Monday, August 26, 2013

mtu asiyejijua

Vyovyote anatumiwa, na wengine kuwafaa,

Yeye kama chombo huwa, mashinani kusagiwa,

Mtu kutojitambua, utumwa kwake tabia!

 

Hushindwa 'jifikiria, sembuse kufikiria?

Kama vile ndoo kuwa, au karai kutumiwa,

Zege akalichangia, pasina na sifa kuwa,

Mtu kutojitambua, utumwa kwake tabia!

 

Dezo atanunuliwa, na walionunuliwa,

Mfukoni akatiwa, ndivyo sivyo kutumiwa,

Vishilingi akipewa, tajiri akajisikia,

Mtu kutojitambua, utumwa kwake tabia!

 

Kwa cheo huzainiwa, hata wana kuwaua,

Ukuu akauwania, kwa damu kujimwagia,

Hesabu akijaijua, hubaki kujijutia,

Mtu kutojitambua, utumwa kwake tabia!

 

Mara huchanganyikiwa, misuli kuitanua,

Kisha akaazimia, kuikusanya dunia,

Hajui hatobakia, dunia kumngojea,

Mtu kutojitambua, utumwa kwake tabia!

 

Miaka keshahesabia, kisha motoni kwingia,

Milele kwenda kukaa, kwa anayoyamua,

Laiti angetambua, vivyo  asingetumiwa,

Mtu kutojitambua, utumwa kwake tabia!

 

Roho inapotolewa, ndio ukweli hujua,

Tena sana akalia, dakika kuruhusiwa,

Mema akachangia, moto kwenda ukimbia,

Mtu kutojitambua, utumwa kwake tabia!

 

Rushwa hutaka kutoa, malaika kugawia,

Wapate kumuachia, dakika akasalia,

Ila hatohurumiwa, macho akayakodoa,

Mtu kutojitambua, utumwa kwake tabia!

 

No comments: