Thursday, December 13, 2012

U R I T H I


BABA anamhofia, ataiaga dunia,
Naye anajiandaa, urithi kuuchukua,
Fursa azichambua, pahali pema kukaa,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Kisa nimehadithiwa, mizungu kilichotiwa,
Ngano ya kuenguliwa, toka tambo za dunia,
Inayotia fadhaa, na  hamasa kupungua,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Kumbe nilivyoyajua, sivyo yalivyotokea,
Kielelezo si dawa, zaidi walichengua,
Ndani wakayafikia, mimi nisiyoyajua,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Fadhaa yawaumbua, neno hili kusikia,
Uraibu umekuwa, pombe waisiyoelewa,
Mlevi sasa kichaa, kila mtu abambua,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Kumbe laini kikiwa, ugumu ndani hulea,
KIla kinachong'aa, hakiachi kufubaa,
Navyo vinavyovutia, mvuto huja kwiishiwa,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Rai niliitengua, haikuwa ya raia,
Mwenzi aliyezidiwa, wala hakuwa mzawa,
Mwana aliyejitia, hakuwa Mtanzania?
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Watumwa waliokuwa, danguroni wamekaa,
Nta sasa wazaa, na mnato kuutia,
Mzinga kupalilia, kuvuna ya ushujaa?
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Hatua wasiotwaa, aibu wanatutia,
Umma wahofu ubia, walikwishauandaa,
Wafanzao wayahua, na kwetu sisi hadaa,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?


Lenu langu litakuwa


Wanyonge wanapokuwa, na mimi nitaingia,
Lao nikalichukua, mpka langu likawa,
Ndicho nilichoumbiwa, musrati kufwatia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Sikuumbiwa dunia, njii hii napitia,
Lengo nimejiwekea, uangavu kufikia,
Kuona msiyojua, wala kuyafikiria,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Hili si la kuombewa, ni tunu ikijaliwa,
Mimi nalifurahia, kuishi naaazimia,
Msongo kwangu likawa, shinikizo kunitia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Maisha nakadiria, taishi kutumikia,
Vingine naviachia, hili kwake nahamaia,
Nikaanzisha ubia, milele kuendela,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Inshallah naitia, siachi kukumbukia,
Neema najiombea, na kinga nikapatiwa,
Akitacho Jalia, na hakika ndilo huwa,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Hili ninalielewa, vingine sijafikiria,
Nafuai nimeitoa, ruksa sijajaliwa,
Yeye ndiye huamua, mimi wa kufatilia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Nia akibarikia, lake ndilo hutimia,
Mimi atanitumia, abdi niliyekuwa,
Lake nikaitikia, na kazi kumfanzia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Muhula akinigea, vyema kutumikia,
Hadi nitapofikia, wengine wakachukua,
Yake akaniridhia, na mimi kumridhia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Akhiri amesikia, yangu atayaridhia,
Nakili lililokuwa, uwakili sijapewa,
Ila kushuhudia, kwa lile ninalojua,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Makombora yanarudi

 YATUPWA kuhilikia, safu wakazipangua,
Asubhi kiingia, mipango wanajipangia,
Jioni ikiishia, tathmini hutolewa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hadithi kuendelea, hurushwa yakarejea,
Mwamvuli wahofia, mlengwa anatumia,
Uyahudi wangejua, huyo wangemnunua,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Wabaki kusingizia, adui kawarushia,
Kumbe ilivyokuwa, yenyewe yajirudia,
Siri hawajaijua, wanazidi kuumia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Aliko hawajajua, nasibu waitumia,
Kapelekewa hidaya, wala hazikupokelewa,
Wadhani ana  kinaya, hayajali ya dunia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Ganzi limeshaingia, ovoovyo yarushiwa,
Lengo sijalitambua, wala pia yake nia,
Hadhira inashangaa, kitali kinavyokuwa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Na mimi najiachia, mlinzi atanifaa,
Kadari sijaijua, pengine hii ndo njia,
Wito nilishaitikia, hutoweza kunitoa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hili sikuigilizia, starehe naijua,
Tena ninafurahia, kulikosa si ridhaa,
Wanyonge ni yangu bia, hunywa hadi nikalewa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hayanipiti masaa, bila kuwaulizia,
Hali zao kuzijua, na nini wapungukiwa,
Sinacho nitakitoa, kukopa nilichopwa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Mkononi huachia, mtupu nikabakia,
Hali nikiangalia, h aziwezi fanania,
Ila raha naijua, wala siwezi kulia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Nderemo inapokuwa, peponi hujisikia,
Na kilio wakilia, ninauvaa ukiwa,
Yao niemshakusudia, ya kwangu budi yakawa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Laiti mngelijua, kusita isingekuwa,
katika hii dunia, uongozi ni kufaa,
Uongozi wa kubwia, na starehe karaha,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hesabu nishahisabia, wa sikio, kusikia,
Ulimi sikuachia, ila kwa kujizuia,
Lengo nalitarajia, Mwenyezi atajalia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Z I M A M O T O


PAPO kwa papo kuamua, pasi kuwa na bajeti,
Sifa za kuserubukia, shukrani kuambua,
Watu wakasujudia, na viatu kurambia,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Hayo ya kujinyanyua, walipokwishagukia,
Wakaondoa udhia, matope kwenda ondoa,
Huruma wakajiuzia, kwenye njaa na ukiwa,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Mamlaka kuyazoa, mtu ukajilimbikia,
Ukabaki kuamua, na wengine kushangaa,
Haiwi kushangilia, ubaya ukitiokea,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Nchi inayo mikoa, kama nchi ilokuwa,
Uhuru isipopewa, nchi tutaichezea,
Mbali hatuafikia, tutaanza kupagawa,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Inatakiwa mikoa, mipango yao kuzua,
Na uongozi ridhaa, wenyewe kujichagua,
Hatua wakajipangia, wapi wataka fikia,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Dar  wakingojea, yao kuja kuamua,
Mikoa itafubaa, na riadha kufulia,
Mbali hawatafikia, kuchekwa iwe tabia,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Uchumi kuunyanyua, wakazi wanatakiwa,
Yao wakayamua, na ulua kuutia,
Kadiri wakaagua, wawezavo jinasua,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Nasaha nimeitoa, naomba hoja kutoa,
Manani akajalia, upevu kuufikia,
Nchi ni kubwa gunia, sio rahisi kujaa,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Si mshairi wa chama


UCHAMA naukataa, haki nazingatia,
Ni mwana demokrasia, pembeni aliyekaa,
Haki kuilingania, itulie mizania,
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Nateta demokrasia, izagae Tanzania,
Udikteta uchwara, chembe kutobakia,
Yale ya chama kimoya, yatoke yasiyofaa,
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Usawa naupigania, fakiri kusaidia,
Vijijii wlaiokuwa, huko kusikoangaliwa,
Hali juu kuinua, makwao kujivunia,
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Ukinitaka ubia, na wew weza ingia,
Vijijini kuingia, ya kwao tukayanoa,
Bongo tukiwapatia, kufikiri wanajua,
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Mipango ukiandaa, kusoma wanaelewa,
Mita ukiwaambia, ni kipimo wakijua,
Umbali ukiongea, wnaaweza kufikia,
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Wazo ukilichimbua, lulu wataigundua,
Haba na haba ikawa, mbele weza endelea,
Mzawa asipojifaa, hivi nani kumfaa?
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !

Kwenu ukiwajengea

 Kwenu ukiangalia, na kwingine saidia,
Haki kuianglaia, usawa ukatimia,
Sio huku kuchukua, kule tu ukawafa,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Mizani kusimamia, usawa kuangalia,
Haki ukashadidia, bila kitu kupungua,
Rehema mkatunukiwa, kwa dhuluma kuiondoa,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Katiba ninavyojua, ulinganifu sheria,
Pasiwe wa kuonewa, wala wa kupendelewa,
Sasa kinachotokea, mashaka kinatutia,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Kwa wapinzani huvia, tawala wakachanua,
Au swahiba pakiwa, mambo yatazinduliwa,
Kwa wengine kunapwaya, nani wa kuangalia ?
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Kwa wakubwa nasikia, ridhaa wakajengewa,
Wengine wakililia, hiyo ndoto waambiwa,
Mizani naihofia, pande inaegemea,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Wanakokupachagua, kwa wakubwa walokuwa,
Wadogo yarukwa njia, hadi mbali kuendea,
Mkubwa palipokuwa, sasa ndio huangaliwa,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!

Hili sijaliridhia, wala sintolliridhia,
Hofu yangu nawambia, ila ninaidhania,
Jema halitajaliwa, mabaya laja kuzua,
Kwenu ukiwajengea, na kwingine angalia!


Hakuna mkamilifu


WAJA hatukujaliwa, ukamilifu kupewa,
Kiasi tunapungua, na wengi tunajijua,
Kadari hatukupewa, ya kuweza kutimia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!


Mjua mwenye kujua, sababu zake ajua,
Upungufu kutegea, kisa chake akijua,
Ukamili kabakia, kuhodhi mwenye kutoa,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Tusije kujihadaa, vingine tukadhania,
Wapambe waliokuwa, miungu kutuumbia,
Wasifu anatakiwa, Mola asiyezaliwa,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Viumbe  hatukupewa, ruhusa kujiumbua,
Kwa kelele na kuzua, yale tusiyojaliwa,
Kuridhika ndiyo njia, na kikomo kukijua,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Mwanzo wetu twaujua, ila mwisho twaotea,
Uchamungu kiingia, nalo tutakadiria,
Hapa si watu wa kukaa, hii njia  twatumia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Kwa kitambo kulijua, tutaiacha dunia,
Visa tungevipangua, na hoja kujijengea,
Hakuna wa kubakia, usawa tungenuia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Haki tungeangalia, tusende mbele kulia,
Na dhuluma kupungua, moto kutokuumbua,
Na adili kutufaa, mizani ikatimia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Fukara tungewafaa, na wala si kuulea,
Tungepiga vita njaa, na sio kuitumia,
Watu tukawanua, na mfukoni kutia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Tungelijua masaa, huwa ni yetu dunia,
Na fumba na kufumbua, hapa tunaezuliwa,
Isingekuwa ridhaa, uongo kupalilia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!

Umma tusingeuubia, na ufukara kuutia,
Udhibiti tungetia, haramu kuikataa,
Halali tukailea, h adi mwisho wa dunia,
Hakuna mkamilifu, hata awe mchamungu!