Monday, August 26, 2013

Huwezi kuwazaini



KUWA bingwa wa hadaa, na kofia kuzivaa,

Kamwe hautojaliwa, wote wakakusikia,

Lako kulihudumia, ukweli ukauawa,

Huwezi kuwazaini, watu wote, pande zote!

 

Idadi hutachukua, ya bure na kununua,

Ndicho tulichoumbiwa, viumbe tuliopotea,

Utumwani hujitia, wenyewe kwa kuchagua,

Huwezi kuwazaini, watu wote, rika zote!

 

Kamba huwa ni hidaya, mkononi kuzitia,

Kisha kujitundukia, tunapoamriwa,

Amri kuzisikia, hata zilizo ukiwa,

Huwezi kuwazaini, watu wote, siku zote!

 

Hatuwi wa kuchagua, ya kwetu kufikiria,

Kubebwa tumezoea, hatutaki kutembea,

Kiyama kinatujia, hali twakiangalia,

Huwezi kuwazaini, watu wote, pande zote!

 

Twashindwa kuyaamua, ya kwenda kutuokoa,

Firdausi kuingia, pepo ya kuteuliwa,

Mithili isiyokuwa, wala haitatokea,

Huwezi kuwazaini, watu wote, rika zote!

 

Twashndwa kujichagua, vikongwe kukimbilia,

Mikongojo sisi kuwa, badala ya kujisimamia,

Ushauri nautoa, bongo zetu kufungua,

Huwezi kuwazaini, watu wote, siku zote!

 

Bongo zetu kufungua, kofuli kuziondoa,

Funduo kuzitumia, Mola keshatupatia,

Njia mkishahofia, mbele kutoendelea,

Huwezi kuwazaini, watu wote, pande zote!

 

Msije kuyayatuia, kwamba haya mliambiwa,

Nanyi hamkusikia, dhihaka mkaitia,

Wa kweli anayejua, pande hatoegemea,

Huwezi kuwazaini, watu wote, rika zote!

 

Rabuka namsifia, itihari kujaliwa,

Kweli nikapigania, na haki kuigombea,

Japo fakiri nikiwa, ikawa yangu ridhaa,

Huwezi kuwazaini, watu wote, siku zote!

No comments: