Wednesday, October 31, 2012

Rais pia raia

KATIBA ya kutwokoa, pande zote kwangalia,
Juu huvunja sheria, kama chini nao pia,
Ovyo tukiachia, yaja kutugeukia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Sana ukiangalia, udhibiti watakiwa,
Nafasi ikichezewa, tunageuzwa majuha,
Nchi wakaichezea, tukabakia kulia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Kuwabana yatakiwa, baya kutotutendea,
Na kama tukilegea, wenyewe tunaumia,
Nchi huja kuigawa, vitani tukaingia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Madhambi ukichungua, si chini yaanzia,
Huwa kama ni mvua, juu inakotokea,
Ni wapambe haramia, njia humchanganyia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.
Katika hii dunia, watu wananunuliwa,
Nje wakajinunulia, nchi yao kujakuwa,
Na sisi tulio raia, ikawa twadharauliwa,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Tafakuri asokuwa, tajiri humnunua,
Wao akatumikia, sio nchi kuifaa,
Na hapo mkifikia, udikteta huzua,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Kuwa chini ya sheria, mahakama juu kuwa,
Hofu itawaingia, nafasi wakichukua,
Kuthubutu huhofia, mabaya kutufanzia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Mahakama chini kuwa, nchi ataichezea,
Fujo akatufanyia, kisha kutusingizia,
Haki ikajapotea, matatani kuingia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Jaji mkuu raia, wapaswa kumridhia,
Bunge wakalitumia, yeye likamteua,
Rais huyu ikiwa, huwa zavizwa sheria,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Kuna walionunuliwa, na wao wananunua,
Mfukoni akaitwia, Nyerere katuambia,
Aibu kuwa 'takuwa, nchi kama Tanzania,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Mama yetu ni sheria, na katiba juu yawa,
Kila hali yatakiwa, nyufa zote kuondoa,
Tusije tukajaliwa, kuja rais kichaa,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Ikawa yake sheria, yamlinda kwa udhia,
Dhambi akazizamia, huku twamuangalia,
Amin mnamjua, Uganda yaliyotokea,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Mali akazichukua, na ovyo kujifujia,
Hakuna la kumzuia, tukabaki twazubaa,
Na nyingine kuchukua, Uswizi akazitia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Mke, wana na jamaa, utajiri kuwagea,
Miradi akaiua, ili wao kuwafaa,
Nasi tukayaridhia, kwani hatunayo njia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Usultani kuzua, japo tuliukataa,
Watoto akatamia, cheo chake kuchukua,
Uarabuni twajua, mambo waliyoyazua,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Rais kushtakiwa, lazima kukubaliwa,
Kama akinunuliwa, hataka kumuondoa,
Watu akiwanunua, awe ameshaumia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Wananchi kuwaambia, si chini waliokuwa,
Ila juu wakalia, katiba wakiijua,
Wanaweza kumwondoa, madudu akifanzia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Budi hofu kumtia, nguvu yetu kuijua,
Kazi si kuichezaya. ila ya kuogopewa,
Ovyo tukiachia, midubwana waingia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Zama za kuwasifia, hivi sasa zajisia,
Kazi wamekusudiwa, mzigo kuuchukua,
Tena huru budi kuwa, bila wao kutumiwa,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

Ahadi namuachia, hii ni yake dunia,
Naye analoamua, ndilo hasa linakuwa,
Na wasiojisadia, hawezi wasaidia,
Rais pia raia, wawe chini ya sheria.

T U N Z O H I Z I T U N A T O A

Tunzo tunawapatia, kwa sifa zilizopewa,
Hadharani twazitoa, kila mtu kuzijua,
Haki tumeangalia, na zote zahifadhiwa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo watu kununua, ukubwa kujipatia,
Hamsini ukitoa, huziganga zao njaa,
Vikundi ukinunua, ngazi za juu kupaa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo jilie nyamaza, yetu kutoyasikia,
Wakubwa tunawatunza, juu waliopitia,
Kisha wakaeneza, kesho yatakayotuua,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya ahadi hewa, nayo twawazawadia,
Kwa ahadi kuzitoa, ukweli zisizokuwa,
Tamaa ikabakia, maajabu kutokea,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo nyumba ni anasa, ustwai motokaa,
Na njaa ikitokea, ni chakula kitakuwa,
Karamu kuiandaa, wale raha Tanzania,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo fisadi ni ndugu, hauwezi mkataa,
Hii ni ya kichwa sugu, kinachong'aa kipaa,
Kutunza wetu undugu, kusahau inafaa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo umaskini dili, misaada kuinyakua,
Wazungu yao akili, burungutu kuachia,
Mtalalia ukili, dhahabu huku watwaa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo wazungu wa unga, kwa wote wanaojaa,
Wenetu wawachabanga, wao ukwasi wakwaa,
Vidagaa kuwafunga, mapapa huru raia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo chakula kibovu, pia na hiyo mbolea,
Kwa wale wote werevu, wapatao kwa kutuua,
Mungu awape wangavu, hadi roho kujitoa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo za kuteuliwa, akili kutoumia,
Sio wa kuchaguliwa, mkoa ukaulilia,
Pasiwe na kidedea, mkoa wahujumiwa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya kubaguliwa, wengine kupendelea,
Hata wasiotufaa, kazi wakaajiriwa,
Maeneo hufulia, yanangoja ogelea,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo fisadi kufaa, wala sio kumuachia,
Huyu mkweli shujaa, atakuja kuwafaa,
Vile tulivyojilia, 'usije jitapikia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo utumwa sheria, wapewe wanasheria,
Haki wanaojiuzia, dhulluma wakaitia,
Hata wasione haya, kungoja wanachopewa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo kilimo cha njaa, ni ujanja kutumia,
Mitumba kuinunua, trekta kama bandia,
Mfukoni ukatia, hela inayozidia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo geuza kibao, haki wanaozinunua,
Kisha wakajiuzia, kwa wakubwa walokuwa,
Tajiri kuwatumia, kama tambaa la mafua,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo rushwa tapakaa, kwa wanaoiachia,
Huku ndani wanalia, ipunguzeni jamaa,
Aibu mnatutia, kila mtu anajua?
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo mikopo hadaa, wapakue na pakua,
Kidogo ukishatoa, kingi ukakichukua,
Nchi yataka kuliwa, ipate kuendelea,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo urongo tumia, wajinga bado wajaa,
Ukweli ukazuia, hakuna watalojua,
Mkono ukishatia, mara moja ni kunawa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo udhibiti duni, mameneja wachukua
Wasiokuwa makini, vya kwao kuangalia,
Na pengine yumkini, watawala nao pia,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya kutofatilia, wengi hii wamepewa,
Yenyewe yajiendea, Mola anasaidia,
Utabiri kuutoa, vigumu haitakuwa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo nifae upate, wachache wazawadiwa,
Awali kupanga kete, zinduko kuzinduliwa,
Mwana ni simupopote, huwepo yasiyokuwa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya mwaga machozi, kuwapa waso hatia,
Akili wasioenzi, kwa nguvu kuzitumia,
Hawanzi mazoezi, mkosa kutambliwa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya maji upupu, mpita njia kumwagiwa,
Na kuachwa utupu, nguo unapozivua,
Ukavitupa vikapu, samaki kujiozea,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya hawa wenetu, wa kwanza kuangalia,
Halafu rafiki zetu, wale kinachobakia,
Asiyekuwa mwenetu, kesho kumfikiria,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya mlipa pigwa, kodi yako kutumiwa,
Wewe mwenyewe kupigwa, kwa silaha za kutungua,
Mgalagala kuagwa, fukweni mchanga hujaa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya maji tope, vijijini kujinywea,
Kisha wazuka mapepe, eti tumeendelea,
Na weusi si weupe, wakoloni weshakuwa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ua yafaayo, mfano kujitegemea,
Na michezo kufulia, pasiwe kuendelea,
Wote tunawapatia, hili waliochangia,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya mikopo njaa, watu wetu kuwafaa,
Hii ni ya ujamaa, kama vile kijamaa,
Tundu tunalitumia, cha kwetu  kupitishia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo mifuko ulaji, kuuza na kununua,
Kugawa kwetu mtaji, unene kupindukia,
Wahiji wanaohiji, sisi kazi kupakua,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo za kuwaibia, fukrara wasiojua,
Mifuko kuitumia, ya kwenu nyie kujaa,
Kila mkipungukiwa, ni kisima mwayazoa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo za simu iba, tafiru wanazotwaa,
Mianya wakaiziba, vyamani ilikojaa,
Mlalahoi kukabwa, kdiogo wakachukua,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya nchi gizani, umeme mtaji kuwa,
Tukiingia nuruni, neema itapotea,
Muhimu kuwa gizani, wafadhili kukamua,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo 'Baah' Ibrahimu, kama kondoo tukawa,
Hata yasiyo na hamu, tukaacha kukosoa,
Twapiga maktaimu, eti mbele twatembea?
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya mweupe bora, hotelini kuwatia,
Na weusi ni hasara, hawajui kutumiwa,
Tena wazidi ukora, na vifo kusingizia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya kula vya umma, kila wakijiuzia,
Wakaziziba tuhuma, na mengine kuhadaa,
Ubepari ni unyama, tumeanza jionea,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunza ya kifaurongo, sauti kuzisikia,
Katiba kupa mgongo, kelele amri ikawa,
Na mwana mlea zongo, haki hana, akapewa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo mipango sanaa, kipangwacho kutokuwa,
Ikawa waigizia, kama lililotokea,
Watu wabaki wakiwa, dhihaka wanafanziwa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo udhalililishaji, midude tunagawia,
Wapate la moto taji, zamu yao ikitua,
Karamu ubabaishaji, duniani huishia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo miradi Ulaji, cha mbele kikitolewa,
Utaifa uhitaji, tumbo linatangulia,
Ambayo sasa wahiji, hata wasio na njaa,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya sahaulisha, madai kutojibiwa,
Watu wakakorofisha, la leo likachelewa,
Ila yao kuyapasha, usiku wakajilia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo yake potezea, nayo hapa yaingia,
Hoja inapoibuliwa, hewani kaishia,
Bengeni yanaanzia, ikulu ikadandia,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo la wala sinia, kisahani wakatoa,
Matumbo walojaliwa, na akiba kumegewa,
Nundu wanaozilea, kifuani zilojaa,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo chama - baba mama, ukoo na familia,
Tamalaki wajituma, Jetwa wakamfikia,
Kuliokufa hekima, ikabakia udhia,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya kubebeshana, takataka kuchukua,
Kisha ukazilipia, aghali isivyokuwa,
Huku hali wafulia, chakula chakuishia,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya njaa wanyama, hifadhini kuwatoa,
Uchumi ukakoroma, yasiyokuwa yakawa,
Wewe ukawa kiyama, cha wanyama Tanzania,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Yuraniamu uhai, tunzo inayotwimbia,
Ienziye maslahi, na ubinafsi kukua,
Hii wote watawahi, uhai wanaotania,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Tunzo ya dhahabu dili, awamu ya tatu yatwaa,
Walivyojaliwa akili, thamani bue kugawa,
Na mzuka kukabili, mwalimu nao alia,
Tunzo hizi tunawapa,  kwa kambi ya washikaji !

Tunzo ya ng'ombe bure, aghali zinazokuwa,
Wamdhihaki Nyerere, na kujifanza wajua,
Na wenye kiherehere, nchi kuja kuiua,
Tunzo hizi tunawapa,  wamiliki Tanzania !

Thursday, June 21, 2012

Nikipendacho si mwili


Nikipendacho mpenzi, ni roho na moyo wako,
Sio mwili wala ngozi,  huisha kwenye maziko,
Viwili hivyo vya enzi, hata huko niendako,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Ni roho na moyo wako, nikipendacho si  mwili,
Na katika uhai wako, hivyo kwangu ndio mali,
Na mimi kila niliko, njema hutakia hali,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Nikipendacho ulimi, usiokuwa muhali,
Daima unaojihami, kutotia idhilali,
Ukataao rasmi, umbeye kuuhimili,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Nipendacho adili, maovu haufumi,
Ukawa kwangu kandili, na ndia yangu ya lami,
Mitego kuikabili, kwangu ukawa ami,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Na roho niipendayo, makuu isiyokuwa,
Heshima ujengayo, bila ya kulaumiwa,
Tamaa isiyo nayo, haliye unaridhia,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Roho isiyo kinyaa, na matapishi kujaa,
Ndani inayotulia, yangu kunihudumia,
Mola inayomhofia, mabaya ikakimbia,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Mema ilodhamiria, kwa mchana na usiku,
Machozi inayotoa, uchamungu na shauku,
Inayowasaidia, walo kule, walo huku,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Moyo ninaoutaka, ovyo usiotamani,
Ujajuayo mashaka, ya uchu wa duniani,
Kila siku huridhika, kipatacho mkononi,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Kwa mwili tunaponzeka, usizo nazo akili,
Watu tukadangayika, wengi tukawa anzali,
Mitihani kuanguka, tuwe daima twafeli,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Mwili mkubwa ajali, bure unathaminiwa,
Hata usio akili, na udhaifu kujaa,
Wenye giza si kandili, mushiriki ulokuwa,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Rijali na wanawali, mwishowe  wakaanguka,
Zidhoofu zao hali, yakawafika mashaka,
Pasiwe na afadhali, iwe vuta na chanika,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Waweza upenda mwili, mtu akose akili,
Na rijali na wanawali, kizazio bilkuli,
Kikawa chote muhali, kujaliwa ya akili,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !

Nenda kaoe akili, nakushauri bilali,
Mwili ni kitu muhali, uitakapo akili,
Ni mkubwa ubahili, bongo kwake ni ajali,
Nikipendacho si mwili, ni roho na moyo wako !


Mganga hadai mchicha



Mchicha hadai mganga, lakini hudai kuku,
Maombi akiyachonga, si ya mia ni ya buku,
Hata  akiwa ni mwanga, ajua hili si huku,
Mganga haagizi tui, aagizacho ni nazi !

Na katu hatojivunga, eti akadai yai,
Ila kama la kuroga, viza lisilostahi,
Kamuone akimwaga,  ni maji wala si chai,
Mganga haagizi tui, aagizacho ni nazi !

Mganga haombi kaniki, ila khanga na baibui,
Tena ni ya urafiki, si Mchina hajawahi,
Mengine hashughuliki, kwa kitenge hufurahi,
Mganga haagizi tui, aagizacho ni nazi !

Mganga haombi hela, mizuka watakuomba,
Faraji sio farijala, kama maziwa akiomba,
Haombi kama ya kula, ni ya  simba ataomba,
Mganga haagizi tui, aagizacho ni nazi !



Monday, June 18, 2012

Ghorofa haina msingi



VIJANA wanaondoka, wazee wamewachoka,
Kisa wanahamanika, ukale unatukuka,
Na nchi wanaoshika, hawataki badilika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Msingi umeng'oleka, wa vijana watukuka,
Vibabu vyahangaika, upepo kuzuilika,
Kwao makubwa mashaka, hawana lenye hakika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Mafuriko yamezuka, maji yazidi mwaika,
Msingi unachimbuka, wazee wameridhika,
Utaifa unatoweka, kwa uchama kuushika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Babu ameshatoweka, wamebaki vibabuka,
Kwa yao kughafilika, na ya watu kubweteka,
Kaniki zimahamanika, vikoi pia na shuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Waizima Tanganyika, kama sio kunyongeka,
Wahofu ikifufuka, itakuja na mizuka,
Kukumbatia wataka, yao wanaoyataka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Tuteni inafanzika, na mabomu kupigika,
Wao wanayoyataka, kuyafosi kufanzika,
Watuzulia mashaka, kutugharimu viraka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Dunia sasa yataka, madogo ya kushikika,
Makubwa wanaepuka, huwezi kuimarika,
Vivuko hautovuka, mtoni utaanguka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Ushirika wanataka, si'noa iso talaka,
Ukitaka kuachika, pasiwe wa kukuteka,
Hili lisipofanyika, utata hatutaepuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Watu sasa wamechoka, ndani kuwa wawekeka,
Wataka yao kuzuka, hadhi yao kupangika,
Na mambo kunyooka, sio yazidi pindika,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Katiba kama  kibaka, katu haitapendekea,
Ikizua ya kutaka, nani atasalimika ?
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Zabzibar wanaotaka, kura huru kupigika,
Kadhalika Tanganyika, Tanzania ikazuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Tatu ndizo tunataka, serikali za hakika,
Ya umoja kuiweka, kcuhangia ushirika,
Ndogo itayojengeka, na watu wenye hakika,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Na uchama kupunguka, utaifa kujengeka,
Na kisha ikajazuka, mikoa ya madaraka,
Mfano ukaushika, nchi hii kujengeka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Hili halina mashaka, ajira zitafufuka,
Mikoa ikichemka, ushindani ukazuka,
Uchumi utanyanyuka, na wakazi kuridhika,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Mikoa itajengeka, Unguja na Tanganyika,
Na Pemba kuerevuka, ukawaisha wahaka,
Kote nchi kujengeka, kwa ushindani kuzuka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Chama kisichoitaka, hiyo  yetu Tanganyika,
Sio cha Watanganyika, wajua walikotoka,
Sasa kumepambazuka, na ujinga watoweka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Utumwa tulivuka, leo ya nguvu mwataka ?
Weusi mmegeuka, wakoloni wa kuteka ?
Uhuru nusu yafika, nusu nyingine twataka,
Barafu ilogandika, kwanza budi kuyenyuka,
Mafuriko na tufani, ghorofa haina msingi !

Tanganyika, tanganyika




Pacha alishatoweka, mmoja amebakia,
Wapi alipofichika, watu wataka kujua,
Mpotevu asemeka, raia kumfichua,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?


Tanzania twaitaka, izidi kuendelea,
Pia yetu Tanganyika upya ikazaliwa,
Tuweze yetu kushika, ikawa twajitambua,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?


Usawa haukufanzika, Tanganyika kuondoa,
Laana ikatufika, mpaka leo balaa,
Yao wanaoyataka, ndio visa wanazua,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Zanzibar na Tanganyika, ndiyo huwa Tanzania,
Mmoja akitoweka, ni kingine kitakuwa,
Msingi hautojengeka, chini utatumbukia,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Hakunao ushirika, upande ukaumia,
Na ubia huponzeka, upande kupendelea,
Ikifika kuhongeka, taabu kubwa inakuwa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Upofu umetufika, ukweli twaukataa,
Mbali sana itafika, Zanzibar itapaa,
Mamboye ikiachiwa, huru ikajifanzia,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Kadhalika bara pia, miko huru ikiwa,
Waziri mkuu akawa, n dio anaangalia,
Mbali sana itapaa, ngazi ya juu ikawa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Ni wanasiasa njaa, ukale waliosalia,
Zama wayang'ang'ania, kwa tija yasiyokuwa,
Kwenye juzi wabakia, utandawazi wakataa ?
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Mawaziri watajaa, pamwe na wabunge pia,
Bara na Zzanzibar, na kisha wale wa mkoa,
Ni shule tutajaliwa, viongozi kusomea,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Ushindani utazaa, mazuri yaliyokuwa,
Na watu bora kuibua, mikoani kuwajua,
Taifani kuingia, na ujuzi waliokuwa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?

Wakati umefikia, Tanzania kuchagua,
Na kama kuendelea, Tanganyika kurejea,
Mola atatujalia, tuyatakayo yakawa,
Tanganyika, Tanganyika, pacha wake Zanzibar;
hivi nani kamuua ?


Friday, June 1, 2012

D O D O M A


Mji mkuu umekwama, unashindwa kusimama,
Kimejikusuru chama, kubeba Darisalama,
Mshumaa unazima, kufikiria kuhama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Huko nyuma walisema, katikati na salama,
Nduli aliporindima, kila kitu kikagoma,
Miezi minane ngoma, wakaamba ni lazima,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Miezi minane ngoma, wakaamba ni lazima,
Hata ilipoyoyoma, meli ikazidi zama,
Mzee akanguruma, IMF akaitoma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Na wajanja wakachuma, uhunzi ulipokoma,
Babu alipotazama, cheche mwisho  akatema,
Kustaafu lazima, nchi  ibaki salama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Thelathini yatetema, mitatu ingali nyuma,
Toka wapya kuegema, na yao wakayafuma,
Bunge kweli limehama, na chuo kinasimama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Ila wizara zakwama, nani ataka kuhama,
Mizizi Darisalama, chini imeshajitoma,
Na bahari waipema, upepo mkavu Dodoma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Sokoine alihama, wao wakarudi nyuma,
Ndwele bado zarindima, zinafichwa ndarahima,
Yapo tusiyoyasema, kuelekea Kigoma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?
Wagogo washika tama, haijafika neema,
Ila nyama ya kuchoma, na shingoni zinakwama,
Maji yazidi yoyoma, kuiga Darisalama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?
Tabora kwenda lazima, na konani ni Kahama,
Reli yaota mtima, wananchi wanazizima,
Na sasa kwao tuhuma, kuyabeba mataruma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Nazi kaziye kugema, mnazi ukiufuma,
Kama hauna mtama, na maziwa yasimama,
Bongo zetu ziko nyuma, kuiunda zimekwama ?
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Au suti wazipima, na reli inaroroma ?
Vijana wakijituma, na mtaji wakauchuma,
Kutengeza watakwa, au sisi tunagoma ?
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Uamuzi ni lazima, kitu gani ni Dodoma,
Kuhama au kutohama, sasa wimbo unakwama,
Nchi isiyo azma, kwneda mbele ni gharama,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya DC ?

Miaka inayoyoma, labaki vumbi Dodoma,
Twangonja mwenye huruma, ya kwetu kwnenda yakama ?
Uhandisi wansoma, au vitabu wachoma ?
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au mapya Ulaya ?

Karne hii kiama, kuyafanza tukikwama,
Intaneti kujitoma, vitendo tukavisoma,
Wenyewe tuna lazima, miundombinu kuchuma,
Makao yetu makuu, hivi bado ni Dodoma :
Au ni Dar es Salaam ?