Monday, August 26, 2013
CHA BURE KINGINE GHALI
Humuachia amali, ajuaye jipangia,
Fahari kuwa fahali, dongo lililoumbwa,
Akasema kwa mithali, mjinga hujibomoa,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !
Rahisi nyingine ghali, mwanangu nakuambia,
Ikubali idhilali, kidogo kuongezea,
Ukajitoa muhali, ili kesho kukufaa,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !
Mbishi hatokubali, bei atapigania,
Kwa kutojua ukweli, aali akakosea,
Muuza akijakubali, thamani keshapangua,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !
Huzigundua dalili, haki hatoiridhia,
Kwa kuondoa idhilali, yeye huyakubalia,
Kwisha kuwa kulhali, maisha yakaendelea,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !
Haambiliki anzali, huna la kumuelezea,
Hudhani astahili, daima ni kusifiwa,
Akakataa kubuli, na hadaa kununua,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !
Humuachia amali, ajuaye jipangia,
Fahari kuwa fahali, dongo lililoumbwa,
Akasema kwa mithali, mjinga hujibomoa,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !
MWENYYE THAMANI
Wengine wa kutumiwa, kwa azijuazo ndia,
Kwa ndogo na kubwa gia,yeye keshajipangia,
Yote keshakadiria, thamani kajipangia,
Kila mtaka ukubwa, mwenye thamani ni yeye!
Kiasi anakijua, kaishawahesabia,
Wagawaji kachagua, vibaba kwenda vitoa,
Kikubwa kinachobakia, kuwadi watapatiwa,
Kila mtaka ukubwa, mwenye thamani ni yeye!
Kama shehe anajua, firdausi katwaa,
Kasri keshajipangia, huko aenda ingia,
Bawabu watamjua, wakati keshaingia,
Kila mtaka ukubwa, mwenye thamani ni yeye!
Mbawa atajiotea, na mbinguni akapaa,
Akaicheka dunia, ubora alishajaliwa,
Daraja akatumia, ya kwake kuyaamua,
Kila mtaka ukubwa, mwenye thamani ni yeye!
Huiba akafidia, kule kulikopungua,
Asopendwa huonewa, kidogo kutoachiwa,
Mbavu wakazikazia, dhiki kumshambulia,
Kila mtaka ukubwa, mwenye thamani ni yeye!
Ila wanaomsifia, karamu watafanziwa,
Vitu kuteremshiwa, hata wasivyofikiria,
Ipambwe yao dunia, mauti kuyatania,
Kila mtaka ukubwa, mwenye thamani ni yeye!
FISADI AKISHAANZA
Nani amekwambia, eti kushiba ajua,
Huyo akishaanzia, daima huwa na njaa,
Tumbo huzidi panua, kama Jetwa hujakua,
Fisadi akishaanza, huwa haachi fasidi!
Fisadi mwana balaa, haramu hatokimbia,
Hutaka kuongezewa, hadi mapipa kujaa,
Raha akajionea, eti kwa k uangalia,
Fisadi akishaanza, huwa haachi fasidi!
Wa ndani humuibia, pasipo ya kutambua,
Cha nje kinapokuwa, kwa deni aweza ua,
Moja ataikimbilia, mia akaziachia,
Fisadi akishaanza, huwa haachi fasidi!
Nikahi anayoijua, ya nje ikitokea,
Kifua huikingia, wa ndani wakaasiwa,
Mitupu waliyokuwa, nani atajilambia?
Fisadi akishaanza, huwa haachi fasidi!
Fisadi mwana tamaa, na sifa huziogea,
Daima huzililia, jasmini yakatiwa,
Udi na uvumba pia, Uarabu kujitia,
Fisadi akishaanza, huwa haachi fasidi!
Hujaribu mwanakuwa, kuikusanya dunia,
Akashindwa kutambuwa, yeye ndiye atakiwa,
Kukusanywa na kutiwa, kwenye la sahau jaa,
Fisadi akishaanza, huwa haachi fasidi!
Mola atampangia, nini ataka fanyiwa,
Na siku kujiwekea, hakika akaitia,
Pasina kujitambua, nyuzi zilizobakia,
Fisadi akishaanza, huwa haachi fasidi!
Ya Afu nakuangukia, karama kunigawia,
La kesho wasilojua, miye nikalitambua,
Mbali nao nikakaa, na kuistadi dunia,
Fisadi akishaanza, huwa haachi fasidi!
HASARA KUBWA KWA N CHI
Rahisi kununuliwa, mfukoni akatiwa,
Kisha akajatumiwa, mwenyewe kuja jiua,
Hajui anachojua, msukule keshakuwa,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !
Atafuta ganga njaa, sio kiongozi kuwa,
Dhiki akaiondoa, katikati amekaa,
Wabaya kuwaondoa, watu wanaonunua,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !
Kujiamini silaha, yeye asiyochukua,
Kubebwa keshazoea, kila kitu hufanziwa,
Kutafuta hatajoua, sikuzote wa kupewa,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !
Huiabudu dunia, Mola akamkimbia,
Upepo akishatiwa, akazidi kuvimbiwa,
Hadi juu hujaa, kwenye anga akapaa,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !
Hapo anapofiikia, Mungu huja jidhania,
Wahyi akautoa, kwa amri zisokuwa,
Hajui la kutumiwa, wala la kufikiria,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !
Kiatu husiginia, watakaomsaidia,
Akili akadhania, pekee amejaliwa,
Kumbe hajajijua, kubaya aogelea,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !
MWENYE KUTOA KWA DHATI
HATAKI kuangaziwa, sadaka akiitoa,
Kwenye siri huingia, Molawe kumuachia,
Viumbe kutotegemea, kitu kumsaidia,l
Mwenye kutoa kwa dhati, tivii huiogopa!
Uungu huukimbia, na riziki kuzigawa,
Apendwaye akapaewa, asopendwa kuchukiwa,
Riziki akakatiwa, na matatani kutiwa,
Mwenye kutoa kwa dhati, gazeti huliogopa!
Mola humtangulia, afaaye ogopewa,
Ndiyo wa kutetemekewa, milki anayegawa,
Na ukuu kuwagiwa, wale anaochagua,
Mwenye kutoa kwa dhati, inteneti huogopa!
Mitihani aijua, kunaguka huhofia,
Asije kuteketea, badala kujiokoa,
Waliomtangulia, zao keshaelezewa,
Mwenye kutoa kwa dhati, redio huzikimbia!
Nafsi aitambua, ilivyojaa hadaa,
Uungu ikalilia, japo kifo chaingojea,
Ila uhai ukiwa, kila kitu hugombania,
Mwenye kutoa kwa dhati, tivii huiogopa!
Kazi moja aijua, mbingu zinaiongojea,
Ibada ya kutulia, na kisha kusaidia,
Kwa faragha kuamua, na kutenda vivyo pia,
Mwenye kutoa kwa dhati, gazeti huliogopa!
Hatonjojea mataa, na kamera kuletwa,
Dunia ipate mjua, ni nani aliyetoa,
Kwani anatambua, walipaji hawajawa,
Mwenye kutoa kwa dhati, inteneti huogopa!
Mlipaji katulia, yeye ajitazamia,
Malaika wahadithia, viumbe zao tabia,
Taarifa huletewa, wa kweli wakawajua,
Mwenye kutoa kwa dhati, redio huzikimbia!
mtu asiyejijua
Vyovyote anatumiwa, na wengine
kuwafaa,
Yeye kama chombo huwa, mashinani
kusagiwa,
Mtu kutojitambua, utumwa kwake
tabia!
Hushindwa 'jifikiria, sembuse
kufikiria?
Kama vile ndoo kuwa, au karai
kutumiwa,
Zege akalichangia, pasina na sifa
kuwa,
Mtu kutojitambua, utumwa kwake
tabia!
Dezo atanunuliwa, na walionunuliwa,
Mfukoni akatiwa, ndivyo sivyo
kutumiwa,
Vishilingi akipewa, tajiri
akajisikia,
Mtu kutojitambua, utumwa kwake
tabia!
Kwa cheo huzainiwa, hata wana
kuwaua,
Ukuu akauwania, kwa damu kujimwagia,
Hesabu akijaijua, hubaki kujijutia,
Mtu kutojitambua, utumwa kwake
tabia!
Mara huchanganyikiwa, misuli
kuitanua,
Kisha akaazimia, kuikusanya dunia,
Hajui hatobakia, dunia kumngojea,
Mtu kutojitambua, utumwa kwake
tabia!
Miaka keshahesabia, kisha motoni
kwingia,
Milele kwenda kukaa, kwa anayoyamua,
Laiti angetambua, vivyo asingetumiwa,
Mtu kutojitambua, utumwa kwake
tabia!
Roho inapotolewa, ndio ukweli hujua,
Tena sana akalia, dakika kuruhusiwa,
Mema akachangia, moto kwenda
ukimbia,
Mtu kutojitambua, utumwa kwake
tabia!
Rushwa hutaka kutoa, malaika kugawia,
Wapate kumuachia, dakika akasalia,
Ila hatohurumiwa, macho akayakodoa,
Mtu kutojitambua, utumwa kwake
tabia!
Huwezi kuwazaini
KUWA bingwa wa hadaa, na kofia
kuzivaa,
Kamwe hautojaliwa, wote wakakusikia,
Lako kulihudumia, ukweli ukauawa,
Huwezi kuwazaini, watu wote, pande
zote!
Idadi hutachukua, ya bure na
kununua,
Ndicho tulichoumbiwa, viumbe
tuliopotea,
Utumwani hujitia, wenyewe kwa
kuchagua,
Huwezi kuwazaini, watu wote, rika
zote!
Kamba huwa ni hidaya, mkononi
kuzitia,
Kisha kujitundukia, tunapoamriwa,
Amri kuzisikia, hata zilizo ukiwa,
Huwezi kuwazaini, watu wote, siku
zote!
Hatuwi wa kuchagua, ya kwetu
kufikiria,
Kubebwa tumezoea, hatutaki kutembea,
Kiyama kinatujia, hali twakiangalia,
Huwezi kuwazaini, watu wote, pande
zote!
Twashindwa kuyaamua, ya kwenda
kutuokoa,
Firdausi kuingia, pepo ya kuteuliwa,
Mithili isiyokuwa, wala haitatokea,
Huwezi kuwazaini, watu wote, rika
zote!
Twashndwa kujichagua, vikongwe
kukimbilia,
Mikongojo sisi kuwa, badala ya
kujisimamia,
Ushauri nautoa, bongo zetu kufungua,
Huwezi kuwazaini, watu wote, siku
zote!
Bongo zetu kufungua, kofuli
kuziondoa,
Funduo kuzitumia, Mola keshatupatia,
Njia mkishahofia, mbele kutoendelea,
Huwezi kuwazaini, watu wote, pande
zote!
Msije kuyayatuia, kwamba haya
mliambiwa,
Nanyi hamkusikia, dhihaka mkaitia,
Wa kweli anayejua, pande hatoegemea,
Huwezi kuwazaini, watu wote, rika
zote!
Rabuka namsifia, itihari kujaliwa,
Kweli nikapigania, na haki
kuigombea,
Japo fakiri nikiwa, ikawa yangu
ridhaa,
Huwezi kuwazaini, watu wote, siku
zote!
Subscribe to:
Posts (Atom)