Shukurani nazitoa, kwa wote walionipenda,
Hisani walonigea, na maisha kunifunda,
Ingawa wamenipotea, kwangu bado ni mawanda,
Wote walionipenda, shukurani nazitoa !
Kuishi tuliokaa, tukawa pete na chanda,
Asante nawatumia, na ningali nawapenda,
Siachi wafikiria, na dua zenu naganda,
Wote walionipenda, shukurani nazitoa !
Haziniishi ruia, kichwani zinavyotanda,
Sura ninajionea, kama pichani zaganda,
Na sauti husikia, za vicheko vikitanda,
Wote walionipenda, shukurani nazitoa !
Maisha yalikataa, pamoja sote kuwanda,
Nasibu hatukupewa, kwa karibu tukaranda,
Yote tumeyaachia, yalazimu kusarenda,
Wote walionipenda, shukurani nazitoa !
Umbali watuzuia, kwa miaka nazo nyanda,
Mikanda imebakia, kula bada na mlenda,
Na Unguja yamedanda, ya urojo kuusunda,
Wote walionipenda, shukurani nazitoa !
No comments:
Post a Comment