Monday, August 26, 2013
MWENYE KUTOA KWA DHATI
HATAKI kuangaziwa, sadaka akiitoa,
Kwenye siri huingia, Molawe kumuachia,
Viumbe kutotegemea, kitu kumsaidia,l
Mwenye kutoa kwa dhati, tivii huiogopa!
Uungu huukimbia, na riziki kuzigawa,
Apendwaye akapaewa, asopendwa kuchukiwa,
Riziki akakatiwa, na matatani kutiwa,
Mwenye kutoa kwa dhati, gazeti huliogopa!
Mola humtangulia, afaaye ogopewa,
Ndiyo wa kutetemekewa, milki anayegawa,
Na ukuu kuwagiwa, wale anaochagua,
Mwenye kutoa kwa dhati, inteneti huogopa!
Mitihani aijua, kunaguka huhofia,
Asije kuteketea, badala kujiokoa,
Waliomtangulia, zao keshaelezewa,
Mwenye kutoa kwa dhati, redio huzikimbia!
Nafsi aitambua, ilivyojaa hadaa,
Uungu ikalilia, japo kifo chaingojea,
Ila uhai ukiwa, kila kitu hugombania,
Mwenye kutoa kwa dhati, tivii huiogopa!
Kazi moja aijua, mbingu zinaiongojea,
Ibada ya kutulia, na kisha kusaidia,
Kwa faragha kuamua, na kutenda vivyo pia,
Mwenye kutoa kwa dhati, gazeti huliogopa!
Hatonjojea mataa, na kamera kuletwa,
Dunia ipate mjua, ni nani aliyetoa,
Kwani anatambua, walipaji hawajawa,
Mwenye kutoa kwa dhati, inteneti huogopa!
Mlipaji katulia, yeye ajitazamia,
Malaika wahadithia, viumbe zao tabia,
Taarifa huletewa, wa kweli wakawajua,
Mwenye kutoa kwa dhati, redio huzikimbia!
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment