Monday, September 23, 2013
KATIBA BILA UWAZI
KATIBA tumeamua, tunaitaka mpya,
Na hili kufanikiwa, ni lazima kuchangia,
Kila unalolijua, lawza kukusaidia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Sera kutochakachua, kwa mifumo ya udhia,
Ikawa zinazuia, watu wetu kuchangia,
Nafasi wakatukua, kitu wasiochangia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Usije pembeni kaa, wengine ukaachia,
Yako hawatayajua, moyoni yaliyokuwa,
Mwenyewe ukitokea, hilo litazungumziwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Ya zamani kupitia, ni uzuri itakuwa,
Ukapata kuijua, kasoro zilizojaa,
Nawe ukaikosoa, na kuujenga ulua,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Yafaa kufikiria, ya leo na ya kuzua,
Mbele yatayotokea, njia kuyaandalia,
Iwe si kushtukiwa, mambo yakituchachia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Inafaa kuamua, ya wakuu wa mikoa,
Wawe ni wa kuteua, au wa kuchaguliwa,
Naona tunaumia, kwa hawa wa kuteua,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Ukubwa wauchukua, bila ya kupigania,
Wa juu wawatumia, ya kwao kufanikiwa,
Nasi katika mkoa, kitu hatutaambulia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Kadhalika na wilaya, kama nao wanafaa,
Au wengine wakawa, kwa bora iliyo njia,
Waweze kutumikia, bila uchama kutia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Na rais kuchagua, mikakati kuwazia,
Ni mikoa kuchagua, wasafi watu kadhaa,
Kisha wakaingia, chamani kuchaguliwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Ni ipi asilimia, ipate kukubaliwa,
Kidogo sana ikiwa, ridhaa inapungua,
Kubwa ikizingatiwa, bora zaidi yafaa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Kuungana vyatakiwa, vyama hapa Tanzania,
Gharama zikapungua, lazima isiyokuwa,
Vitatu vikibakia, nafuu tutaambulia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Na nchi kuyaamua, mbili au tatu zikawa,
Watu uhuru kuvua, ya kwao wakaangalia,
Isiwe kutawaliwa, na ndani waliokuwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Dola nayo kuamua, nguvu zinapoishia,
Hawa wanaotumiwa, pabaya watuchukua,
Juu wakiwa raia, nidhamuwataijua,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Mishahara twatakiwa, pia kwenda kuamua,
Vipi itakavyokuwa, utenzi kuzingatia,
Sio wanaopepewa, masultani wakawa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Vijana tunatakiwa, uhuru kupigania,
Na sio kujatumiwa, na wazee walokuwa,
Kisha wakatuhadaa, kama panzi tulokuwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Kisha wakatuhadaa, kama panzi tulokuwa,
Nao kunguru wakawa, riziki wajipatia,
Nasi bila kujijua, tuzidi kuangamia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Wazee mnatakiwa, kutumiwa kukataa,
Leo kuzungumzia, myapate manufaa,
Siasa kutowagawa, kwa vyama kuvitumia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Wazee mkapigania, yalo yenu manufaa,
Isiwe mnatumiwa, na waliovimbiwa,
Hili mkishguhulikia, yenu yatazingatiwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Watoto mnatakiwa, haki zenu kuzijua,
Na kisha kushikilia, katibani kuingia,
Pasaiwe lisilokuwa, kwa vyovyote itavyokuwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Umoja mnatakiwa, wanawake kuulea,
Msije mkatumiwa, na wahuni walokuwa,
Nao wakishawagawa, yenu kutoangalia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
Baraka nawaombea, ndugu zangu Watanzania,
Yenu yakifanikiwa, na wangu watafanikiwa,
Nayo yakliharibiwa, nao huharibikiwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!
AINA ZA UGAIDI
Mambo mengi ugaidi, jambo moja halijawa,
Nabonyeza kwako hodi,Upate kuyatambua,
Si moja kufaidi, na mengi kutokujua,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Ufisadi ugaidi, japo hatujalitambua,
Nao mkubwa mradi, duniani waenea,
Wengi wauona sudi, neema zinavyojaa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Rabsha inajinadi, dhana kila kitu kuwa,
Kwalo sijaona idi, kufaidi sijajua,
Si mmoja ugaidi, asa umeshatambua,
Naupandisha mdadi, kuushusha natakiwa,
Wa maneno ugaidi, sasa unachipukia,
Wasema kwa ukaidi, na vitisho kuvitoa,
Hii haikuwa jadi, yatuzushia balaa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Leo wanaofaidi, hawatakia kuachia,
Wafanza zote juhudi, wengi chini kudidimia,
Ili wabaki jadidi, juu wanashikilia,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Umeanza wa fisadi, mlo wote kupakua,
Hata dini kuritadi, lishe sababu ikiwa,
Akafanza ukaidi, kuipindua dunia,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Aidha wa ukaidi, na jeuri kuzitia,
Akachapwa mijeledi, mnyonge aliyekuwa,
Kisa ataka idadi, na vyanzo kuving'amua,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Kuna ule wa mdadi, na hasira kuvimbiwa,
Usimhofu Abadi, na vitisho kuvitoa,
Watu ukawafasidi, haki zao kuzitwaa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Uongo pia mradi, nao ni ugaidi pia,
Kweli zisiwe ahadi, bali uongo kujaa,
Asojua hafaidi, hadi akitindikiwa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Upo wa kutaradadi, utukufu kuombewa,
Au kwa zako juhudi, ukataka juu paa,
Asili ukakaidi, ikakutema dunia,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Kuna ule wa kijadi, na silaha kutumia,
Kwa bidii na juhudi, nguvu ukazitumia,
Cha wengi ukikinadi, na pengine kukitwaa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Kuna ule wa magadi, pa chumvi ukaitia,
Na wa kutumia radi, watu ukawatumia,
Ajuaye ni Wadudi, vipi inavyotokea,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Upo ule wa hasidi, wengine kuwachukia,
Na ukiwapa ahadi, iwe isiyotimia,
Isikughasi fuadi, kawaida kwako kuwa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Kuna ule wa baridi, mtu kimya kukaa,
Hana kadi, hana kodi, yake yanajiendea,
Amtanguliza Hadi, hata pasipotakiwa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Na wasio maabuddi, Ibilisi huwavaa,
Yake waasiyakaidi, yeye akawatumia,
Haya yake ya mihadi, hadi mwisho kwenda kuwa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Baraza nataradadi, tawakali tangulia,
Usiipate nakidi, na hasara kuingia,
Si mmoja ugaidi, sasa umeshang'amua,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
Mwenye nguvu na mgodi, ndo' wa kumtambua?
Mwenye hisa na miradi, hatojanisingizia ?
Ayalilia Masudi, kuchora atarudia ?
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!
KATIBA YA WATANZANIA
Mola tunakulilia, batili kuikataa,
Halali kutupatia, kwa tunayoyatarajia,
Mama wa zetu sheria, mbele kumtangulia,
Katiba ya Tanzania, si ya chama kimoja !
Wamezuka waso haya, wajinga watudhania,
Ya kwao wapalilia, mchakato kupitia,
Ilhali tunajua, si halali yalokuwa,
Katiba ya Tanzania, si ya mtu mmoja !
Uchache wautumia, wingi wetu kufukia,
Sauti waikataa, yao wataka sikia,
Kisha waje kuamua, kizazi yasiyokifaa,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !
Nchi yetu twaijua, na makundi yalokuwa,
Akili ukitumia, wawakilishi twajua,
Wiano kuangaliwa, kwa wenyewe kuchagua,
Katiba ya Tanzania, si ya chama kimoja !
Mfumo tulishaamua, wa wingi sio umoya,
Sasa yanayotokea, yarejesha historia,
Chama kinasimamia, kisichokistahilia,
Katiba ya Tanzania, si ya mtu mmoja !
Uwakilishi ni njia, watu wote kufikia,
Sio sisi kutugawa, kwa vijisenti kutoa,
Kisha wakateuliwa, ndiyo ndiyo kwitikia,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !
Makundi tunayajua, na idadi nayo pia,
Hata waliokikataa, zamani kuhesabiwa,
Kipofu anawajua, barazani watakiwa,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !
Wawapuuza raia, kama vile ni bidhaa,
Wengine wananunua, na mfukoni kutia,
Mwalimu angeshangaa, ukubwa wa kututia,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !
Raia wanatambua, nani wamtarajia,
Barazani kwenda kaa, ili yao kutetewa,
Sasa wanachofanyiwa, zezeta waandaliwa,
Katiba ya Tanzania, si ya chama kimoja !
Wajuu waliokuwa, hawataki kusikia,
Maoni yanatolewa, dharau wanaitia,
Nchi utafikiria, haki yao imekuwa!
Katiba ya Tanzania, si ya mtu mmoja !
Kila wanaloambiwa, upuuzi wajionea,
Kama kawa kwendelea, pasi soni walla haya,
Ilhali tunajua, pabaya twaelekea,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !
NCHI iliahidiwa, katiba bora kupewa,
Idumu miaka mia, kizazi kufurahia,
Leo tunashuhudia, ya mwaka mmoja wazua?
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !
NCHI iliahidiwa, katiba bora kupewa,
Idumu miaka mia, kizazi kufurahia,
Leo tunashuhudia, ya mwaka mmoja wazua?
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !
Rabi twakuhimidia, tuepushe na balaa,
Hekima kuwapatia, wakuu waliokuwa,
Zuri wakaliamua, kuokoa Tanzania,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !
Rabana mwenye kujua, Bashiri uliyekuwa,
Upofu 'ngeliondoa, na busara kujalia,
Wakasimama raia, haki yao kupatiwa,
HIVI CHAMA KINA DIRA ?
KICHWA hutokijua, wala wapi ni mkia,
Kule unakodhania, uamuzi hutolewa,
Wao nao wangojea, wa chini kuja amua ?
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Pembeni tuliokaa, dhaifu mabaharia,
Wakati umeshaingia, chama chetu kukitwaa,
Dira tukakipatia, baharini kuelea,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Mashaka tunayazua, kwa uongozi kufifia,
Wengi tuloachia, kazi yao kusifia,
Kombakomba walokuwa, eti vyeo wangojea,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Uoga umetujaa, chinichini twasemea,
Ukweli tunaujua, na batili nayo pia,
Vipi tunaendelea, kama vile hii kawa?
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Mansuri kajitolea, ukweli kuutumbua,
Wazuka wa kuzomea, kumbe wanajishushua,
Ukweli ndio shujaa, daima tama adawa,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Watu tunawakimbia, wenyewe twajitumikia,
Pasi aibu na haya, kazi yetu imekuwa,
Huko tunakoeleka, walahi nakuhofia,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Kimya ninakikataa, tangazo hili kutoa,
Wenye chama watakiwa, ukweli kuutambua,
Tumeichagua njia, Mwalimu aliyokataa,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Kuongoza twatambua, ndilo tunalotakiwa,
Sasa tunaamriwa, kilingeni twatolewa,
Watu wanajionea, haya yote washangaa,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Tulishaongoza njia, si tu hapa Tanzania,
Afrika nako pia, pamwe nayo dunia,
Leo tumekuwa mkia, nyuma nyuma kufatia,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Falsafa imevia, wala hatunayo taa,
Gizani tunatembea, mambo kubahatishia,
Ya ndani wanaojua, pakupiga wapajua,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Wafofaa twaachia, kazi zetu kuzikwea,
Ovyo wanajifanzia, kepesti na kukopia,
Majilisi kiingia, kichekesho kinakuwa,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Hawasomi wakajua, na makosa kuyatoa,
Ndio wanaitikia, pasina kufikiria,
Uwakilishi wavia, na watu hili wajua,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Changamoto twaitoa, kwa upya kuzaliwa,
Wenye uchungu na nia,hivi sasa kujitoa,
Mkono nawaachia, sikufunga nafungua,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!
Katiba ikija mbovu
Vijana waangalia, tunachowaamulia,
Mushkeli kikijaa, yasije yakawafaa,
Hatua watachukua, adhabu kali kutoa,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!
Tuache jifikiria, kizazi kuangalia,
Ya leo tunayajua, kesho yasije zuia,
Maovu tuakayazua, kwenye pepo Tanzania,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!
Viongozi wayajua, ndo kisa kuyakemea,
Isitumike hadaa, baharini twaelea,
Pepo zitatuumbua, kichangani kuelea,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!
Macho tungeyafungua, tusome tuolosusia,
Mistari kujijua, kwa kujitafakaria,
Upofu tukijitia, wenyewe twaja kulia,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!
Tusije kuvumilia, mbovu tukajapatiwa,
Mishipa tutaizua, na pumzi kulipua,
Nchi ikawa balaa, pasiwepo pa kukaa,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!
Kwa hiari nayatoa, katikati nilokuwa,
Upande sijaegemea, mkweli wa Tanzania,
Haki nimepgiania, uhaini kuzuliwa,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!
Maradhi nayatambua, kwa waliokisinzia,
Haya tukiyaachia, pabaya twaelekea,
Sangari kuing'ofoa, hiyo ni ya shamba dawa,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!
Jalali twakulilia, uongozi kuzindua,
Wasije tuamulia, yawe ukimwi mpya,
Nchi itateketea, hali twaiangalia,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!
Saturday, September 21, 2013
K A T I B A I J U U Y A W O T E
Juu atayejitia, asimame kutwambia,
Nani amemchagua, juu ya wengine kuwa,
Kigezo kilichotumiwa, na bei aliyotoa,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Wapi imeruhusiwa, mstari kudadavua,
Nasi hatutambishia, njia tutamuachia,
Ila tunavyotambua, kwa juu hapatakuwa,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Juu anayejitia, ataka kuichezea,
Usanii kujitia, asiyejua sanaa,
Ujuzi hakujaliwa, mabavu ayatumia,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Usanifu kujitia, na uashi anajua,
Yule tunayetambua, hayo kamwe hakusomea,
Ni msiba twangojea, hali tunachekelea,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Jengo akitujengea, laja kutuangukia,
Na wengine kufukiwa, kuzikwa hai wakiwa,
Wajifanzao wajua, kisha mbali wakakaa,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Sisi wote ni raia, wakuu na wasiokuwa,
Hakuna alozidia, katiba yatuambia,
Vipi ikaja ikawa, mmoja juu akwaa?
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Ubinafsi twahofia, kwa madhara na nazaa,
Ndiio maana usia, huu wa historia,
Wote chini twarejea, nini tena kuambiwa?
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Chama kinapojitia, nchi kinaipindua,
Hila wakizitumia, ufidadi wajitia,
Batili kuitumia, halali wakaachia,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Yao wajiandalia, na palizi kuitia,
Kwenye shamba la kuzua, kabaila kakodiwa,
Kondeni bomu zajaa, zisije tulipukia,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Aihadaa Tanania, wakati haijasinzia,
Kono fukoni katia, halali avichomoa,
Vingine vyamwagikia, chini vikatapakaa,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Yajichokea dunia, kuizoea mizaha,
Guu likijimbia, na kuutunga usahaa,
Siku itapowadia, uchungu tutasikia,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !
Friday, September 6, 2013
D U N I A H A I W A P E N D I
Haiwapendi dunia, japo yawavumilia,
Uungu wanaojitia, na kiburi kuwajaa,
Huonekana mzaha, Mola wanamfanzia,
Haiwapendi dunia, uungu wajitiao!
Ovu wanaotishia, hata kwa waoto pia,
Watu wanawachukia, na kuwaona kinyaa,
Huwa mkubwa udhia, japo ukavumiliwa,
Haiwapendi dunia, waishio kwa vitisho!
Wafutuao vifua, na maguvu kutumia,
Ilhali wakiishiwa. upepo waja pungua,
Kinyamkera ni jaa, kila kitu huchukua,
Dunia haiwapendi, watunishao vifua !
Wajanja kupotezea, ni nadra kuridhiwa,
Kamba wanaachiiwa, za kwenda jitundikia,
Nao bila kujijua, vichwa wanavipanua,
Dunia haiwapendi, walokubuhu hadaa !
La mtu wasosikia, songombingo kujendea,
Hekima wakajitia, kwa busara kuitoa,
Rahisi kuvumiliwa, na sio kukubaliwa,
Dunia haiwapendi, ushauri wasotaka!
Wanaotaka kupaa, kwenye mwezi kutembea,
Hali ni hii dunia, wanayoikanyagia,
Huru watajisikia, ila deni walitwaa,
Dunia haiwapendi, wale wanaojiona !
Wale wanaounuia, kila mtu kuwajua,
Hata pasipowafaa, wakawa ni wa kuingia,
Nafsi hujichubua, dhihaka ikawajaa,
Dunia haiwapendi, wajifanzao sinema !
Wanaojilimbikizia, hadi wana kuvimbiwa,
Kisha wakajiachia, mitegoni kuingia,
Salama huwaachia, mbali nao ikakaa,
Dunia haiwapendi, waozao kwa fasidi !
Fahari wanaojitia, na mbwembwe kushangilia,
Dunia kuwazuzua, kisha ikawachezea,
Viumbe wasiojijua, si aghali kupotea,
Dunia haiwapendi, wale wanaojidai!
Ukuu wanaolilia, mafuu wengine kuwa,
Ngazi wakazitumia, kisha teke kuzitia,
Huku moyo wakomaa, uovu kuendelea,
Dunia haiwapendi, wale wanaojikweza !
Kelele waliojaa, hata kwa wasoyajua,
Katikati kwingilia, madebe wakapasua,
Huonekana nazaa, kicheko cha kuchefua,
Dunia haiwapendi, viumbe wenye kelele!
Ulimi wasiolea, ovyovyo kutumia,
Maneno wakayatoa, ya kuwakwaza raia,
Huonekana balaa, si wa kutegemewa,
Dunia haiwapendi, ulimi wasiochunga!
Uongo wanaoujua, wakashindwa ukataa,
Huwa ni waongo pia, wanafaa kuhofiwa,
Shimoni huja watia, machoni wawaangalia,
Dunia haiwapendi, waabuduo uongo!
Wageuzwao bidhaa, watu wakawanunua,
Kisha wakawatumia, kwa mengi yasiyokufaa,
Hawa ukiwaachia, hatiani unajitia,
Dunia haiwapendi, wageuzwao bidhaa !
Wasiokuwa na haya, maovu kutohofia,
Waziwazi wakavua, ilhali watembea,
Ni watu wa kuoghofya, ukiweza mbali kaa,
Dunia haiwapendi, haya wanaoikosa !
Kisasi waliojaa, na huruma kusinyaa,
Mola hatowaangalia, kiyama kikiingia,
Mgongo hugeuziwa, na motoni kwenda kaa,
Dunia haiwapendi, kisasi wanaojaa!
Mema hutarajia, uoza wakisifiwa,
Vichwa kukomalia, na mifuko kulegea,
Ila siku ikiingia, tundu hawatoshuhudia,
Dunia haiwapendi, wanaokosa huruma !
Watu wanaopakazia, makosa wakawazulia,
Kesi wakabambikiwa, na waovu kuwavaa,
Adhabu wakaipewa, chanzo wasichokijua,
Dunia haiwapendi,
wasingiziao watu !
NI wanaogeuziwa, na mamlaka zilokuwa,
Mola awaandalia, adhabu ya kurudia,
Motoni jivu wakawa, kisha tena kurejea,
Dunia haiwapendi, kibao wageuzao !
Rushwa wanaopalilia, na fanaka kupatia,
Miiba wapalilia, ya kesho wakifikia,
Nusura kutoijua, ila ni kuraruliwa,
Dunia haiwapendi, wazoea chauchau!
Shibe wasioijua, hadi tumbo kupasuwa,
Wala hadi kuvimbiwa, na magonjwa kuingia,
Adhabu ya wangojea, ilhali hai wakiwa,
Dunia haiwapendi, walao kama nguruwe!
Ya watu yaliyokuwa, kama majibwa wakawa,
Wakawa wenye ridhaa, pasina kweli kujua,
Wezi wakawatumia, ya kwao kujijengea,
Dunia haiwapendi, waishio kama mbwa
Dhuluma waliojaa, hata kwa wenye ukiwa,
Mola awaandalia, kibaya kilichokuwa,
Muhali kuwahurumia, wao wasipohurumia,
Dunia haiwapendi, wote wanaodhulumu!
Wanyonge wanaoonea, na vya kwao kuchukua,
Kubwa ardhi ikiwa, dunia inawajua,
Kuna siku watajua, ijapo kuwakataa,
Dunia haiwapendi,
watu wanaoonea !
Dharau wanaotia, kwa sana kujisheua,
Dunia huwabugia, kisha ikawacheua,
Mzoga ukaja liwa, na mafisi enye njaa,
Dunia haiwapendi, wanaofanza dharau !
Unafiki walojaa, huwakataa dunia,
Wanapoihitajia, 'no' huwatamkia,
Njiani wakaishia, na upwa kugaagaa,
Dunia haiwapendi, wale wenye unafiki !
Wanaozinyanyapaa, imani wasozijua,
Kumbe za kweli zikawa, hofu hawajaijua,
Laiti wakijitambua, watataka kufukiwa,
Dunia haiwapendi, watibuao imani!
Haki wanaonunua, wengine kuwauzuia,
Riziki kujipatia, wengine wakazuliwa,
Hadi ndani wakatiwa, uovu kwenda fanziwa,
Dunia haiwapendi, haki wanaonunua !
Haki wanaouziwa, matumbo huwaumbua,
Huja yakafutuliwa, kama baluni yakawa,
Ilhali wanakuwa, sinema kujionea,
Dunia haiwapendi, wanaouziwa haki !
Walokithiri tamaa, kila kitu walilia,
Hata vya kuja waua,
na uchizi kuwatia,
Si wa kujitambua,
viumbe wa kuhurumiwa,
Dunia haiwapendi, walokithiri tamaa !
Hudhani wanasifiwa, na mapambo kupambiwa,
Kumbe chini watumiwa, wenye njaa kuwafaa,
Siku wakijaishiwa, hupuputika manyoya,
Dunia haiwapendi, ila inawadanganya !
Kobe akadhindwa paa, duniani kureja,
Mgonjwa ajapokuwa, pasiwe wa kumwangalia,
Na hiyo ndiyo dunia, na mambo yake ni haya,
Dunia haiwapendi, wasomjua mgonjwa !
Fakiri wasoangalia,
haiwapendi dunia,
Mali wakijichumia, mchwa huja kujilia,
Na wana waliozaa, maskini hujifia,
Dunia haiwapendi, wasojua aso nacho !
Ukweli wanaofukia, na uongo kutumia,
Hawajui walaaniwa, ilihai wanakuwa,
Na siku huja ingia, vichwa vikawashangaa,
Dunia haiwapendi, wauzikao ukweli !
Wataniao dunia, huja mwisho kutaniwa,
Na hiyo hiyo dunia,
waliokiitania,
Na wa mwisho huambiwa, kicheko kikubwa huwa,
Dunia haiwapendi, wataniao dunia !
Thursday, September 5, 2013
hivi kosa ni la nani?
Wakitamka bahali, hudhani Java natua,
Hushindwa tamka ghali, gari ukalisikia,
Hukambia kalili, kumbe kariri wambiwa,
Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?
Hukutajia fahali, ng'ombe ukamdhania,
Kumbe umulimuli, na kung'ara kwa tabia,
Kiswahili dhofu hali, wahariri waugua?
Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?
Wakitamka ya hali, ulivyo huidhania,
Kumbe joto dalili, ndo wanalofikiria,
Wasemapo ya mahari, ndipo huchanganyikiwa,
Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?
Mahali ndiyo mahari, hivi lini imekuwa,
Na kwanini mhariri, haya anayaridhia ?
Au hanayo habari, kwa yanayoripotiwa?
Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?
Lini ikawa ni shali, hali ya kuwa ni shari,
Piri haijawa pili, hilo naona dosari,
Bado kwetu ni ajali, na ajari si sanjari,
Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?
Kabuli huwa ukweli, haijawa ni kaburi,
Na ishara ni dalili, si hariri si dariri.
Na johari si johali, hilo kwa kweli athari,
Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?
Kalili sio kariri, ni kidogo kitakuwa,
Wala reri sio reli, na wala haitakuwa,
Stairi si staili, mushkeli inakuwa,
Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?
Ajira kama ajali, nasamehe wahariri,
Dampo la mwenye mali, huna ila ya hiari,
Ila wateja muhali, inataka ujibari,
Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?
huwa kimya kimya
Mlipe vyema mlipa, siri atawafichia,
Chochote weza amua, haki yenu kujakuwa,
Na ataye wasumbua, haki yenu huambiwa,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Kuna kazi
za kupewa, na kanuni kujengewa,
Kama
unashateuliwa, sheria za kutetea,
Mifuko utajaziwa, na ziada kuchukua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Oisi hufunguliwa, na funguo kufungua,
Kila kitu wazi kuwa, waweza kujichukulia,
Nani wa kuangalia, cha mtu kisichokuwa?
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Sinema nazo sanaa, kuchota wabarikiwa,
Akili wakatwambia, wenzetu wanatumia,
Sisi tusiojaliwa, twabakia kufulia,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Watunzi wazuzuliwa, waimbaji nao pia,
Bulungutu kugawiwa, kwa kazi zisizokaa,
Haziachi kufubaa, pesa weshazichukua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Wakala watuanzishia, wakawajaza jamaa,
Kufumba na kfuumbua, matajiri wanakuwa,
Kila ukiangalia, huoni tulilojaliwa,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Ukuu wanagawiwa, na vilembe kufungiwa,
Majoho nayo kupewa, na senti zanye mkia,
Kila ukifuatilia, huoni unachoambua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Tume wanazizindua, mamilioni wakapewa,
Sasa nao watumbua, wafurahi Tanzania,
Kukumbukwa radhia, nini tena watalia?
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Ila ukiangalia, uwiano unavia,
Vijijini kwenye njaa, neema kutoijua,
Laana wamekamia, ubani kujichomea,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Kiasi isipokuwa, amani huifagia,
Kiasi kikipotea, umoja hujibangua,
Kiasi isipokuwa, husuda huja kuua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
njaa aina mbili
Walio na njaa huwa, chakula wakimbilia,
Kukila tumbo kujaa, na maji wakajazia,
Wala sio kuchezea, mchanga wakakitia,
Wapo wenye nja'ya kula, na njaa ya kuharibu!
Wenye ya ajabu njaa, israfu wanatia,
Chakula hukichezea, kwani si ya kweli njaa,
Sana walikililia, ili sheri kufanzia,
Wapo wenye nja'ya kula, na njaa ya kuharibu!
Matumbo yamewajaa, wazito utadhania,
Bado wakakililia, hali kuishatkia,
Pindi wanapopatiwa, huanza kukichezea,
Wapo wenye nja'ya kula, na njaa ya kuharibu!
U D I K T E T A
Ndani ukijichimbia, ukaanza kuamua,
Kupe waliotulia, huzidi kujichimbia,
Hawana la kulijua, zaidi ya kuambiwa,
Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !
Amri huwa silaha, toka juu wakipewa,
Kugeuka si ridhaa, lazima kuitikia,
Hata likiwa ni baya, kwao zuri huambiwa,
Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !
Aidha roboti huwa, chama kimeshafyatua,
Si wa kufikiria, kujua wasilojua,
Gea ilishaingia, yote ndiyo kwitikia,
Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !
Hoja zote hufulia, na umma kunyanyapaa,
Wao wakajidhania, wajua wasiyojua,
Hadi machweo yakawa, shuka wanakimbilia,
Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !
Hutweta na kutetua, na vingama kupitia,
Ibura zikakimbia, na miujiza kupaa,
Majani mtu hutwaa, kama nguo akavaa,
Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !
Yaja tusiyoyajua, tena ya kutuumbua,
Wenzangu nawashtua, mmeacha kujitambua,
Na hakuna mkubwa udhia, kama mtu kutojijua,
Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !
Watu wanawahofia, huko mnakoelekea,
Njia mmeshapotea, kugeuka mwakataa ?
Na pori wanalijua, salama halijakuwa ?
Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !
FIKRA
Hucheka nikisikia, yasiyokuwa najua,
Vivumishi kuvizua, utadhani wanapaa,
Ila ninavyoyajua, kutua yamekwishatua,
Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!
Hadithi imebakia, na nyingi zao tamaa,
Mioyo yanunuliwa, na akili nazo pia,
Hawana la kuamua, ila la kutarajiwa,
Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!
Nani amekuambia, finyu, pana litazaa,
Na chanya haitazaliwa, na hasi kinachokuwa,
Nyimbo wanajiimbia, kweli sintoitarajia,
Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!
Wanapenda kusikiwa, japo hewa wanatoa,
Aalli kisichokuwa, zaidi kukwepa njaa,
Wengine wanaugua, kukariri wasojua,
Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!
Wamezivaa kofia, matundu zilizojaa,
Zawavujia mvua, na hoja zisizokuwa,
Watu wanawashangaa, wao wanajisifia?
Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!
Hoja wainshauflia, na wengine waogea,
Kazi ni kurejearea, utadani mbovu pleya,
Wapenda kujisikia, hata kwa kisichonukia,
Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!
Juu waweza paua, na msingi hujatia,
Watu mnawakimbia, ushirikishi mwavua,
Kisha mnajisema, yakuwa na yasokuwa?
Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!
Chini mngejichimbia, na mizizi kuitia,
Ndipo mngeyafikia, ya matokeo kujua,
Kasi ipi ingekuwa, hilo noma twaawambia,
Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!
takataka
Angalia takataka, zazidi kuimarika,
Tunu hii ya hakika, kwake yeye Mwafrika,
Hajafa haujaumbika kabla hajawa taka,
Hawajali takataka, vipi wakujali wewe !
Ndivyo alivyoumbika, kihuru au mateka ?
Au analogeka, na juu waliioshika,
Akili zikakunjika, jipya kutokufanzika?
Hawajali takataka, vipi wakujali wewe !
Makwao wanapotoka, na kwa vimada kufika,
Kila kona kwapambika, kwa wingi wa takataka,
Haya yanakubalika, wala hawana mashaka,
Hawajali takataka, vipi wakujali wewe !
Kwa wageni kwarembeka, kwa Mwafrika ni mahoka,
Nchi ukiizunguka, hili sasa lajengeka,
Hata kulikosifika, sasa kunaharibika,
Hawajali takataka, vipi wakujali wewe !
Kila kttu wakishika, sasa chageuka taka,
Ila wao wapambika, na majoho kubebeka,
Huu nchi yanyongeka, vipi tutayaepuka?
Hawajali takataka, vipi wakujali wewe !
Akili za takataka, usafi hazitotaka,
Maana kunawirika, ni lazima kuchafuka,
Ndiyo wanayoyataka, hawawezi kugeuka,
Hawajali takataka, vipi wakujali wewe !
Ahadi ilishawekwa, muda unasubirika,
Siku yao kuja fika, wavune waliyotaka,
Na si mkosa Rabuka, mamboye ni ya hakika,
Hawajali takataka, vipi wakujali wewe !
Wednesday, September 4, 2013
huwa kimya kimya...
Mlipe vyema mlipa, siri atawafichia,
Chochote weza amua, haki yenu kujakuwa,
Na ataye wasumbua, haki yenu huambiwa,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Kuna kazi
za kupewa, na kanuni kujengewa,
Kama
unashateuliwa, sheria za kutetea,
Mifuko utajaziwa, na ziada kuchukua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Oisi hufunguliwa, na funguo kufungua,
Kila kitu wazi kuwa, waweza kujichukulia,
Nani wa kuangalia, cha mtu kisichokuwa?
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Sinema nazo sanaa, kuchota wabarikiwa,
Akili wakatwambia, wenzetu wanatumia,
Sisi tusiojaliwa, twabakia kufulia,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Watunzi wazuzuliwa, waimbaji nao pia,
Bulungutu kugawiwa, kwa kazi zisizokaa,
Haziachi kufubaa, pesa weshazichukua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Wakala watuanzishia, wakawajaza jamaa,
Kufumba na kfuumbua, matajiri wanakuwa,
Kila ukiangalia, huoni tulilojaliwa,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Ukuu wanagawiwa, na vilembe kufungiwa,
Majoho nayo kupewa, na senti zanye mkia,
Kila ukifuatilia, huoni unachoambua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Tume wanazizindua, mamilioni wakapewa,
Sasa nao watumbua, wafurahi Tanzania,
Kukumbukwa radhia, nini tena watalia?
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Ila ukiangalia, uwiano unavia,
Vijijini kwenye njaa, neema kutoijua,
Laana wamekamia, ubani kujichomea,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Kiasi isipokuwa, amani huifagia,
Kiasi kikipotea, umoja hujibangua,
Kiasi isipokuwa, husuda huja kuua,
Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!
Subscribe to:
Posts (Atom)