Thursday, December 13, 2012

MSHAIRI WA WANANCHI

 KUSIFU yao napwaya, vipi watanisikiya,
Hao wameshazoea, sikuzote kusifiwa,
Washairi  huwalea, uongo wakapepea,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Elimu ikapwelea, kama watoto wakawa,
Hukariri pasi jua, kauli wanazotoa,
Wakafulia sanaa, kwa kuvalishwa manyoya,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Wengi watanunuliwa, kwenda kuwatumikia,
Tenzi wakawaimbia, uongo zashehenea,
Vipimo wakatumia, usawa visivyotiwa,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Wajibu huusifia, haki inayotakiwa,
Mtu akijifanyia, na ujira akapewa,
Ni uzushi kuingia, kwalo hilo kumsifia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Mahitaji twayajua, ya msingi yaliyokuwa,
Vipi utamsifia, jukumu kuangalia?
Stahili naijua, sifa si haki kupewa,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Barabara zatakiwa, sisi sote kutumia,
Vipi tutakusifia, eti kwa kutletea?
Madaraja nayo pia, budi yakawepo pia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Madaraja nayo pia, budi yakawepo pia,
Ni kazi  kuangaliwa, hao waliopangiwa,
Marufuku kusifiwa, ikiwa hivyo nazaa,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Maji kote yatakiwa, watu wanayalilia,
Vipi wataka sifiwa, wajibu ukitimia,
Ajabu ingelikuwa, ya kwako kunyunyizia,
Madaraja nayo pia, budi yakawepo pia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Umeme unapwelea, gharama watubambikia,
Kiwizi watuibia, tayari watupunguzia,
Uniti chache zikawa, wiki kutosaidia,
Madaraja nayo pia, budi yakawepo pia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Kisha watuzungukia, zaidi kutuongzezea,
Nadhani wanatania, wafanyalo wajua,
Wameishatuzungukia, ujanja watufanzia,
Madaraja nayo pia, budi yakawepo pia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Tisini asilimia, sio waliopaiwa,
Sasa wataka kamua, kumi tuliojaliwa,
Hata mawe yanalia, uhuni kutufanyia,
Madaraja nayo pia, budi yakawepo pia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Shrika kujichungua, hivi laona udhia,
Naona mijitu yajaa, na kazi isiyokuwa,
Nchi wanaichezea, tabu tupu inakuwa,
Madaraja nayo pia, budi yakawepo pia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Hili mkilinchungua, mianya tele yajaa,
Nyufa zinazotanua, gharama kutuzidishia,
Na wakubwa wanajua, ubazazi kuamua,
Madaraja nayo pia, budi yakawepo pia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Vijiji vyasahauliwa, mijini tumehamia,
Hata waliozaliwa, sasa wanakuchukia,
Hii siachi shangaa, wapi tunaeleeka,
Madaraja nayo pia, budi yakawepo pia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Fikra tumefulia, ukubwa kuugombea,
Wajinga tulivyokuwa, haya tunayaridhia,
Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Watu wapate kukua, kiuchumi kwendelea,
Na kijamii wakawa, ustawi waujua,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Wanaojisaidia, wenyewe kuendelea,
Vionozi  hawajawa, mamluki wa kujifaa,
Yao yakishatimia, yenu hawatoangalia,
Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Wengi wanaolilia, ukubwa hili huzua,
Wataka yao kupaa, sio yenu kutatua,
Kura mkiwaachia, mwaja kesho kujutia,
Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Thamani wamepania, ya kwenu kupungua,
Sio kitu mlokuwa, kura mkishazitoa,
Huuzwa na kununuliwa, jinsi wanavyoamua,
Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Na mimi nawazindua, ili mpate kujua,
Vipi watafurahia, wapate kunitambua,
Watataka nifukia, pasiwe wa kunisikia,
Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Kifo watashangilia, na rambirambi  kutoa,
Mwehu niliyekuwa, ya wajinga kutetea,
Tena nilipungukiwa, na zaidi kukashifiwa,
Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Mola ninamuachia, malengo kusaidia,
Ukiwani kuwatoa, niwezao kuwatoa,
Kuchoka nitakataa,  hadi siku ya kiyama,
Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Ukweli wanaoua, rafiki hawatakuwa,
Ubaya kunizulia, na mengi kusingiziwa,
Imeoza Tanzania, kwa uongo kuulea,
Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Wasafi mkichagua, watakuja ligundua,
Yangu watashangilia, na ukweli kuujua,
Siku hiyo kujakuwa, nisiwe wenda ikawa,
Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

Ila nitalisikia, kaburini kuambiwa,
Moyo nikaufungua, kama ua kuchanua,
Niridhie Tanzania, nayo ikaniridhia,
Laiti tungelijua, ukubwa kutumikia,
Mshairi wa wananchi, wakubwa watanipenda ?

ASAKAYE KUSIFIWA


Kazi umejifanyia, na ujira unapewa,
Wajibu uliokuwa, wala haujatimia,
Ufanisi umevia, na ufanifu nazaa,
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Ziada hatujajua, kawaida inakuwa,
Kiasi inapingua, kwa wlaiotangulia,
Ila wakiri raia, mapambo  mwawazidia,
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Wastani wafatia, ajabu hajaibua,
Wachache waliopewa, na wengi hawajapewa,
Mizani ukitumia, pande gani yazidia?
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Saa hazijafikia, siku ya kuandikiwa,
Shinikizo unatia, ovataimu kupewa?
Mfanyakazi shangaa, weye wanakuumbua?
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Kama nguo ingekuwa, wengine wakazivaa,
Sura tu huondoa, zilezile zinakuwa,
Lakuajabikia, wallahi sijalijua,
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Mbio ingelkuwa, na wale mloanzia,
Wa mwisho mngelikuwa, zawadi mnalilia ?
Majaji watazubaa, washindwe kukuelewa,
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Riadha tunafulia, kumbe hivi inakuwa,
Tunataka zawadiwa, bila jasho kulitoa ?
Rahisi ilivyokuwa, kila mtu anuia,
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Rahisi ilivyokuwa, kutwaa bila kutoa,
Wengi wanakimbilia, nani atawasumbua,
Kazi tusingechachua, wengi wangelikimbia,
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Katiba inatakiwa, viwango kutuwekea,
Kati isipofikia, kofia ni kuwavua,
Kelele kutotupigia, stahili isokuwa,
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Kandanda twaondolewa, kisa hiki kimekuwa,
Hatujipangi muruwa, na ratiba twakataa,
Uwekezaji wavia, na motisha zafifia,
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Mazingira mwatakiwa, yote kuyaangalia,
Vipimo mkachukua, vigezo kujiwekea,
Haya mnapojitia, aibu mwajiombea,
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

Kilio mkiangua, uongo tutakijua,
Msiba wa kujitakia, jirni hukukimbia,
Nduguzo wakaachiwa, wenyewe kukufukia,
Atakaye kusifiwa, wasiwasi anitia !

KWA NYOTE MLIONIPENDA


Shukurani nazitoa, kwa wote walionipenda,
 Hisani walonigea, na maisha kunifunda,
Ingawa wamenipotea, kwangu bado ni mawanda,
Wote walionipenda, shukurani nazitoa !

Kuishi tuliokaa, tukawa pete na chanda,
Asante nawatumia,  na ningali nawapenda,
Siachi wafikiria, na dua zenu naganda,
Wote walionipenda, shukurani nazitoa !

Haziniishi ruia, kichwani zinavyotanda,
Sura ninajionea,  kama pichani zaganda,
Na sauti husikia, za vicheko vikitanda,
Wote walionipenda, shukurani nazitoa !

Maisha yalikataa, pamoja sote kuwanda,
Nasibu hatukupewa,  kwa karibu tukaranda,
Yote tumeyaachia, yalazimu kusarenda,
Wote walionipenda, shukurani nazitoa !

Umbali watuzuia, kwa miaka nazo nyanda,
Mikanda imebakia, kula  bada na mlenda,
Na Unguja yamedanda, ya urojo kuusunda,
Wote walionipenda, shukurani nazitoa !

HIVI SASA ASINZIA


Kitu hajakiongea, naona anikoromea,
Hakuna cha kuambua, ila gia za kukataa,
Masikio yaumia, pumziko latakiwa,
Hivi sasa asinzia, mimi naenda kulala!

Wakataa makataa, utumwa kununuliwa,
Viroja wavihofia, na njia wasizojua,
Mafagio wanunua, barabara kufagia,
Hivi sasa asinzia, mimi naenda kulala!

Weupe waliokuwa, kichwani  wameishiwa,
Wabaki kushangilia, hawajui ya kuzua,
Siku ikijawadaia, wasiache kuzubaa,
Hivi sasa asinzia, mimi naenda kulala!

Hili halijawa ngekewa, ni mtego mwategewa,
Nao wanaosinzia, ndoano mmepatiwa,
Na nyavu zinawajia, wapate wengi kuvua,
Hivi sasa asinzia, mimi naenda kulala!

Mnafiki angalia, alama zimemjaa,
Kweli wongo kwake huwa, na ahadi hufulia,
Mwingi wa kuiisifia, hata akitindikiwa,
Hivi sasa asinzia, mimi naenda kulala!

Ishara ukizjua, yake utayaelewa,
Si muhali kujinasua, bora ukaangalia,
Sio rahisi dunia, miteremko ikawa,
Hivi sasa asinzia, mimi naenda kulala!

Hapa ninamalizia, kesho kutoihofia,
Yumkini kukimbia, hakika usiyojua,
Yakini kupalilia, bora litakalokuwa,
Hivi sasa asinzia, mimi naenda kulala!

HAO NDIO HAO HAO


HUJIFANZA Sio wao, lakini ni hao hao,
Kazi ni kupiga mwao,  na ukora wa vilio,
Kelele mtindo wao, kuepa ni kazi yao,
Ya jibwa mbweka wowowo, hao ndio hao hao!

Hufatwa paka miyao, kila akilia taoo,
Wakenda nazo chepuo, vita visivyo na ngao,
Mazoezi mazomeo, na dharau za ng'oo,
Ya jibwa mbweka wowowo, hao ndio hao hao!

Hao si kitu washikao, kuachia kazi yao,
Halisimami jambo lao, ila kwa nguzo za teo,
Yakishafika machweo, ndio macho wafungao,
Ya jibwa mbweka wowowo, hao ndio hao hao!
Haviishi vipepeo, kufukuza harufuyo,
Vigelegele vimeo, ndivyo wavitumiao,
Ni washindwa washindao, na madhambi wavunao,
Ya jibwa mbweka wowowo, hao ndio hao hao!

Ni milango wafungao, yao si tusikiayo,
Akili nje waachao, utupu ndani uwao,
Ni ni walewayo, isipokuwa uchoyo,
Ya jibwa mbweka wowowo, hao ndio hao hao!

Si watu wajengao, huwa ni wabomoao,
Sio paa wawekao, ila ndio waezuwao,
Maji yao kwenye ndoo, umaskini ngao yao,
Ya jibwa mbweka wowowo, hao ndio hao hao!

Na hili ni jaribio, pango nyoka wamtoao,
Kisicho na muelekeo, hakina matamanio,
Wasiotumia kioo, sura si waijuayo,
Ya jibwa mbweka wowowo, hao ndio hao hao!

Hii kwako kumbukumbu

 Unadhani umefika, na garini umeshuka,
Hakika umepotoka, mwishowe haujafika,
Safari ina masika, ni vuli ulikotoka,
Hii kwako kumbukumbu, safariyo haijesha!

Hii siyo ya haraka, kwa umbali yasifika,
Mwanzo wake wa marika, miaka kuhesabika,
Mwisho wake  si shaka, tamati inatoweka,
Hii kwako kumbukumbu, safariyo haijesha!

Na wanaoweweseka, hudhania wamefika,
Mikoba wakaishika, huku wataka kushuka,
Ila wakijazinduka, popote hawajafika,
Hii kwako kumbukumbu, safariyo haijesha!

Tao ukierevuka, hili halina mashaka,
Mtawa keshayandika, mtandaoni kaweka,
Ukitaka elimika, tembelea kupevuka,
Hii kwako kumbukumbu, safariyo haijesha!

M K U B W A


Kazi nimejifanzia, wajibu iliyokuwa,
Cheo nilishakipewa, ziada naikataa,
Hapa nilipofikia ukubwa kwangu hadaa,
Lipi nililolifanza, hata niitwe mkubwa!

Ukubwa kwangu hadaa, ziada isiyofaa,
Na anayenyenyekea, h ofu sana anitia,
Yuleyule nilikuwa, yuleyule nitakuwa,
Lipi nililolifanza, hata niitwe mkubwa!

LAITI NINGELIJUA


Siku nikiziringia, na miezi kufatia,
Miaka nikanuia, duniani  nitakaa,
Dakika sikuchukua, ng'ambo nimesharushiwa,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Laiti ningelijua, nisingetia udhia,
Roho safi ningekuwa, kila mtu kumwangalia,
Wema ningeunuia, watu wote kugawia,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Huruma ningeilea, mayatima kuwalea,
Kama wana wangekuwa, kwa mapenzi kuyanoa,
Ukiwa wasingejua, kama wangu wangekuwa,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Fakiri wasingekuwa, wale ninaowajua,
Zaka ngeliwagawia, umaskini kuutoa,
Kisha kuwasaidia, hadi yao yakakua,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Ya dini ningeyajua, yake nikapalilia,
Tajiwidi kunuia, mengine nikahofia,
Imani ingenijaa, sio mambo ya ruia,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Ujana ningetumia, kwa wengine kuwafaa,
Dini ningejisomea, kihiyo nisingekuwa,
Kiarabu ningejua, na hija nisingeachia,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Umri ningeutumia, ibada kujifanzia,
Anasa ningekimbia, pamwe kujitangazia,
Yangu ningeangalia, sabilllahi yakawa,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Mali nisingeichezea, kwa fujo kuitumia,
Anisi kusainia, na ukafiri kufaa,
Haki ningepigania, wanyonge kusaidia,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Elimu ningeitumia, kwa wengine kugawia,
Mwisho nisingefikia, milango mingi kwingia,
Hadi China kuingia, yao nikajisomea,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Afya isingenifaa, pasina wengi kufaa,
Yao nikaangalia, hadi siha wakajawa,
Hapo ningeliridhia, laiti ningelijua,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

LIPI NILILOFANZA

Ukubwa wa kujipuliza, kama mwana na kondomu,
Huu ninaupuuza, hauwezi kwangu dumu,
Ni ajizi ya ajuza, mabinti kuwa hirimu,
Lipi nililolifanza, hata niitwe mkubwa!

Ni muhali sintoweza, moyo hautojihimu,
Ningekuwa Mwanaweza, ningekuwa binadamu?
Bei sijajiagiza, nisije kushushuliwa,
Lipi nililolifanza, hata niitwe mkubwa!

Wala yangu si ya pweza, mikono kujikirimu,
Naiona miujiza, na mie siifahamu,
Nafanza ninachoweza, mengine yake Karimu,
Lipi nililolifanza, hata niitwe mkubwa!

Watu sitaki kuteza, na kisha kuwadhulumu,
Mwili wangu nautuza, uhai na marehemu,
Nikawaponza mafunza,  yangu wasiwe na hamu,
Lipi nililolifanza, hata niitwe mkubwa!

Ninakuomba Muweza, unyonge unikitimu,
Nizuie kujikweza, mahala nisipodumu,
Ngazi yangu kuongeza, mbele ya umarehemu,
Lipi nililolifanza, hata niitwe mkubwa!


Sijaiona thamni


YUMKINI siioni, ya kunitukuza shani,
Matamanio nahini, naijua tathmini,
Utawa sijabaini, na uwalii sidhani,
Sijaiona thamni, niringie kitu gani!

Naitafuta thamani, kutoka kwa aliinsani,
Waniweke kundi gani, ubinadamu kuwini,
Kisha kwa hatua gani, uishapo uzaini,
Sijaiona thamni, niringie kitu gani!

Naitafuta imani, pasina ya usononi,
Aidha pia amani, pasina huu utani,
Na umoja kuauni. kwa wakweli wumini,
Sijaiona thamni, niringie kitu gani!

I chini yangu mizani, najiona bado duni,
Dhalili ni mashakani, na dhaifu akilini,
Ubora sijabaini, ningalipo kichakani,
Sijaiona thamni, niringie kitu gani!

Haki sijaithamini, nikaitia moyoni,
Nguli wananirubuni, kuwaatia zaini,
Nawahofia Kaini, waliopo duniani,
Sijaiona thamni, niringie kitu gani!

Kwa ukweli mhaini, na siasa wadhamni,
Nikiitia moyoni, waitoa akilini,
Nabebeshwa mkononi, kisicho nayo thamani,
Sijaiona thamni, niringie kitu gani!

Wako wapi wenye shani, yangu wakayadhamini,
Nikimbie nukstani, na kujihini moyoni,
Nikaipata amani, akilini na rohoni?
Sijaiona thamni, niringie kitu gani!

Rabana wewe rubani, tena wa juu angani,
Anga zako hawaoni, wanaishia pembezoni,
Niwe wako aliamini, unisafishe moyoni,
Sijaiona thamni, niringie kitu gani!

Dharau siichukii

 JUU walishanzia, thamani wakanitoa,
Wageni wakiingia, sithaminiwi wajua,
Wao kinachafia, aitivii inakuwa,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Hadhi sijathaminiwa, na hali waichimbua,
Heri wamejigawia, makiwa kunigawia,
Hawapo kuninyanyua, ila kunishindilia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Yao wanafatilia, kwa karibu kwangalia,
Doti wanaitambua, hadi nukta kulea,
Hawawezi kuachia, cha kwao kikapotea,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Vya wengine hubeua, udhalili kuvitia,
Kisha wakavitifua, kama wasipotumia,
Yatima kumuibia, kisha utumwa kumtia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Jadi yangu kufulia, wengine kusaidia,
Ni jiwe kukanyagia, ng'ambo kwenda kuvukia,
Heshimake naijua, kingine sintolilia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Sawa wote tungekuwa, isingekalika dunia,
Kipawa ukijaliwa, si wote watapewa,
Wewe unayoyajua, vipi wao kuyajua,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Leo hii waijua, ghaibu wameshafulia,
Hapa ndipo hudhania, huwa mwanzo kuishia,
Wewe unalielewa, maisha yaendelea,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Ni hatua kupitia, mwisho hatujafikia,
Wengi inawazudua, wakadhani wametua,
Kisha wakajifanyia, ya dhuluma na izaya,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Yarabi nakusifia, mjua mwenye kujua,
Macho umenifungua, kuiona yangu njia,
Zaidi sintolilia, ila kuniangalia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Dharau siichukii

 JUU walishanzia, thamani wakanitoa,
Wageni wakiingia, sithaminiwi wajua,
Wao kinachafia, aitivii inakuwa,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Hadhi sijathaminiwa, na hali waichimbua,
Heri wamejigawia, makiwa kunigawia,
Hawapo kuninyanyua, ila kunishindilia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Yao wanafatilia, kwa karibu kwangalia,
Doti wanaitambua, hadi nukta kulea,
Hawawezi kuachia, cha kwao kikapotea,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Vya wengine hubeua, udhalili kuvitia,
Kisha wakavitifua, kama wasipotumia,
Yatima kumuibia, kisha utumwa kumtia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Jadi yangu kufulia, wengine kusaidia,
Ni jiwe kukanyagia, ng'ambo kwenda kuvukia,
Heshimake naijua, kingine sintolilia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Sawa wote tungekuwa, isingekalika dunia,
Kipawa ukijaliwa, si wote watapewa,
Wewe unayoyajua, vipi wao kuyajua,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Leo hii waijua, ghaibu wameshafulia,
Hapa ndipo hudhania, huwa mwanzo kuishia,
Wewe unalielewa, maisha yaendelea,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Ni hatua kupitia, mwisho hatujafikia,
Wengi inawazudua, wakadhani wametua,
Kisha wakajifanyia, ya dhuluma na izaya,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

Yarabi nakusifia, mjua mwenye kujua,
Macho umenifungua, kuiona yangu njia,
Zaidi sintolilia, ila kuniangalia,
Dharau siichukii, mzawa sinayo  hadhi!

k u p a l i l i a


ZA dini zilizokuwa, na ukabila kutia,
Kwao kupalilia, magugu kwetu kwotea,
Tunashindwa kwelewa, nini chapaliliwa ?
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Siri hatujaijua, sinema twajionea,
Wahariri wakatia, kurasa isotakiwa,
Na tivii kutumia, na haja pasipokuwa,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Papi pasipougua, kwetu hapa Tanzania,
Kumoja kukatibiwa, na kwingine kuchiwa,
Kadari kama ikiwa, hilo basi naridhia,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Ila ninayoyajua, cheo si kupendelea,
Kwenu ukawajengea, wengine wakafulia,
Neema ukaigawa, jinsi unavyojisikia,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Imani ukazigawa, hawa ukasaidia,
Wengine ukawaambaa, na ya kwao kupuuzia,
Mioyo hufa hisia, na upendo kupotea,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Mbegu mlizochukua, ardhi yazikataa,
Mkilazamisha wakiwa, wanawenu kuja kuwa,
Hili msipolijua, mtakuja kushangaa,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Hadithi zasimuliwa, wanafiki kuwajua,
Ahadi zao nazaa, kweli haitatokea,
Naye akiaminiwa, usadiki hatojua,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Na mijini wamejaa, sasa wayaogelea,
Kawaida kufulia, pasi wakaingojea,
Bila ya maji kutia, na moto umekolea,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!

Kijijini natulia, moyo wangu kuufua,
Kwaniridhi, naridhia, nakuona maridhia,
Hakika hii ni njia, pepo katika dunia,
Ni nini lapaliliwa, harambee za mnafiki!


KUNG'ARA KWENYE TIVII

 BIASHARA wamezua, sura kuziangazia,
Tivii wazinunua, ya kwao kutangaziwa,
Hata ushuzi ukiwa, mradi una rupia,
Kung'ara kwenye tivii, siri ya mafanikio?

Bishara zinatukia, hadhi sasa zinapewa,
Ukubwa kutangaziwa, pasina ya kusinzia,
Kama hukutangaziwa, kujitangaza amua,
Kung'ara kwenye jarida, siri ya mafanikio?

Kwenye habari kivia, na lako huwa lavia,
Wapaswa twaa hatua, usikose angaziwa,
Hata kama kulipia, utaja kurejeshewa,
Kung'ara kwenye tovuti, siri ya mafanikio?

Cheo ukikichukua, gharama ndogo ikawa,
Kwingi utakukwambua, hata mawe nayo pia,
Hubinywa damu kutoa, kwa dawa ukatumia,
Kung'ara kwenye tivii, siri ya mafanikio?

Shani imetufikia, ya mazuri kutononoa,
Na sauti kusikiwa, hata na wenye mafua,
Vigugumizi wakawa, kwenye vyombo ni fasaha,
Kung'ara kwenye jarida, siri ya mafanikio?

Uchumi wa zawadiwa, bila ya kutumikia,
Enzie zimefikia, wajuao watambua,
Jasho wanaolitoa, papo hapo hubakia,
Kung'ara kwenye tovuti, siri ya mafanikio?

Kizungumkuti kikawa, dhihaka kupaliliwa,
Nami hilo nimeng'amua, ang'arae atumiwa,
Mishipi washilkilia, mwanasesere akawa,
Kung'ara kwenye tivii, siri ya mafanikio?

Itihari hatakuwa, kaziye kutumikia,
Hufanza la kuambiwa, hutumwa kutumikia,
Nchi atawauzia, bila ya kuulizia,
Kung'ara kwenye jarida, siri ya mafanikio?

Ni nani asiyejua, hadhihi ya kuambiwa,
Huyo wa kukimbilia, kitu gani afatia,
Nini aenda fichua, au ulinzi kutoa ?
Kung'ara kwenye tovuti, siri ya mafanikio?

U R I T H I


BABA anamhofia, ataiaga dunia,
Naye anajiandaa, urithi kuuchukua,
Fursa azichambua, pahali pema kukaa,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Kisa nimehadithiwa, mizungu kilichotiwa,
Ngano ya kuenguliwa, toka tambo za dunia,
Inayotia fadhaa, na  hamasa kupungua,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Kumbe nilivyoyajua, sivyo yalivyotokea,
Kielelezo si dawa, zaidi walichengua,
Ndani wakayafikia, mimi nisiyoyajua,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Fadhaa yawaumbua, neno hili kusikia,
Uraibu umekuwa, pombe waisiyoelewa,
Mlevi sasa kichaa, kila mtu abambua,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Kumbe laini kikiwa, ugumu ndani hulea,
KIla kinachong'aa, hakiachi kufubaa,
Navyo vinavyovutia, mvuto huja kwiishiwa,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Rai niliitengua, haikuwa ya raia,
Mwenzi aliyezidiwa, wala hakuwa mzawa,
Mwana aliyejitia, hakuwa Mtanzania?
Si mshairi wa chama, na wala haitakuwa !
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Watumwa waliokuwa, danguroni wamekaa,
Nta sasa wazaa, na mnato kuutia,
Mzinga kupalilia, kuvuna ya ushujaa?
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?

Hatua wasiotwaa, aibu wanatutia,
Umma wahofu ubia, walikwishauandaa,
Wafanzao wayahua, na kwetu sisi hadaa,
Ukubwa aulilia, kurithi mali za chama ?


Lenu langu litakuwa


Wanyonge wanapokuwa, na mimi nitaingia,
Lao nikalichukua, mpka langu likawa,
Ndicho nilichoumbiwa, musrati kufwatia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Sikuumbiwa dunia, njii hii napitia,
Lengo nimejiwekea, uangavu kufikia,
Kuona msiyojua, wala kuyafikiria,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Hili si la kuombewa, ni tunu ikijaliwa,
Mimi nalifurahia, kuishi naaazimia,
Msongo kwangu likawa, shinikizo kunitia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Maisha nakadiria, taishi kutumikia,
Vingine naviachia, hili kwake nahamaia,
Nikaanzisha ubia, milele kuendela,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Inshallah naitia, siachi kukumbukia,
Neema najiombea, na kinga nikapatiwa,
Akitacho Jalia, na hakika ndilo huwa,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Hili ninalielewa, vingine sijafikiria,
Nafuai nimeitoa, ruksa sijajaliwa,
Yeye ndiye huamua, mimi wa kufatilia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Nia akibarikia, lake ndilo hutimia,
Mimi atanitumia, abdi niliyekuwa,
Lake nikaitikia, na kazi kumfanzia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Muhula akinigea, vyema kutumikia,
Hadi nitapofikia, wengine wakachukua,
Yake akaniridhia, na mimi kumridhia,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Akhiri amesikia, yangu atayaridhia,
Nakili lililokuwa, uwakili sijapewa,
Ila kushuhudia, kwa lile ninalojua,
Ya kwangu kufanikiwa, lenu langu kujakuwa!

Makombora yanarudi

 YATUPWA kuhilikia, safu wakazipangua,
Asubhi kiingia, mipango wanajipangia,
Jioni ikiishia, tathmini hutolewa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hadithi kuendelea, hurushwa yakarejea,
Mwamvuli wahofia, mlengwa anatumia,
Uyahudi wangejua, huyo wangemnunua,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Wabaki kusingizia, adui kawarushia,
Kumbe ilivyokuwa, yenyewe yajirudia,
Siri hawajaijua, wanazidi kuumia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Aliko hawajajua, nasibu waitumia,
Kapelekewa hidaya, wala hazikupokelewa,
Wadhani ana  kinaya, hayajali ya dunia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Ganzi limeshaingia, ovoovyo yarushiwa,
Lengo sijalitambua, wala pia yake nia,
Hadhira inashangaa, kitali kinavyokuwa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Na mimi najiachia, mlinzi atanifaa,
Kadari sijaijua, pengine hii ndo njia,
Wito nilishaitikia, hutoweza kunitoa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hili sikuigilizia, starehe naijua,
Tena ninafurahia, kulikosa si ridhaa,
Wanyonge ni yangu bia, hunywa hadi nikalewa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hayanipiti masaa, bila kuwaulizia,
Hali zao kuzijua, na nini wapungukiwa,
Sinacho nitakitoa, kukopa nilichopwa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Mkononi huachia, mtupu nikabakia,
Hali nikiangalia, h aziwezi fanania,
Ila raha naijua, wala siwezi kulia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Nderemo inapokuwa, peponi hujisikia,
Na kilio wakilia, ninauvaa ukiwa,
Yao niemshakusudia, ya kwangu budi yakawa,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Laiti mngelijua, kusita isingekuwa,
katika hii dunia, uongozi ni kufaa,
Uongozi wa kubwia, na starehe karaha,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Hesabu nishahisabia, wa sikio, kusikia,
Ulimi sikuachia, ila kwa kujizuia,
Lengo nalitarajia, Mwenyezi atajalia,
Makombora yanarudi, kule yalikotokea !

Z I M A M O T O


PAPO kwa papo kuamua, pasi kuwa na bajeti,
Sifa za kuserubukia, shukrani kuambua,
Watu wakasujudia, na viatu kurambia,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Hayo ya kujinyanyua, walipokwishagukia,
Wakaondoa udhia, matope kwenda ondoa,
Huruma wakajiuzia, kwenye njaa na ukiwa,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Mamlaka kuyazoa, mtu ukajilimbikia,
Ukabaki kuamua, na wengine kushangaa,
Haiwi kushangilia, ubaya ukitiokea,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Nchi inayo mikoa, kama nchi ilokuwa,
Uhuru isipopewa, nchi tutaichezea,
Mbali hatuafikia, tutaanza kupagawa,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Inatakiwa mikoa, mipango yao kuzua,
Na uongozi ridhaa, wenyewe kujichagua,
Hatua wakajipangia, wapi wataka fikia,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Dar  wakingojea, yao kuja kuamua,
Mikoa itafubaa, na riadha kufulia,
Mbali hawatafikia, kuchekwa iwe tabia,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Uchumi kuunyanyua, wakazi wanatakiwa,
Yao wakayamua, na ulua kuutia,
Kadiri wakaagua, wawezavo jinasua,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !

Nasaha nimeitoa, naomba hoja kutoa,
Manani akajalia, upevu kuufikia,
Nchi ni kubwa gunia, sio rahisi kujaa,
Nchi yanaiyumbisha, maamuzi ZIMAMOTO !