwele bado zarindima, zinafichwa ndarahima,
Yapo tusiyoyasema, kuelekea Kigoma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?
Wagogo washika tama, haijafika neema,
Ila nyama ya kuchoma, na shingoni zinakwama,
Maji yazidi yoyoma, kuiga Darisalama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?
Tabora kwenda lazima, na konani ni Kahama,
Reli yaota mtima, wananchi wanazizima,
Na sasa kwao tuhuma, kuyabeba mataruma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Nazi kaziye kugema, mnazi ukiufuma,
Kama hauna mtama, na maziwa yasimama,
Bongo zetu ziko nyuma, kuiunda zimekwama ?
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Au suti wazipima, na reli inaroroma ?
Vijana wakijituma, na mtaji wakauchuma,
Kutengeza watakwa, au sisi tunagoma ?
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Uamuzi ni lazima, kitu gani ni Dodoma,
Kuhama au kutohama, sasa wimbo unakwama,
Nchi isiyo azma, kwneda mbele ni gharama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Miaka inayoyoma, labaki vumbi Dodoma,
Twangonja mwenye huruma, ya kwetu kwnenda yakama ?
Uhandisi wansoma, au vitabu wachoma ?
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Karne hii kiama, kuyafanza tukikwama,
Intaneti kujitoma, vitendo tukavisoma,
Wenyewe tuna lazima, miundombinu kuchuma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au ni Dar es Salaam ?

Saturday, May 5, 2012

KIswahili kinazikwa



Watu wamenunuliwa, Kiswahili kukiua,
Ujanja wanatumia, wengine kuwahadaa,
Kumbe wao kulemaa, ndio wanakazania,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Ugiriki walikuwa, wa kwanza kwenye dunia,
Elimu kupalilia, mengi tusiyoyajua,
Hadi leo tunajua, mema yaliyozaliwa,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Ila walihadaiwa, dharau ikawajaa,
Lugha wakapuuzia, Kilatini kuingia,
Walipokujashtukia, marehemu imekuwa,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Walipokujashtukia, marehemu imekuwa,
Kimataifa yapwaya, ngumu kujaheshimiwa,
Uzito imepungua, ukimwi kuiingia,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Kilatini nacho pia, siku kilipozainiwa,
Wasomi wakajitia, tajiri tu wanafaa,
Na wakubwa walokuwa, lugha hiyo kuijua,
Walipokujashtukia, marehemu imekuwa,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Masikini kuambiwa, kubwa kwao imekuwa,
Hawafai kuijua, haitowasaidia,
Kumbe imehukumiwa, kaburini kuingia,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Zipo nyingi lugha pia, katika hii dunia,
Wakubwa walipopwaya, ulinzi wakaachia,
Mageni kukumbatia, madawa yakawalevya,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Na pale walipolewa, lugha zao kujifia,
Ni watumwa wamekua, inawacheka dunia,
Laiti wangelijua, haya yasingetokea,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Yatufunza historia, lugha uwezavyo kuua,
Hapa kwetu Tanzania, ndicho sasa chatokea,
Bungeni imefikia, wauangaji  waingia,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Laana nawaombea, mema wasiyoitakia,
Ianze kwao kutua, na kizazi kufatia,
Kama wakija kuua, lugha yetu asilia,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Masikini mwatakiwa, lugha yenu kutetea,
Kwa uchumi imejaa, si fukara nawambia,
Ila wasiojaliwa, udni wanatutia,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Kiswhili mashalaa, kutawala kinafaa,
Tena sio Tanzania, hata pia na dunia,
Kiarabu kimejaa, themanini yake mia,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Kiarabu kimejaa, thamania asilimia,
Kama chaweza wafaa, kwanini sisi kuvia,
Ila tumelogewa, wanyonyaji kutunywea?
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Hasira nimeitia, na kweli nawaambia,
Viongozi walokuwa, dhambi wametufanyia,
Na alam tutatia, Kiswahili waliua,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

KIONGOZI maridhia, kuenziwa Tanzania,
Lugha atakayeamua, Kiswahili kutumiwa,
Wengi wapate jaliwa, elimu kuendelea,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Wengi wapate jaliwa, elimu kuendelea,
Lugha wakifundishiwa, hadi daktari kuwa,
Ikiwa wanaridhia, nyingine watazijua,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Ikiwa wataridhia, nyingine watazijua,
Tena wawe wachagua, na sio kuamriwa,
Kiarabu kikifaa, basi wataendelea,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Kiarabu kikifaa, hiyo sawa itakuwa,
Kichina chafaa pia, maabara wataingia,
Huko watajisomea, hata pia lugha mia,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Lakini kuendelea, chetu tutakitumia,
Hadi tafiti kutia, wenyewe kuzitumia,
Siri tukajitunzia, sio kila mtu kutujua,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Mapeni wamechukua, Mwingereza kuyatoa,
Mfukoni wakatia, lugha yetu kuiua,
Na uzungu kujitia, lipi wanalolijua?
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Hebu sasa angalia, Uchina imeshapaa,
Na India nayo pia, juu juu waelea,
Kisa yao kutumia, na si cha kung'ang'aniwa,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Yarabi nakulilia, lugha kutuhifadhia,
Waovu kutowaachia, wasije wakakiua,
Kije sisi kutufaa, na vizazi vyetu pia,
Kiswahili kinazikwa, na sisi twaangalia?

Ndugu zetu Waarabu



Nimekuja kugundua, ahali sikuwajua,
Ila walotulalia, akili kutuchezea,
Hadi kuwaabudia, na sasa tunapotea,
Ndugu zetu Waarabu, na wala sio wazungu !

Damu nimeigundua, kila pembe yaenea,
Dini waliichukia, mpya na asilia,
Nasara wakavamia, athari kuziondoa,
Ndugu zetu Waarabu, na wala sio wazungu !

Ila hawakujaliwa, ulinzi umebakia,
Mwenyewe kaangalia, hadi leo kufikia,
Haifai kumwachia, uamsho watakiwa,
Ndugu zetu Waarabu, na wala sio wazungu !

Hapa linalokusudiwa, dini yetu kurejea,
Huku tunajitambua, Kiswahili tulipewa,
Vyama tukikitumia, mbali sana tutapaa,
Ndugu zetu Waarabu, na wala sio wazungu !

Vyuo mnangojewa, kuja kujianzishia,
Elimu ikaitoa, kwa lugha pacha zikawa,
Kiswahili na Arabia, tulivyokwishajaliwa,
Ndugu zetu Waarabu, na wala sio wazungu !

Vyuo vikuu pia, lugha kuzifundishia,
Hadi dokta wakawa, ndugu zetu Tanzania,
Na kisha kufuatia, Afrika ikapaa,
Ndugu zetu Waarabu, na wala sio wazungu !

Themanini kwayo mia, ni yake asilimia,
Maneno Kiarabia, Kiswahii imetwaa,
Hili ukizingatia, lugha kujua inafaa,
Ndugu zetu Waarabu, na wala sio wazungu !

Gele wanatuonea, Wahausa Nigeria,
Kama wao wangekuwa, hatua wangeshachukua,
Na mazuri yakajaa, na wala sio balaa,
Ndugu zetu Waarabu, na wala sio wazungu !

Kitu hatujapungukiwa, yabaki kuzitumia,
Unyonge tukajivua, na asili kuringia,
Kiingereza kitapwaya, wallahi nawaambia,
Ndugu zetu Waarabu, na wala sio wazungu !

Ndugu zetu twawajua, umoja tunatakiwa,
Yetu kuja fanikiwa, kitu kimoja i dua,
Vingine tukiachia, lazima tutahujumiwa,
Ndugu zetu Waarabu, na wala sio wazungu !

Rafiki zetu Wachina



Kasumba yatuhadaa, magharibi kwangalia,
Mugabe keshatwambia, nyakati zimefikia,
Mashariki kuingia, rahisi kukubaliwa,
Rafiki zetu Wachina, na wala sio wazungu !

Funguo za kuendelea, Magharibi zafulia,
Asia ndiko kwafaa, kuuza na kununua,
Hamuoni yatokea, au vipogu mmekua?
 Rafiki zetu Wachina, na wala sio wazungu !

Wachina tunawajua, mengi wametusaidia,
Akili tukijaliwa, hawa kuwashikilia,
Mengi watatupatia, kielimu tukajua,
Rafiki zetu Wachina, na wala sio wazungu !

Treni walitujengea, kwanini kutofufua,
Meli wanajiundia, na magari nayo pia,
Hata ndege wanajua, sio tena kununua,
Rafiki zetu Wachina, na wala sio wazungu !

Kompyuta wazifua, na simu wajiundia,
Sawasawa tukiingia, yote haya twajivunia,
Sisi tunawakimbia, kwingine kuwaendea ?
Rafiki zetu Wachina, na wala sio wazungu !

Tunazifata hadaa, na wajanja walokuwa,
Waliozusha balaa, wakaiumiza dunia,
Na Mungu kumshukia, watu wake wakaua?
Rafiki zetu Wachina, na wala sio wazungu !

Mola tunamshtakia, hukumu yake kutoa,
Wanaotung'ang'anizia, mbali sana kutofikia,
Mapema kuwaumbua wakweli tukachagua,
Rafiki zetu Wachina, na wala sio wazungu !

Qatar onyesha njia



Qatar nawasifia, Aljazeera tangazia,
Milango mwaifungua, nchi zetu kuendelea,
Wazungu watuhadaa, shere wanatuchezea,
Qatar onyesha njia, wengine wafuatia !

Ugonjwa wanaujua, pia dawa waijua,
Ni sisi kuwaingia, wapate tusaidia,
Macho watatufungua, mengi sana kuyajua,
Qatar onyesha njia, wengine wafuatia !

Uchumi tumekalia, wazungu watuchezea,
Pipi wanatuigaia, dhahabu twawaachia,
Ujinga tumejaliwa, si mdogo ulokuwa,
Qatar onyesha njia, wengine wafuatia !

Ninakuomba Jalia, hili kuliangalia,
Wema kutuchagulia, wakaweza kutufaa,
Na udugu kuungia, walio na manufaa,
Qatar onyesha njia, wengine wafuatia !