Thursday, December 13, 2012

LAITI NINGELIJUA


Siku nikiziringia, na miezi kufatia,
Miaka nikanuia, duniani  nitakaa,
Dakika sikuchukua, ng'ambo nimesharushiwa,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Laiti ningelijua, nisingetia udhia,
Roho safi ningekuwa, kila mtu kumwangalia,
Wema ningeunuia, watu wote kugawia,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Huruma ningeilea, mayatima kuwalea,
Kama wana wangekuwa, kwa mapenzi kuyanoa,
Ukiwa wasingejua, kama wangu wangekuwa,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Fakiri wasingekuwa, wale ninaowajua,
Zaka ngeliwagawia, umaskini kuutoa,
Kisha kuwasaidia, hadi yao yakakua,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Ya dini ningeyajua, yake nikapalilia,
Tajiwidi kunuia, mengine nikahofia,
Imani ingenijaa, sio mambo ya ruia,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Ujana ningetumia, kwa wengine kuwafaa,
Dini ningejisomea, kihiyo nisingekuwa,
Kiarabu ningejua, na hija nisingeachia,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Umri ningeutumia, ibada kujifanzia,
Anasa ningekimbia, pamwe kujitangazia,
Yangu ningeangalia, sabilllahi yakawa,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Mali nisingeichezea, kwa fujo kuitumia,
Anisi kusainia, na ukafiri kufaa,
Haki ningepigania, wanyonge kusaidia,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Elimu ningeitumia, kwa wengine kugawia,
Mwisho nisingefikia, milango mingi kwingia,
Hadi China kuingia, yao nikajisomea,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

Afya isingenifaa, pasina wengi kufaa,
Yao nikaangalia, hadi siha wakajawa,
Hapo ningeliridhia, laiti ningelijua,
Laiti ningelijua, kuishi kumbe masaa !

No comments: