Monday, August 26, 2013

HASARA KUBWA KWA N CHI


Rahisi kununuliwa, mfukoni akatiwa,
Kisha akajatumiwa, mwenyewe kuja jiua,
Hajui anachojua, msukule keshakuwa,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !


Atafuta ganga njaa, sio kiongozi kuwa,
Dhiki akaiondoa, katikati amekaa,
Wabaya  kuwaondoa, watu wanaonunua,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !

Kujiamini silaha, yeye asiyochukua,
Kubebwa keshazoea, kila kitu hufanziwa,
Kutafuta hatajoua, sikuzote wa kupewa,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !

Huiabudu dunia, Mola akamkimbia,
Upepo akishatiwa, akazidi kuvimbiwa,
Hadi juu hujaa, kwenye anga akapaa,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !

Hapo anapofiikia, Mungu huja jidhania,
Wahyi akautoa, kwa amri zisokuwa,
Hajui la kutumiwa, wala la kufikiria,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !

Kiatu husiginia, watakaomsaidia,
Akili akadhania, pekee amejaliwa,
Kumbe hajajijua, kubaya aogelea,
Hasara kubwa kwa nchi, kijana asojijua !


No comments: