Monday, August 26, 2013

CHA BURE KINGINE GHALI


Humuachia amali, ajuaye jipangia,
Fahari kuwa fahali,  dongo lililoumbwa,
Akasema kwa mithali, mjinga hujibomoa,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !

Rahisi nyingine ghali, mwanangu nakuambia,
Ikubali idhilali, kidogo kuongezea,
Ukajitoa muhali, ili kesho kukufaa,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !

Mbishi hatokubali, bei atapigania,
Kwa kutojua ukweli, aali akakosea,
Muuza akijakubali, thamani keshapangua,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !

Huzigundua dalili, haki hatoiridhia,
Kwa kuondoa idhilali, yeye huyakubalia,
Kwisha kuwa kulhali, maisha yakaendelea,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !

Haambiliki anzali, huna la kumuelezea,
Hudhani astahili, daima ni kusifiwa,
Akakataa kubuli, na hadaa kununua,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !

Humuachia amali, ajuaye jipangia,
Fahari kuwa fahali,  dongo lililoumbwa,
Akasema kwa mithali, mjinga hujibomoa,
Sasa nimeshatambua, rahisi nyingine ghali !

No comments: