Saturday, November 30, 2013

KUNA VICHAA WA FEDHA...


 

HABARI nimesikia, kuwa wa fedha vichaa,

Wameishajilimbikia, eti sasa wazimwaa,

Kusudi na yao nia, hakuna anayejua,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Kwa wingi zilivyojaa, kila mtu agawiwa,

Hakuna wa kuchagua, wote kwao abiria,

Lengo sijalitambua, nabakia kushangaa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Punda ingelikuwa, ngejuwa wamelemewa,

Mwenye punda achezewa, na dhihaka kufanyiwa,

Mtoni akajitia, chumvi  maji kwenda kuwa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Na wanaokusudiwa, kura wanaoshikilia,

Vyamani walimokuwa, waziwazi ni bidhaa,

Bei imeshaamuliwa, taslimu wanatoa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Karuni ninayemjua, japo wingi ulimzidia,

Bure kitu hakutoa, hadi alipofukiwa,

Hawa sijawaelewa, gia gani watumia?

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Nyumbani wazichukua, ugenini kufukia,

Kisha wanajichengua, na mikwara kujitia,

Ukiona yaelea, juwa wameazimia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Matofali wachukua, dhahabu yaliyokuwa,

Kaziye si kujengea, ila kuji9nyeshea,

Ukubwa uliokuwa, hasara kwenye dunia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Wanywa hadi kujinywea, ibilisi kakolea,

Hio waalofurahia, Mola hajafurahia,

Kicheko kilichokuwa, kilio kakitohoa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Milma waelemea, bondeni kulikouwa,

Huku juu umejaa, chini wazidi kupyway,

Na bado twatarajia,  kisiwa tutabakia ?

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Kama pombe ingekuwa, sababu ningeijua,

Wataka watu kulewa, ovyo wakajisemea,

Kisha lao wakalitwaa, pasina wao kujua,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Keki ingelikuwa, kwenye basi imekuwa,

Kisha dawa imetiwa, shabaha ningegundua,

Wanuia abiria, kwenda mbele waibia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Mimi hili sijajua, la tajiri kuwa na njaa,

Ikawa yamelvyaa, hadi chini twamzoa,

Kuna kitu sijajua, bado nakiangalia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Si wa bure ukichaa, ovyoovyo kuzigawa,

Kuna sababu na nia, ila sijaigundua,

Kofia nitaivua, kija mtu kunambia,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Semeni Watanzania, haya mnayoyajua,

Vimbgwanga vyakaribia, mengi tutashuhdia,

Watu nguo watavua, sapoti kwenda kutoa,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

 

Ni wakati wa maridhia, watu kuyafikiria,

Akili wakatumiwa, si kwa moyo kuzainiwa,

Kisha wakaja kuyajutia, siku wasioitambua,

Kuna vichaa wa fedha, msijekuwachagua !

Monday, October 14, 2013

N Y E R E R E DEI 2013


Bismillahi Jalia, mmiliki wa dunia,
Mbingu na sayari pia, tujuazo, tusojua,
Yahillahi mtambua, msafi pasipungukiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Peke wa kuabudiwa, aidha wa kutegemewa,
Mshiriki usiyekuwa, japo wakusingizia,
Daraja unayejua, waja za kuwapatia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Laiti ungelikuwa, haya ningekushtakia,
Nchini yanayoingia, na macho twayafungia,
Nchi uliowaachia, weye ungewashangaa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ibilisi katuvaa, twaiabudu dunia,
Watu miungu wakawa, na ibada kufanziwa,
Wa kutusamehea, hawezi mwingine kuwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ufahari wamejaa, nchi uliowachia,
Matumizi watumia, tajiri utadhania,
Washindwa kuvipangia, fakiri kutunasua,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Hekalu wajijengea, matembe tunakalia,
Na manyatta ndio njia, Umasaini sikia,
Ila kuna walojaliwa, vya milioni kuvaa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Nyumba wanatuvunjia, wala si kutujengea,
Mali aisli yatumiwa, ughali kutwongezea,
Nusura h atuaijua, japo tumeahidiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ibada wasiojua, migongano wanazua,
Kuchinja ulichinjiwa, na Islamu alokuwa,
Vipi wawakatalia, au visa wanavizua ?
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Udini unaingia, manabii twajaliwa,
Cheo wanajinyanyua, na njia kufaragua,
Wakuu wakawaambia,  kifalme kujiishia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Elimu twaichezea, kifaurongo ikawa,
Watasi wanakamia, wa kwao kupendelewa,
Hatarini kuigawa, nchi ulotuachia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Maji yazidi potea, na tenda zinaongea,
Masikini wafulia, walonacho kwogelea,
Shilingi yazidi kupaa, mwezini itafikia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Umeme sasa nazaa, tayari imeshakuwa,
Mashamba wajilimia, Kwa ya Mtera kumwaa,
Mengi tusiyoyajua, nani aatatuambia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Amoeba imekua, tatizo linalojizaa,
Ngomba inavyozidi kulia, viraka twaongezewa,
Nafuu inatukimbia, kilio kimebakia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Udugu wajifufua, macho tunaufumbia,
Wakubwa inapokuwa, hatuna la kuongea,
Kisirani inakuwa, wazidi kujichimbia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Vyama vimeingiliwa, na hasidi na nazaa,
Vyao wanajifanzia, wapendalo huamua,
Waviza demokrasia, ya kwao kufanikiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !
makundi

Yabanwa demokrasia, na ndondocha walokuwa,
Vyumbani waliotiwa, misumari kupigiliwa,
Kisha kwa kukosa hewa, weupe hugeukia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ukabila wa siasa, nchini umeshaingia,
Wachache wajiteua,  ya wengi wakafukia,
Anayejifaragua, uhaini atatiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ukubwa twauchukua, ila maendo yavia,
Nyuma vile twarejea,  kilichopo kupotea,
Upya tunayaanzia, hata yaliyotangulia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Ufisadi umetua, nani aje kuung'oa,
Manake una wafaa, wajuao wanajua,
Kulalama sijajua, mabomu nayahofia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Twatakiwa kunyamaa, ukweli kuufukia,
Kulaumu si sheria, hakiye yachukuliwa,
Twatakiwa vumilia, lolote tukitendewa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Maguvu sasa ni njia, wenye nayo watumia,
Fedha nayo sasa pia,  imeshapewa sheria,
Kama nayo sipokuwa,  haki inanunuliwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Madini yachimbuliwa, hata na gesi nayo pia,
Swali lisilojibiwa, hivi nani kumfaa,
Ni wengi itajakuwa, au ndugu na jamaa?
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Twahofia kutokea, kama kule Nigeria,
Na JIneikwatoria,  ambako zabanjuliwa,
Wakuu wakaogelea, hadi wa chini wafulia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Wazawa wasimuliwa, thamani yaondolewa,
Maisha juu yapaa, hali chini wadumaa,
Wataipataje furaha, inashangaa dunia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Imani zimeachiwa, mikingamo kuingia,
Wa chini juu akawa, ya wengine kuamua,
Ndio wakajisemea, ya wakuu wasokuwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Mengi waliahidiwa, dirishani yatokea,
Mlangoni yazuiwa, ngangari yanashupaa,
Musuli zikishakuwa, za akili kutanua,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Mipango twaihofia, kinyume yakaakaa,
Ya mbele yanakosewa, ya nyuma yakafatia,
Kipaumbele chavia, shamba na mjini pia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Si vyema haijawa, mikakati Tanzania,
Mifumo tunafumua, badala kujishonea,
Watu wajiamlia, jinsi wanavyosikia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Uimla twauzua, utakuja tuumbua,
Na kwenye hii dunia, tuishio kwa kupaa,
Yallahi twakulilia, baa kutuepushia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Vijiji vinadumaa, vile ulivyotuachia,
Laiti ungerejea, Mwalimu ungeshangaa,
Maktaimu vinatia, na watu washangilia ?
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Kinamama wanalia, shamba wanasahauliwa,
Wateta wawanyapaa, wa mjini wanabebwa,
Wataacha nyong'onyea, na uzee kuingia ?
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Mshairi achukiwa, kwenye  yako Tanzania,
Sasa wamnyanyapaa, kwa uongo kukataa,
Kweli akapigania, watu macho kufungua,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Maisha yetu ya jaa, uleo yamechelewa,
Wanayoyafikiria, sio yanayotakiwa,
Na wanayoyaamua, tafiti zake ukiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Arijojo imekuwa, mengi yanajiendea,
Ila inapokuwa, maandamano kung'oa,
Na machinga kusanzuliwa, na vyao  vikaharibiwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Hoi demokrasia, dripu imeekewa,
Spitali yatibiwa, unyafuzi wazidia,
Katibani kuingia, mengi sana yapunguwa,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Katiba twaililia, mbali ikatuchukua,
Tusiwe wa kudumaa, kwa uoga kutwingia,
Mola tunokusudia, yote ungeyajalia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Wachache wapigania, ya kwao kufanikiwa,
Ya wengine kutibua, kwa nguvu au ridhaa,
Hatari twajionea, ujanja ukizidia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Latifu mhimidiwa, ipokee yangu dua,
Batili kuiondoa, ya haki yakabakia,
Haramu kuicheua, halali ikasalia,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

Tamati nimefikia, mbele sintoendelea,
Miye kusahauliwa, ni haki nimeridhia,
Ila ninayowambia, haya mngeyachukua,
Zimebaki kumbukumbu, Nyerere Dei yapita !

makillla
Nyerere Dei, 2013.

UKIZIDISHA UCHOYO


Angalia historia, toka utoto wakiwa,
Shuleni tulipokuwa, dishi walilivamia,
Kingi wakajimegea, kidunchu kikabakia,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Chuoni tumeingia, sasa ninakumbukia,
Shimoni kulimokuwa, chakula tukigombea,
Mara mbili warejea, ngwini tulipokaangiwa,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Yaendelea tabia, ukubwani kuingia,
Nchi wanajimegea, wengine kutogeea,
Nafsi yawachezea, kumg'ang'ania dunia,,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Ila ninayahofia, walivyochoka raia,
Furaha yawakimbia, na hasira kuwajaa,
Kulipuka ndio njia, nalilia Tanzania,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Tuidhibiti tabia, yenye wingi wa tamaa,
Ovyo kujilimbikia, hata kwa yasiyotufaa,
Yataja tutumbukia, tukabaki tunalia,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Mmoja tungeanzia, mitaani kuingia,
Makubwa hayajakuwa, matatizo Tanzania,
Madogo yanayokuwa, tusiache kutatua,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Upofu tukijitia, twampa shoka kichaa,
Wana na wanaofatia, salama hawatakuwa,
Mbegu tutajipandia, ya hasama na adawa,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Uchoyo ukizidia, kupendwa haitakuwa,
Watu watakuchukiya, na unafiki kutia,
Ilhali wazomewa, udhani washangiliwa,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Rafiki watakimbia, mwenyewe ukabakia,
Ikawa wao umbeya,  tadi kuiongelea,
Mengi wakakupakia, weye usiyechukua,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

Kama kuna majaliwa,  hili nisingejaliwa,
Riziki ningeachia, kila mtu kujaliwa,
Yangu nikawagawia, tunu kwenda zawadiwa,
Ukishazidi uchoyo, wengi watakuchukia !

MNAPOKUWA SHULENI, VYUONI


WENGI nimeuliziwa, waliokuwa vipenzi,
Rafiki wa kutulia, tusofendana ajizi,
Habari nikaambiwa, dongo halikuwaenzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Najua wa chekekechea, wamerdi kwa Mwenyezi,
Jichoni sikuwatia, nilipoianza kazi,
Taarifa sikupewa, si za jana si za juzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Msingi na huko pia, tumepishana kwa ngazi,
Peter alishapotea, na Ummy naye ni wa juzi,
Sasa ninasimuliwa, na hata wangu wanafunzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Sekondari tulijaa, pasina ya kizuizi,
Milango tulotumia, ya shule ile Mawenzi,
Wameondoka mamia, na kujua si wajuzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Chuo kikuu najua, kwa hesabu siiwezi,
Waliojiondokea, kina kazi kikotezi,
Sammy analialia, ya Freddy, Mboya vipenzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Rafiki aliyekuwa, na pili ni mkufunzi,
Dunia yatuhadaa, ila yake hatuwezi,
Lati tungelijua, mambo yepi ya kuenzi ?
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Ukaribu tusokuwa, tumuachia Mwenyezi,
Siri zake azijua, mapenzi hatuyawezi,
Huenda kwa kuandikiwa, zikabaki simulizi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

Mola namwangukia, aliye wetu mlinzi,
Hao walotangulia, kuwapa njema hifadhi,
Viwango anavijua, hilo kwangu mwanafunzi,
Mnapokuwa shuleni, hebu ishini kwa wema:
mwaweza msionane, tena baada ya hapo!

KIKULACHO


Kwanza 'ngejiangalia, vizuri kujichungua,
Wa nje kutosingizia, masahibu wakutia,
Pengine hujatambua, ndaniyo aweka kuwa,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

Labda keshakuingia,  kwa mithili yake chawa,
Kwenye nywele kaingia, pango keshalilipia,
Anasa ajifanzia, rusha roho azizua,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

Stihizai hutia, wengine ukadhania,
Shere akautezea, jirani kusingizia,
Ila yatakustua, kung'atwa ukigundua,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

Damu anajinyonyea, kuwanda akazidia,
Wewe unapalilia, yeye anajivunia,
Au ng'ombe umekuwa, kaziye kukukamua,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

Yako unaharibikiwa, yake yanasimuliwa,
Kichinichini ikawa, kitu hautosikia,
Husema amepatia, mahala kashikilia,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

Utamu kashikilia, hawezi kupungukiwa,
Ila niavyotambua, kuna siku yaingia,
Nywele ukijakunyoa, atakosa pa kukaa,
Kikulacho uko nacho, unacho nguoni mwako!

USIMSOGELEE


HATA dadayo akiwa,  simsogelee mnafiki,
Stara hajajaliwa, rohoye ni mamluki,
Ndarahima adhania, Mola wake wadhihaki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Kiumbe ninakataa, hajawa naye rafiki,
Kazi yake kfukua, udhaifu kuulaki,
Kisha akakufanzia, ya kuja kutaharuki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Kifo atakuombea,  ami wa kindakindaki,
Huku anakutekea, nawe wampa malaki,
Au unalomfaa, pasina nayo mikki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Dhiki atakuombea, njiani ije kulaki,
Kadri unavyofulia, furaha haimtoki,
Yake yakiogelea, kuzama  yako huafiki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Usoni hukuchekea, hali moyoni ni chuki,
Hutaka kumalizia, ya uimbeya kuafiki,
Kisasi akakitia, msingi kisichonaki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Pagani ninakwambia, bora yake mnafiki,
Kisomo hajakijua, nafsi ingeafiki,
Dua ukimuombea, hudumu kwa urafiki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

Dini hukurubia, mwisho akaiafiki,
Ashaduu akatia, akapendezwa Mulki,
Ila ninalikataa, hayawezi mnafiki,
'Simsogelee mnafiki, mwisho atakuumbua !

P U L I Z O



Upepo ukilitia, kwa kiasi hufumuka,
Hupanuka likajaa, na viungo kuitika,
Usipolishikilia, juu laweza chomoka,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Arijojo hukimbia, kwenda lisikokutaka,
Wahaka ukakujaa, hali unaweweseka,
Huwezi likimbilia, si kiumbe wa kupaa,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Jua litaliachia, hali mahala kufika,
Hari ikishazidia, kawaida kufumuka,
Na viumbe wanajua, jambo hili la hakika,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Hawataki kusikia, ukawatia mashaka,
Ya kwao yakasinyaa, waendako kutofika,
Wanaipenda hadaa, kwa kuzua na kuzuka,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Juu wanaidhania, furaha imefichika,
Nini utawaambia, wasiache kuteseka,
Ukichaa inakuwa, eti ni shani kuzuka,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Mbio wanazitimua, haraka wapate fika,
Ushindani kuutia, hata pasipotakika,
Malaika wavizia, nani wataoanguka,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Kamba wameshazitia, na viuzi kuviweka,
Kuruka asiyejua, huenda akateguka,
Pumzi wanaoishiwa, hao mabli kutofika,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Hii halina ngekewa, kadara yahitajika,
Kila asiyeijua, haiwezi nunulika,
Bure unajisumbua, akiba ungeiweka,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Kalamu naiachia, hapa ninapumizka,
Siwezi ya kukimbia, kutembea natosheka,
Umri nikiongezewa, ukweli kudhihirika,
Pulizo likishajaa, mwisho wake kupasuka !

Monday, September 23, 2013

KATIBA BILA UWAZI



KATIBA tumeamua, tunaitaka mpya,
Na hili kufanikiwa, ni lazima kuchangia,
Kila unalolijua, lawza kukusaidia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Sera kutochakachua, kwa mifumo ya udhia,
Ikawa zinazuia, watu wetu kuchangia,
Nafasi wakatukua, kitu wasiochangia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Usije pembeni kaa, wengine ukaachia,
Yako hawatayajua, moyoni yaliyokuwa,
Mwenyewe ukitokea, hilo litazungumziwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Ya zamani kupitia, ni uzuri itakuwa,
Ukapata kuijua, kasoro zilizojaa,
Nawe ukaikosoa, na kuujenga ulua,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Yafaa kufikiria, ya leo na ya kuzua,
Mbele yatayotokea, njia kuyaandalia,
Iwe si kushtukiwa, mambo yakituchachia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Inafaa kuamua, ya wakuu wa mikoa,
Wawe ni wa kuteua, au wa kuchaguliwa,
Naona tunaumia, kwa hawa wa kuteua,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Ukubwa wauchukua, bila ya kupigania,
Wa juu wawatumia, ya kwao kufanikiwa,
Nasi katika mkoa, kitu hatutaambulia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Kadhalika na wilaya, kama nao wanafaa,
Au wengine wakawa, kwa bora iliyo njia,
Waweze kutumikia, bila uchama kutia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Na rais kuchagua, mikakati kuwazia,
Ni mikoa kuchagua, wasafi watu kadhaa,
Kisha wakaingia, chamani kuchaguliwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Ni ipi asilimia, ipate kukubaliwa,
Kidogo sana ikiwa, ridhaa inapungua,
Kubwa ikizingatiwa, bora zaidi yafaa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Kuungana vyatakiwa, vyama hapa Tanzania,
Gharama zikapungua, lazima isiyokuwa,
Vitatu vikibakia, nafuu tutaambulia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Na nchi kuyaamua, mbili au tatu zikawa,
Watu uhuru kuvua, ya kwao wakaangalia,
Isiwe kutawaliwa, na ndani waliokuwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Dola nayo kuamua, nguvu zinapoishia,
Hawa wanaotumiwa, pabaya watuchukua,
Juu wakiwa raia, nidhamuwataijua,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Mishahara twatakiwa, pia kwenda kuamua,
Vipi itakavyokuwa, utenzi kuzingatia,
Sio wanaopepewa, masultani wakawa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Vijana tunatakiwa, uhuru kupigania,
Na sio kujatumiwa, na wazee walokuwa,
Kisha wakatuhadaa, kama panzi tulokuwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Kisha wakatuhadaa, kama panzi tulokuwa,
Nao kunguru wakawa, riziki wajipatia,
Nasi bila kujijua, tuzidi kuangamia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Wazee mnatakiwa, kutumiwa kukataa,
Leo kuzungumzia, myapate manufaa,
Siasa kutowagawa, kwa vyama kuvitumia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Wazee mkapigania, yalo yenu manufaa,
Isiwe mnatumiwa, na waliovimbiwa,
Hili mkishguhulikia, yenu yatazingatiwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Watoto mnatakiwa, haki zenu kuzijua,
Na kisha kushikilia, katibani kuingia,
Pasaiwe lisilokuwa, kwa vyovyote itavyokuwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Umoja mnatakiwa, wanawake kuulea,
Msije mkatumiwa, na wahuni walokuwa,
Nao wakishawagawa, yenu kutoangalia,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

Baraka nawaombea, ndugu zangu Watanzania,
Yenu yakifanikiwa, na wangu watafanikiwa,
Nayo yakliharibiwa, nao huharibikiwa,
Uwazi unatakiwa, katiba kuichangia!

AINA ZA UGAIDI



Mambo mengi ugaidi, jambo moja halijawa,
Nabonyeza kwako hodi,Upate kuyatambua,
Si moja kufaidi, na mengi kutokujua,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Ufisadi ugaidi, japo hatujalitambua,
Nao mkubwa mradi, duniani waenea,
Wengi wauona sudi, neema zinavyojaa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Rabsha inajinadi, dhana kila kitu kuwa,
Kwalo sijaona idi, kufaidi sijajua,
Si mmoja ugaidi, asa umeshatambua,
Naupandisha mdadi, kuushusha natakiwa,

Wa maneno ugaidi, sasa unachipukia,
Wasema kwa ukaidi, na vitisho kuvitoa,
Hii haikuwa jadi, yatuzushia balaa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Leo wanaofaidi, hawatakia kuachia,
Wafanza zote juhudi, wengi chini kudidimia,
Ili wabaki jadidi, juu wanashikilia,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Umeanza wa fisadi, mlo wote kupakua,
Hata dini kuritadi, lishe sababu ikiwa,
Akafanza ukaidi, kuipindua dunia,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Aidha wa ukaidi, na jeuri kuzitia,
Akachapwa mijeledi, mnyonge aliyekuwa,
Kisa ataka idadi, na vyanzo kuving'amua,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Kuna ule wa mdadi, na hasira kuvimbiwa,
Usimhofu Abadi, na vitisho kuvitoa,
Watu ukawafasidi, haki zao kuzitwaa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Uongo pia mradi, nao ni ugaidi pia,
Kweli zisiwe ahadi, bali uongo kujaa,
Asojua hafaidi, hadi akitindikiwa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Upo wa kutaradadi, utukufu kuombewa,
Au kwa zako juhudi, ukataka juu paa,
Asili ukakaidi, ikakutema dunia,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Kuna ule wa kijadi, na silaha kutumia,
Kwa bidii na juhudi, nguvu ukazitumia,
Cha wengi ukikinadi, na pengine kukitwaa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Kuna ule wa magadi, pa chumvi ukaitia,
Na wa kutumia radi, watu ukawatumia,
Ajuaye ni Wadudi, vipi inavyotokea,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Upo ule wa hasidi, wengine kuwachukia,
Na ukiwapa ahadi, iwe isiyotimia,
Isikughasi fuadi, kawaida kwako kuwa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Kuna ule wa baridi, mtu kimya kukaa,
Hana kadi, hana kodi, yake yanajiendea,
Amtanguliza Hadi, hata pasipotakiwa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Na wasio maabuddi, Ibilisi huwavaa,
Yake waasiyakaidi, yeye akawatumia,
Haya yake ya mihadi, hadi mwisho kwenda kuwa,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Baraza nataradadi, tawakali tangulia,
Usiipate nakidi, na hasara kuingia,
Si mmoja ugaidi, sasa umeshang'amua,
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

Mwenye nguvu na mgodi, ndo' wa kumtambua?
Mwenye hisa na miradi, hatojanisingizia ?
Ayalilia Masudi, kuchora atarudia ?
Aina za ugaidi, hapa ninazianika!

KATIBA YA WATANZANIA


Mola tunakulilia, batili kuikataa,
Halali kutupatia, kwa tunayoyatarajia,
Mama wa zetu sheria, mbele kumtangulia,
Katiba ya Tanzania, si ya chama kimoja !

Wamezuka waso haya, wajinga watudhania,
Ya kwao wapalilia, mchakato kupitia,
Ilhali tunajua, si halali yalokuwa,
Katiba ya Tanzania, si ya mtu mmoja !

Uchache wautumia, wingi wetu kufukia,
Sauti waikataa, yao wataka sikia,
Kisha waje kuamua, kizazi yasiyokifaa,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !

Nchi yetu twaijua, na makundi yalokuwa,
Akili ukitumia, wawakilishi twajua,
Wiano kuangaliwa, kwa wenyewe kuchagua,
Katiba ya Tanzania, si ya chama kimoja !

Mfumo tulishaamua, wa wingi sio umoya,
Sasa yanayotokea, yarejesha historia,
Chama kinasimamia, kisichokistahilia,
Katiba ya Tanzania, si ya mtu mmoja !

Uwakilishi ni njia, watu wote kufikia,
Sio sisi kutugawa, kwa vijisenti kutoa,
Kisha wakateuliwa, ndiyo ndiyo kwitikia,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !

Makundi tunayajua, na idadi nayo pia,
Hata waliokikataa, zamani kuhesabiwa,
Kipofu anawajua, barazani watakiwa,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !

Wawapuuza raia, kama vile ni bidhaa,
Wengine wananunua, na mfukoni kutia,
Mwalimu angeshangaa, ukubwa wa kututia,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !

Raia wanatambua, nani wamtarajia,
Barazani kwenda kaa, ili yao kutetewa,
Sasa wanachofanyiwa, zezeta waandaliwa,
Katiba ya Tanzania, si ya chama kimoja !

Wajuu waliokuwa, hawataki kusikia,
Maoni yanatolewa, dharau wanaitia,
Nchi utafikiria, haki yao imekuwa!
Katiba ya Tanzania, si ya mtu mmoja !

Kila wanaloambiwa, upuuzi wajionea,
Kama kawa kwendelea, pasi soni walla haya,
Ilhali tunajua, pabaya twaelekea,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !

NCHI iliahidiwa, katiba bora kupewa,
Idumu miaka mia, kizazi kufurahia,
Leo tunashuhudia, ya mwaka mmoja wazua?
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !

NCHI iliahidiwa, katiba bora kupewa,
Idumu miaka mia, kizazi kufurahia,
Leo tunashuhudia, ya mwaka mmoja wazua?
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !

Rabi twakuhimidia, tuepushe na balaa,
Hekima kuwapatia, wakuu waliokuwa,
Zuri wakaliamua, kuokoa Tanzania,
Katiba ya Tanzania, ya Watanzania wote !

Rabana mwenye kujua, Bashiri uliyekuwa,
Upofu 'ngeliondoa, na busara kujalia,
Wakasimama raia, haki yao kupatiwa,

HIVI CHAMA KINA DIRA ?


KICHWA hutokijua, wala wapi ni mkia,
Kule unakodhania, uamuzi hutolewa,
Wao nao wangojea, wa chini kuja amua ?
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Pembeni tuliokaa, dhaifu mabaharia,
Wakati umeshaingia, chama chetu kukitwaa,
Dira tukakipatia, baharini kuelea,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Mashaka tunayazua, kwa uongozi kufifia,
Wengi tuloachia, kazi yao kusifia,
Kombakomba walokuwa, eti vyeo wangojea,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Uoga umetujaa, chinichini twasemea,
Ukweli tunaujua, na batili nayo pia,
Vipi tunaendelea, kama vile hii kawa?
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Mansuri kajitolea, ukweli kuutumbua,
Wazuka wa kuzomea, kumbe wanajishushua,
Ukweli ndio shujaa, daima tama adawa,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Watu tunawakimbia, wenyewe twajitumikia,
Pasi aibu na haya, kazi yetu imekuwa,
Huko tunakoeleka, walahi nakuhofia,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Kimya ninakikataa, tangazo hili kutoa,
Wenye chama watakiwa, ukweli kuutambua,
Tumeichagua njia, Mwalimu aliyokataa,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Kuongoza twatambua, ndilo tunalotakiwa,
Sasa tunaamriwa, kilingeni twatolewa,
Watu wanajionea, haya yote washangaa,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Tulishaongoza njia, si tu hapa Tanzania,
Afrika nako pia, pamwe nayo dunia,
Leo tumekuwa mkia, nyuma nyuma kufatia,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Falsafa imevia, wala hatunayo taa,
Gizani tunatembea, mambo kubahatishia,
Ya ndani wanaojua,  pakupiga wapajua,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Wafofaa twaachia, kazi zetu kuzikwea,
Ovyo wanajifanzia, kepesti na kukopia,
Majilisi kiingia, kichekesho kinakuwa,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Hawasomi wakajua,  na makosa kuyatoa,
Ndio wanaitikia, pasina kufikiria,
Uwakilishi wavia, na watu hili wajua,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!

Changamoto twaitoa, kwa upya kuzaliwa,
Wenye uchungu na nia,hivi sasa kujitoa,
Mkono nawaachia, sikufunga nafungua,
Chama kinakosa dira, tukiokoe baharia!


Katiba ikija mbovu



Vijana waangalia, tunachowaamulia,
Mushkeli kikijaa, yasije yakawafaa,
Hatua watachukua, adhabu kali kutoa,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!

Tuache jifikiria, kizazi kuangalia,
Ya leo tunayajua, kesho yasije zuia,
Maovu tuakayazua, kwenye pepo Tanzania,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!

Viongozi wayajua, ndo kisa kuyakemea,
Isitumike hadaa,  baharini twaelea,
Pepo zitatuumbua, kichangani kuelea,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!

Macho tungeyafungua, tusome tuolosusia,
Mistari kujijua, kwa kujitafakaria,
Upofu tukijitia, wenyewe twaja kulia,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!

Tusije kuvumilia, mbovu tukajapatiwa,
Mishipa tutaizua, na pumzi kulipua,
Nchi ikawa balaa, pasiwepo pa kukaa,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!

Kwa hiari nayatoa, katikati nilokuwa,
Upande sijaegemea, mkweli wa Tanzania,
Haki nimepgiania,  uhaini kuzuliwa,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!

Maradhi nayatambua, kwa waliokisinzia,
Haya tukiyaachia, pabaya twaelekea,
Sangari kuing'ofoa, hiyo ni ya shamba dawa,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!

Jalali twakulilia, uongozi kuzindua,
Wasije tuamulia, yawe ukimwi mpya,
Nchi itateketea, hali twaiangalia,
Katiba ikija mbovu, chama kuwa dhaifu!


Saturday, September 21, 2013

K A T I B A I J U U Y A W O T E



Juu atayejitia, asimame kutwambia,
Nani amemchagua, juu ya wengine kuwa,
Kigezo kilichotumiwa, na bei aliyotoa,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !

Wapi imeruhusiwa, mstari kudadavua,
Nasi hatutambishia, njia tutamuachia,
Ila tunavyotambua, kwa juu hapatakuwa,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !

Juu anayejitia, ataka kuichezea,
Usanii kujitia, asiyejua sanaa,
Ujuzi hakujaliwa, mabavu ayatumia,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !

Usanifu kujitia, na uashi anajua,
Yule tunayetambua, hayo kamwe hakusomea,
Ni msiba twangojea, hali tunachekelea,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !

Jengo akitujengea, laja kutuangukia,
Na wengine kufukiwa, kuzikwa hai wakiwa,
Wajifanzao wajua, kisha mbali wakakaa,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !

Sisi wote ni raia, wakuu na wasiokuwa,
Hakuna alozidia, katiba yatuambia,
Vipi ikaja ikawa, mmoja juu akwaa?
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !

Ubinafsi twahofia, kwa madhara na nazaa,
Ndiio maana usia, huu wa historia,
Wote chini twarejea, nini tena kuambiwa?
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !

Chama kinapojitia, nchi kinaipindua,
Hila wakizitumia, ufidadi wajitia,
Batili kuitumia, halali wakaachia,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !

Yao wajiandalia, na palizi kuitia,
Kwenye shamba la kuzua, kabaila kakodiwa,
Kondeni bomu zajaa, zisije tulipukia,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !

Aihadaa Tanania, wakati haijasinzia,
Kono fukoni katia, halali avichomoa,
Vingine vyamwagikia, chini vikatapakaa,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !

Yajichokea dunia, kuizoea mizaha,
Guu likijimbia, na kuutunga usahaa,
Siku itapowadia, uchungu tutasikia,
Katiba kitu kikubwa, wadogo sote raia !




Friday, September 6, 2013

D U N I A H A I W A P E N D I


Haiwapendi dunia, japo yawavumilia,

Uungu wanaojitia, na kiburi kuwajaa,

Huonekana mzaha, Mola wanamfanzia,

Haiwapendi dunia, uungu wajitiao!

 

Ovu wanaotishia, hata kwa waoto pia,

Watu wanawachukia, na kuwaona kinyaa,

Huwa mkubwa udhia, japo ukavumiliwa,

Haiwapendi dunia, waishio kwa vitisho!

 

Wafutuao vifua, na maguvu kutumia,

Ilhali wakiishiwa. upepo waja pungua,

Kinyamkera ni jaa, kila kitu huchukua,

Dunia haiwapendi, watunishao vifua !

 

Wajanja kupotezea, ni nadra kuridhiwa,

Kamba wanaachiiwa, za kwenda jitundikia,

Nao bila kujijua, vichwa wanavipanua,

Dunia haiwapendi, walokubuhu hadaa !

 

La mtu wasosikia, songombingo kujendea,

Hekima wakajitia, kwa busara kuitoa,

Rahisi kuvumiliwa, na sio kukubaliwa,

Dunia haiwapendi, ushauri wasotaka!

 

Wanaotaka kupaa, kwenye mwezi kutembea,

Hali ni hii dunia, wanayoikanyagia,

Huru watajisikia, ila deni walitwaa,

Dunia haiwapendi, wale wanaojiona !

 

Wale wanaounuia, kila mtu kuwajua,

Hata pasipowafaa, wakawa ni wa kuingia,

Nafsi hujichubua, dhihaka ikawajaa,

Dunia haiwapendi, wajifanzao sinema !

 

Wanaojilimbikizia, hadi wana kuvimbiwa,

Kisha wakajiachia, mitegoni kuingia,

Salama huwaachia, mbali nao ikakaa,

Dunia haiwapendi, waozao kwa fasidi !

 

Fahari wanaojitia, na mbwembwe kushangilia,

Dunia kuwazuzua, kisha ikawachezea,

Viumbe wasiojijua, si aghali kupotea,

Dunia haiwapendi, wale wanaojidai!

 

Ukuu wanaolilia, mafuu wengine kuwa,

Ngazi wakazitumia, kisha teke kuzitia,

Huku moyo wakomaa, uovu kuendelea,

Dunia haiwapendi, wale wanaojikweza !

 

Kelele waliojaa, hata kwa wasoyajua,

Katikati kwingilia, madebe wakapasua,

Huonekana nazaa, kicheko cha kuchefua,

Dunia haiwapendi, viumbe wenye kelele!

 

Ulimi wasiolea, ovyovyo kutumia,

Maneno wakayatoa, ya kuwakwaza raia,

Huonekana balaa, si wa kutegemewa,

Dunia haiwapendi, ulimi wasiochunga!

 

Uongo wanaoujua, wakashindwa ukataa,

Huwa ni waongo pia, wanafaa kuhofiwa,

Shimoni huja watia, machoni wawaangalia,

Dunia haiwapendi, waabuduo uongo!

 

Wageuzwao bidhaa, watu wakawanunua,

Kisha wakawatumia, kwa mengi yasiyokufaa,

Hawa ukiwaachia, hatiani unajitia,

Dunia haiwapendi, wageuzwao bidhaa !

 

Wasiokuwa na haya, maovu kutohofia,

Waziwazi wakavua, ilhali watembea,

Ni watu wa kuoghofya, ukiweza mbali kaa,

Dunia haiwapendi, haya wanaoikosa !

 

Kisasi waliojaa, na huruma kusinyaa,

Mola hatowaangalia, kiyama kikiingia,

Mgongo hugeuziwa, na motoni kwenda kaa,

Dunia haiwapendi, kisasi wanaojaa!

 

Mema hutarajia, uoza wakisifiwa,

Vichwa kukomalia, na mifuko kulegea,

Ila siku ikiingia, tundu hawatoshuhudia,

Dunia haiwapendi, wanaokosa huruma !

 

Watu wanaopakazia, makosa wakawazulia,

Kesi wakabambikiwa, na waovu kuwavaa,

Adhabu wakaipewa, chanzo wasichokijua,

Dunia haiwapendi,  wasingiziao watu !

 

NI wanaogeuziwa, na mamlaka zilokuwa,

Mola awaandalia, adhabu ya kurudia,

Motoni jivu wakawa, kisha tena kurejea,

Dunia haiwapendi, kibao wageuzao !

 

Rushwa wanaopalilia, na fanaka kupatia,

Miiba wapalilia, ya kesho wakifikia,

Nusura kutoijua, ila ni kuraruliwa,

Dunia haiwapendi, wazoea chauchau!

 

Shibe wasioijua, hadi tumbo kupasuwa,

Wala hadi kuvimbiwa, na magonjwa kuingia,

Adhabu ya wangojea, ilhali hai wakiwa,

Dunia haiwapendi, walao kama nguruwe!

 

Ya watu yaliyokuwa, kama majibwa wakawa,

Wakawa wenye ridhaa, pasina kweli kujua,

Wezi wakawatumia, ya kwao kujijengea,

Dunia haiwapendi, waishio kama mbwa

 

Dhuluma waliojaa, hata kwa wenye ukiwa,

Mola awaandalia, kibaya kilichokuwa,

Muhali kuwahurumia, wao wasipohurumia,

Dunia haiwapendi, wote wanaodhulumu!

 

Wanyonge wanaoonea, na vya kwao kuchukua,

Kubwa ardhi ikiwa, dunia inawajua,

Kuna siku watajua, ijapo kuwakataa,

Dunia haiwapendi,  watu wanaoonea !

 

Dharau wanaotia, kwa sana kujisheua,

Dunia huwabugia, kisha ikawacheua,

Mzoga ukaja liwa, na mafisi enye njaa,

Dunia haiwapendi, wanaofanza dharau !

 

Unafiki walojaa, huwakataa dunia,

Wanapoihitajia, 'no' huwatamkia,

Njiani wakaishia, na upwa kugaagaa,

Dunia haiwapendi, wale wenye unafiki !

 

Wanaozinyanyapaa, imani wasozijua,

Kumbe za kweli zikawa, hofu hawajaijua,

Laiti wakijitambua, watataka kufukiwa,

Dunia haiwapendi, watibuao imani!

 

Haki wanaonunua, wengine kuwauzuia,

Riziki kujipatia, wengine wakazuliwa,

Hadi ndani wakatiwa, uovu kwenda fanziwa,

Dunia haiwapendi, haki wanaonunua !

 

Haki wanaouziwa, matumbo huwaumbua,

Huja yakafutuliwa, kama baluni yakawa,

Ilhali wanakuwa, sinema kujionea,

Dunia haiwapendi, wanaouziwa haki !

 

Walokithiri tamaa, kila kitu walilia,

Hata vya  kuja waua, na uchizi kuwatia,

Si wa  kujitambua, viumbe wa kuhurumiwa,

Dunia haiwapendi, walokithiri tamaa !

 

Hudhani wanasifiwa, na mapambo kupambiwa,

Kumbe chini watumiwa, wenye njaa kuwafaa,

Siku wakijaishiwa, hupuputika manyoya,

Dunia haiwapendi, ila inawadanganya !

 

Kobe akadhindwa paa, duniani kureja,

Mgonjwa ajapokuwa, pasiwe wa kumwangalia,

Na hiyo ndiyo dunia, na mambo yake ni haya,

Dunia haiwapendi, wasomjua mgonjwa !

 

Fakiri wasoangalia,  haiwapendi dunia,

Mali wakijichumia, mchwa huja kujilia,

Na wana waliozaa, maskini hujifia,

Dunia haiwapendi, wasojua aso nacho !

 

Ukweli wanaofukia, na uongo kutumia,

Hawajui walaaniwa, ilihai wanakuwa,

Na siku huja ingia, vichwa vikawashangaa,

Dunia haiwapendi, wauzikao ukweli !

 

Wataniao dunia, huja mwisho kutaniwa,

Na hiyo  hiyo dunia, waliokiitania,

Na wa mwisho huambiwa, kicheko kikubwa huwa,

Dunia haiwapendi, wataniao dunia !

Thursday, September 5, 2013

hivi kosa ni la nani?



Wakitamka bahali, hudhani Java natua,

Hushindwa tamka ghali, gari ukalisikia,

Hukambia kalili, kumbe kariri wambiwa,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Hukutajia fahali, ng'ombe ukamdhania,

Kumbe umulimuli, na kung'ara kwa tabia,

Kiswahili dhofu hali,  wahariri waugua?

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Wakitamka ya hali, ulivyo huidhania,

Kumbe joto dalili, ndo wanalofikiria,

Wasemapo ya mahari, ndipo huchanganyikiwa,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Mahali ndiyo mahari, hivi lini imekuwa,

Na kwanini mhariri, haya anayaridhia ?

Au hanayo habari, kwa yanayoripotiwa?

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Lini ikawa ni shali, hali ya kuwa ni shari,

Piri haijawa pili, hilo naona dosari,

Bado kwetu ni ajali, na ajari si sanjari,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Kabuli huwa ukweli, haijawa ni kaburi,

Na ishara ni dalili, si hariri si dariri.

Na johari si johali, hilo kwa kweli athari,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Kalili sio kariri, ni kidogo kitakuwa,

Wala reri sio reli, na wala haitakuwa,

Stairi si staili, mushkeli inakuwa,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

Ajira kama ajali, nasamehe wahariri,

Dampo la mwenye mali, huna ila ya hiari,

Ila wateja muhali, inataka ujibari,

Ni kosa la mwenye mali, au lake mhariri?

 

 

huwa kimya kimya


Mlipe vyema mlipa, siri atawafichia,

Chochote weza amua, haki yenu kujakuwa,

Na ataye wasumbua, haki yenu  huambiwa,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Kuna kazi  za kupewa, na kanuni kujengewa,

Kama  unashateuliwa, sheria za kutetea,

Mifuko utajaziwa, na ziada kuchukua,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Oisi hufunguliwa, na funguo kufungua,

Kila kitu wazi kuwa, waweza kujichukulia,

Nani wa kuangalia, cha mtu kisichokuwa?

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Sinema nazo sanaa, kuchota wabarikiwa,

Akili wakatwambia, wenzetu wanatumia,

Sisi tusiojaliwa, twabakia kufulia,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Watunzi wazuzuliwa, waimbaji nao pia,

Bulungutu kugawiwa, kwa kazi zisizokaa,

Haziachi kufubaa, pesa weshazichukua,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Wakala watuanzishia, wakawajaza jamaa,

Kufumba na kfuumbua, matajiri wanakuwa,

Kila ukiangalia, huoni tulilojaliwa,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Ukuu wanagawiwa, na vilembe kufungiwa,

Majoho nayo kupewa, na senti zanye mkia,

Kila ukifuatilia, huoni unachoambua,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Tume wanazizindua, mamilioni wakapewa,

Sasa nao watumbua, wafurahi Tanzania,

Kukumbukwa radhia, nini tena watalia?

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Ila ukiangalia, uwiano unavia,

Vijijini kwenye njaa, neema kutoijua,

Laana wamekamia, ubani kujichomea,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

 

Kiasi isipokuwa, amani huifagia,

Kiasi kikipotea, umoja hujibangua,

Kiasi isipokuwa, husuda huja kuua,

Kuna malipo kufuru, huwa kimya kimya!

njaa aina mbili



Walio na njaa huwa, chakula wakimbilia,

Kukila tumbo kujaa, na maji wakajazia,

Wala sio kuchezea, mchanga wakakitia,

Wapo wenye nja'ya kula, na njaa ya kuharibu!

 

Wenye ya ajabu njaa, israfu wanatia,

Chakula hukichezea, kwani si ya kweli njaa,

Sana walikililia, ili sheri kufanzia,

Wapo wenye nja'ya kula, na njaa ya kuharibu!

 

 

Matumbo yamewajaa, wazito utadhania,

Bado wakakililia, hali kuishatkia,

Pindi wanapopatiwa, huanza kukichezea,

Wapo wenye nja'ya kula, na njaa ya kuharibu!

 

 

U D I K T E T A



Ndani ukijichimbia, ukaanza kuamua,

Kupe waliotulia, huzidi kujichimbia,

Hawana la kulijua, zaidi ya kuambiwa,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Amri huwa silaha, toka  juu wakipewa,

Kugeuka si ridhaa, lazima kuitikia,

Hata likiwa ni baya, kwao zuri huambiwa,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Aidha roboti huwa, chama kimeshafyatua,

Si wa kufikiria, kujua wasilojua,

Gea ilishaingia, yote ndiyo kwitikia,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Hoja zote hufulia, na umma kunyanyapaa,

Wao wakajidhania, wajua wasiyojua,

Hadi machweo yakawa, shuka wanakimbilia,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Hutweta na kutetua, na vingama kupitia,

Ibura zikakimbia, na miujiza kupaa,

Majani mtu hutwaa, kama nguo akavaa,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Yaja tusiyoyajua, tena ya kutuumbua,

Wenzangu nawashtua, mmeacha kujitambua,

Na hakuna mkubwa udhia, kama mtu kutojijua,

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

Watu wanawahofia, huko mnakoelekea,

Njia mmeshapotea, kugeuka mwakataa ?

Na pori wanalijua, salama halijakuwa ?

Udikteta ukiiva, watu hulishwa vibichi !

 

FIKRA


 

Hucheka nikisikia,  yasiyokuwa najua,

Vivumishi kuvizua, utadhani wanapaa,

Ila ninavyoyajua, kutua yamekwishatua,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Hadithi imebakia, na nyingi zao tamaa,

Mioyo yanunuliwa, na akili nazo pia,

Hawana la kuamua, ila la  kutarajiwa,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Nani amekuambia, finyu, pana litazaa,

Na chanya haitazaliwa,  na hasi kinachokuwa,

Nyimbo wanajiimbia, kweli sintoitarajia,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Wanapenda kusikiwa, japo hewa wanatoa,

Aalli kisichokuwa, zaidi kukwepa njaa,

Wengine wanaugua, kukariri wasojua,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Wamezivaa kofia, matundu zilizojaa,

Zawavujia mvua, na hoja zisizokuwa,

Watu wanawashangaa, wao wanajisifia?

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Hoja wainshauflia, na wengine waogea,

Kazi ni kurejearea, utadani mbovu pleya,

Wapenda kujisikia, hata kwa kisichonukia,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Juu waweza paua, na msingi hujatia,

Watu mnawakimbia, ushirikishi mwavua,

Kisha mnajisema, yakuwa na yasokuwa?

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

Chini mngejichimbia, na mizizi kuitia,

Ndipo mngeyafikia, ya matokeo kujua,

Kasi ipi ingekuwa, hilo noma twaawambia,

Fikra ndogo muhali, kuja kuzaa makubwa!

 

 

 

takataka


Angalia takataka, zazidi kuimarika,
Tunu hii ya hakika, kwake yeye Mwafrika,
Hajafa haujaumbika kabla hajawa taka,
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Ndivyo alivyoumbika, kihuru au mateka ?
Au analogeka, na juu waliioshika,
Akili zikakunjika, jipya kutokufanzika?
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Makwao wanapotoka, na kwa vimada kufika,
Kila kona kwapambika, kwa wingi wa takataka,
Haya yanakubalika, wala hawana mashaka,
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Kwa wageni kwarembeka, kwa Mwafrika ni mahoka,
Nchi ukiizunguka, hili sasa lajengeka,
Hata kulikosifika, sasa kunaharibika,
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Kila kttu wakishika, sasa chageuka taka,
Ila wao wapambika, na majoho kubebeka,
Huu nchi yanyongeka, vipi tutayaepuka?
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Akili za takataka, usafi hazitotaka,
Maana kunawirika, ni lazima kuchafuka,
Ndiyo wanayoyataka, hawawezi kugeuka,
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !
 
Ahadi ilishawekwa, muda unasubirika,
Siku yao kuja fika, wavune waliyotaka,
Na si mkosa Rabuka, mamboye ni ya hakika,
Hawajali takataka, vipi  wakujali wewe !