Monday, August 26, 2013
BARUA
Barua nimepokea, pasina kujitambua,
Jina nishaling'amua, langu wala haikuwa,
Maudhui nashangaa, ni jambo nisilojua,
Barua uliyotuma, haikuwa na anwani !
Raha nilijisikia, namiye kuandikiwa,
Japo sikumtambua, aliyeniandikia,
Kusoma nikajitia, kwa juhudi kuuvmbua,
Barua uliyotuma, haikuwa na anwani !
Wallahi sikudadavua, wala kitu kutambua,
Ila nimechanganyikiwa, asili nisiyoijua,
Na sasa najiinamia, kuwaza na kuwazua,
Barua uliyotuma, haikuwa na anwani !
Dhamira sijaijua, wala lililokusudiwa,
Lengo sijalitambua, ramli sikujaliwa,
Kichwa ninaugulia, yote nataka kujua,
Barua uliyotuma, haikuwa na anwani !
Utata unenijaa, nasibu naichezea,
Geresha ingelikuwa, nia sijaitambua,
Mengine kuyang'amua, subira yahitajiwa,
Barua uliyotuma, haikuwa na anwani !
Mwanga ninaungojea, hili kuja niangazia,
Pengine nitagundua, japo palipoanzia,
Kisha nikaendelea, kufuma na kufumua,
Barua uliyotuma, haikuwa na anwani !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment