Thursday, January 31, 2013

Binti wa Kimarekani


Machoye ya samawati, na nywele ni za dhahabu,

Kanipiga kwa manati, hadi nimekuwa bubu,

Sumakuye haisiti, yavuta kama kulabu,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Kanimaliza binati, hali yangu taabani,

Ninakuwa kama chizi, kama yeye simuoni,

Chini siwezi kuketi, hadi nimtie machoni,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Kwangu kawa kama kiti,  mkweizi wa maruwani,

Simhofu afriti, yeye kinga wa imani,

Nafsi aidhibiti, kingine sikitamani,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Napenda hostelini, avipangavyo vya ndani,

Kwangu ikawa ni shani, kama vile bustani,

Na harufu utadhani, anacuhoma ubani,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Ninampenda kichwani, nywele akizibaini,

Zinazokuja usoni, akarudisha uwani,

Kisha akawa makini, kuteta anachoamini,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Napenda mgahawani, kwa anavyojiamini,

Mkiwa mazungumzoni, watu wakamuamini,

Alama wakazighani, ugavana atawini,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Nampenda darasani, kwa kuwa ni namba wani,

Asiyejali ya nani, akikaa ubavuni,

Hazihofu shotigani, na sheria mkononi,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Mwana huyu mahluti, weusi sio yakini,

Na weupe si wa dhati, unaishia njiani,

Utadhani kalkiti, nyweleze kwa ulaini,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Macho yake ya kijani, huionyesha hisani,

Yakilegea laini, kama nyepesi  jibini,

Akilia hujilani, kwa nini umemuhini,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya

 

Sautiye ya puani, hukutoa mashakani,

Kuisikia ya thamani, ni muziki wenye shani,

Hauuchoki yakini ,kuisikia  hewani,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya

 

Jina lake Carolyn, anatokea Brooklyn,

Amenipa anwani, nimtafute mjini,

Nikiwasili mwakani, kuiona Marekani,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya

Binti wa Kimarekani


 

Machoye ya samawati, na nywele ni za dhahabu,

Kanipiga kwa manati, hadi nimekuwa bubu,

Sumakuye haisiti, yavuta kama kulabu,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Kanimaliza binati, hali yangu taabani,

Ninakuwa kama chizi, kama yeye simuoni,

Chini siwezi kuketi, hadi nimtie machoni,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Kwangu kawa kama kiti,  mkweizi wa maruwani,

Simhofu afriti, yeye kinga wa imani,

Nafsi aidhibiti, kingine sikitamani,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Napenda hostelini, avipangavyo vya ndani,

Kwangu ikawa ni shani, kama vile bustani,

Na harufu utadhani, anacuhoma ubani,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Ninampenda kichwani, nywele akizibaini,

Zinazokuja usoni, akarudisha uwani,

Kisha akawa makini, kuteta anachoamini,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Napenda mgahawani, kwa anavyojiamini,

Mkiwa mazungumzoni, watu wakamuamini,

Alama wakazighani, ugavana atawini,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Nampenda darasani, kwa kuwa ni namba wani,

Asiyejali ya nani, akikaa ubavuni,

Hazihofu shotigani, na sheria mkononi,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Mwana huyu mahluti, weusi sio yakini,

Na weupe si wa dhati, unaishia njiani,

Utadhani kalkiti, nyweleze kwa ulaini,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya!

 

Macho yake ya kijani, huionyesha hisani,

Yakilegea laini, kama nyepesi  jibini,

Akilia hujilani, kwa nini umemuhini,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya

 

Sautiye ya puani, hukutoa mashakani,

Kuisikia ya thamani, ni muziki wenye shani,

Hauuchoki yakini ,kuisikia  hewani,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya

 

Jina lake Carolyn, anatokea Brooklyn,

Amenipa anwani, nimtafute mjini,

Nikiwasili mwakani, kuiona Marekani,

Binti wa Kimarekani, akili anichanganya

Mazagazaga


HAYA kinagaubaga, nasema mazagazaga,
Hauwezi kunizuga, vingine ukanitega,
Hilo litakuwa soga, vigumu mimi kumega,
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Mengine mkiyaiga, wenyewe mnajiroga,
Wenzene watia sega, nyie vitako vyagomba,
Wao wajua kutaga, nyie mwajua kuaga?
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Utadhani wakufuga, wakakuvalia njuga,
Kisha kutabananga, kwa teule nazo soga,
Mwana bin kuvuruga, mzaliwa rugaruga,
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Toka lini naye Mchagga, akawa ndonya atoga,
Mmakonde kutobiringa, na mbega akaiswaga,
Watu wasimwite mwanga, na kelele kuzipiga,
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Iga we mwana wa kuiga, tembo hufa kwa kiboga,
Ukitingisha mabega,hio wala si kuringa,
Na kila lenye kunoga, wahuni hulivuruga,         
Enzi zao Viburugwa, washamba kwenda kukoga,
Manyanga weshayabwaga, wabakia kujizuga,
Ngebe ikiwa ngariba, yataishia ujuba,           
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Maisha sasa kusagwa, na vijinga vya ujinga,
Nasaba zake kuiga, na tambo za kujiganga,
Husuda kumbe hufugwa, wasiotaga, kutaga,
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Msiba hujavuruga, yaliyopangwa kubwaga,
Mzaramo na mafiga, ngomaye haiitwi mbega,
Kuzika haiwi kinga, ya umbali kuchabanga,
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Mwanamme kama mwoga, mke kinyonga humwiga,
Rangi akazikoroga, mazingira kuenga,
Maisha yenye kuvunga, mwishowe huwa kupenga,
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Mwanamme bila nanga, chombowe hakina anga,
Kokote chaweza tinga, na ghubani kikazinga,
Kiumbe mwenye kuringa, kifafa humcharanga,
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Maleenga ukimtenga, adili unazitwanga,
Na akili kuzinyonga, ukauenzi ujinga,
Kiuno pasina shanga, huwa chaisha uchanga?
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Walinikoga Mapinga, shabaha walizolenga,
Kinachowapiga chenga, mitihani kuwaganga,
Mshairi ninalonga, hamba halianisonga,
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
Yangu mkiyapinga, yatakuja kujipganga,
Yakachanua kianga, na sambamba kuviringa,
Duara ikijatinga, na rohoni kuviringa,
Mamboyo mazagazaga, hebu acha kunikoga.
 
 

Amfichiaye mwizi



LIMEZUKA jinamizi, ardhi haiwahifadhi,

Wauliza waulizi, utadhania bazazi,

Maswali yao yaudhi, yashika kwenye mizizi,

Amfichiaye mwizi, hivi naye sio mwizi?

 

Lingine hawaulizi, wauliza ufichizi,

Mhifadhi vya waizi, hivi naye sio mwizi?

Wauma vichwa wajuzi, jibule hawaliwezi,

Amfichiaye mwizi, hivi naye sio mwizi?

 

Kikali kigugumizi, meno yakauma fizi,

Na tabasamu la ndizi, linageuka kiazi,

Wakawateta wakwezi, pia na wapiga mbizi,

Amfichiaye mwizi, hivi naye sio mwizi?

 

Wawapaa usingizi, vitanda hawaviwezi,

Tivii zawa machizi, kwa kugoma ving'amuzi,

Hakuna kilo azizi, tuhuma haziwalazi,

Amfichiaye mwizi, hivi naye sio mwizi?

 

Vinara wa mafichizi, na gwiji wa ufukizi,

Mbio wanazidarizi, kuyageuza Uswizi,

Na huku zatamba radhi, za wanyonge kwa walozi,

Amfichiaye mwizi, hivi naye sio mwizi?

 

Yamegota mapinduzi, pamebaki siyawezi,

Na ziada vidokozi, kama nusu jambawazi,

Yaliyojiri majuzi, ndio kisa manukuzi,

Amfichiaye mwizi, hivi naye sio mwizi?

 

Hapanao ugunduzi, uhujumu uko wazi,

Sahani sio saizi, unazidi upotezi,

Watumia nne nazi, hali moja inakidhi?

Amfichiaye mwizi, hivi naye sio mwizi?

 

Yanawafika wazazi, wa ufu utandawazi,

Kwa kujifanya wajuzi, wa kuyachoma mandazi,

Kukaanga hawawezi, jadi yao haifunzi,

Amfichiaye mwizi, hivi naye sio mwizi?

 

Wamuhofuo Mwenyezi, dalili zake ni wazi,

Mbingu na yote ardhi, kaifanzia malezi,

Ayafanyaye maudhi, haipati yake radhi,

Amfichiaye mwizi, hivi naye sio mwizi?

 

Mwanamme wa uongo


Wa uongo mwanamme, asiliye ufisadi,

Huutaliki udume, imani akaritadi,

Akabakia mahame, na maghofu ya fuadi,

Mwanamme wa uongo, ufisadi asiliye!

 

Mwiliwe ndiyo kaziye, na moyowe maabadi,

Sio aridhikaye, daima ana nakidi,

Kesho si afikiriaye, wala si mtunza ahadi,

Mwanamme wa uongo, ibada yake ni ngono!

 

Mme huyu wa nazaa, asiliye kukaidi,

Kila siku hungojea, anapoliwa na Idi,

Siye mwenye kutulia,  asili kutaradadi,

 

Wanaozuka janibu, ujira wao zawadi,

Na wnaokuwa ghaibu, jivu lao makusudi,

Hadhara huja kujibu, ipayukapo mihadi,

Mwanamme wa uongo, ufisadi asiliye!

 

Huipamia nasibu, wakaona ni juhudi,

Wakaiweka kwa ghibu, yasiyokuwa ni sudi,

Na mitende ya adhabu, ikaja kuwafaidi,

Mwanamme wa uongo, ibada yake ni ngono!

 

Hana muda kwangalia, mateso waogeleao,

Kiburi chake hukwea, kuitani taabu zao,

Hali kwa asilimia, ni ndani ya uwezo wao,

Mwanamme wa uongo, ufisadi asiliye!

 

Kila wanachokigusa, budi kuvuta nuksi,

Kila wanachokinusa, hutapakaa mikosi,

Wadudi kutomtakasa, wote wakawa kamasi,

Mwanamme wa uongo, ibada yake ni ngono!

 

Huja wakanyofolewa, kwenye uongo wazua,

Roho kwenda kutupiwa, Bahari tusizojua,

Mfu wakabakia, huku washughulikiwa,

Mwanamme wa uongo, ufisadi asiliye!

 

Jabari kumwelekea, zitapungua balaa,

Vingine tutapokuwa, tutazidi kuumia,

Fursa ameshaitoa, tawba kuililia,

Mwanamme wa uongo, ibada yake ni ngono!

 

Tuesday, January 29, 2013

Hanky -yo, bado ninayo


CHA mkonokitambaa, machozi ulofutia,

Mimi nilikichukua, na sasa nakitumia,

Machozi kujiuftia, kwa wewe kuondokewa,

Hanky -yo, bado ninayo, najifutia machozi!

 

Marashiyo yanukia, kama vile yanalia,

Na poda uliyotia, kikohozi yanitia,

Kila nikijiwazia, kosa langu sijajua,

Hanky -yo, bado ninayo, najifutia machozi!

 

Ufukara nakisia, waweza ukachangia,

Njaa ninayonukia, rahisi kuifichua,

Wewe ulipogundua, hukuweza vumilia,

Hanky -yo, bado ninayo, najifutia machozi!

 

Kwaheri hukuitoa, wala kunisimbulia,

Njia uliichagua, ifaayo kufatia,

Upweke kuniachia, mwenye nacho kujaliwa,

Hanky -yo, bado ninayo, najifutia machozi!

 

Ila ninachokijua, langu kweli lilikuwa,

Mizanini ungetia, zana ingelizubaa,

Kwa upande kuzidiwa, hadi chini kugotea,

Hanky -yo, bado ninayo, najifutia machozi!

 

Moyo nilikuachia, upate kupalilia,

Bustani kuchanua, mengine yangefatia,

Haraka uliyokuwa, hukuweza jizuia,

Hanky -yo, bado ninayo, najifutia machozi!

 

Kuishi ulihilakiwa, mapema kutangulia,

Fisadi kumkimbilia, idadi asiyewajua,

Silaani, ninakwambia, hilo utalijutia,

Hanky -yo, bado ninayo, najifutia machozi!

 

Ya kweli umeachia, ukafata ya kuzua,

Yaliyojaa sanaa, ukweli zisizokuwa,

Laiti ningelijua, nisingelikuangalia,

Hanky -yo, bado ninayo, najifutia machozi!

 

Laiti ningelijua, nisingelikuangalia,

Machowe yalolegea, ukawa wanilogea,

Nami sikujitambua, na ukweli kuujua,

Hanky -yo, bado ninayo, najifutia machozi!

DNA Gaidi


HUYU mkubwa gaidi, lazima kumwangamiza,

Atufanyia ukaidi, ndoa zetu kuziponza,

Ili yeye afaida, asichokipandikiza,

DNA gaidi, anapaswa kuuawa!

 

Marikani kamkodi, kuja kutukengeuza,

Kama vichaa twanadi, dokta tutamueleza,

Yamekuwa maabudi, twasali bila tawaza,

DNA gaidi, anapaswa kuuawa!

 

Wenza wapanda midadi, watoto kuwakataa,

Wenye sura za kifodi, uzuri unawakwaza,

Na Jaluo wananadi, weupe kwao muujiza,

DNA gaidi, anapaswa kuuawa!

 

Walala kifudifudi, malengo kuyapoteza,

Uchawi huu wa lodi, mweusi hatauweza,

Ni mkubwa ugaidi, Mzungu tu atauweza,

DNA gaidi, anapaswa kuuawa!

 

Yakija bila magadi, waweza kuyapuuza,

lla halina ahadi, lenyewe linajitweza,

Huzuzuka likibidi, maneno likateleza,

DNA gaidi, anapaswa kuuawa!

 

Kamtazame Daudi,  jinsi anavyowaza,

Imani imekaidi, na hisia zamponza,

Anajiona kafidi, dharau inamkwaza,

DNA gaidi, anapaswa kuuawa!

 

Gaidi kwa umaridadi, ulimbo auuguza,

Watu wasipojirudi, nyumba hatutaziweza,

Ikajapaa idadi, za wazazi wa pwekeza,

DNA gaidi, anapaswa kuuawa!

 

Kesi hii murtadi, yenyewe yajieleza,

Haitaki mashahidi, hakuna wa kuibeza,

Inajiona shadidi, kila kazi yatimiza,

DNA gaidi, anapaswa kuuawa!

 

Imezishusha gredi, ndoa zilizo aziza,

Watu walizokindadi, na wana wa miujiza,

Hadimu kuwa hadidi, dunia yajitangaza,

DNA gaidi, anapaswa kuuawa!

 

Zinayoyomea sudi, za uzazi uso viza,

Wachafuka ukuwadi, na wana wa kuagiza,

Atunusuru Wadudi, huko mbele kuna giza,

DNA gaidi, anapaswa kuuawa!

Monday, January 28, 2013

NDUGU WANAPOGOMBANA...


YAO kutoingilia, ni busara inakuwa,

Katika hii dunia, ndugu ni kuwaachia,

Yao wanayatambua, kwa dira na historia,

Ndugu wanapogombana, chukua jembe kalime!

 

Huna la kukadiria, katikati kuingia,

Udhia utajiria, pamwe aibu na haya,

Ila wakishatulia, 'siache wasalimia,

Ndugu wanapopatana, chukua kapu kavune!

 

Matusi yakitembea, na magumi kutambaa,

Nyumbani kwako ingia, jembe kwenda kuchukua,

Ujihimu kwelekea, shambani kujilimia,

Ndugu wanapogombana, chukua jembe kalime!

 

Kununa kukikiishia, tabasamu wakatoa,

Wakawa wakumbatia, kile walichochukia,

Kapu wende kutungua, kivuno kitakujia,

Ndugu wanapopatana, chukua kapu kavune!

 

Ngebe zinapotambaa, na mateke kutembea,

Inuka ulipokaa, kiserema kuchukua,

Matembele kuwania, uende kupalilia,

Ndugu wanapogombana, chukua jembe kalime!

 

Kicheko wakiangua, na hafla kuisikia,

Usiache karibia, na hodi kujigongea,

Sahau ikishaingia, huwa raha na furaha,

Ndugu wanapopatana, chukua kapu kavune!

 

Mbwa wakikubwekea, mguu ukate njia,

Mlango kutouvaa, usije ukavuliwa,

Yako ukakimbilia, hadi uishe wasaa,

Ndugu wanapogombana, chukua jembe kalime!

 

Nyimbo ukizikia, kama vile wamelewa,

Milango hufunguliwa, yote wazi inakuwa,

Ndani weza kuingia,nawe upate tanua,

Ndugu wanapopatana, chukua kapu kavune!

 

Bunduki ukisikia, usiwe wachungulia,

Waweza kutunguliwa, dirishani ukikaa,

Mvunguni kiingia, usalama  wanunua,

Ndugu wanapogombana, chukua jembe kalime!

 

Sherehe zikikolea, na mapambo yakajaa,

Jua yameamuliwa, na wewe kujititimua,

Kapu kutokuachia, tupu halitarejea,

Ndugu wanapopatana, chukua kapu kavune!

U M O J A W A K I T A I F A


KAMA hujaligundua, wala siri haijawa,

Kwa tunakoelekea, uhuni wafichuliwa,

Dhahiri inaingia, watu wote kuijua,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Ukabila Tanzania, wa chama umebakia,

Na nchi kuiokoa, ni lazima kujifia,

Usawa ukaingia, nafasi kupigania,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Koo tutajazigawa, uchama kuendelea,

Na vijiji kufulia, kitu visije ambua,

Uongo tunaozua, haujengi, wabomoa,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

IJe mbele Tanzania, mengine yakafatia,

Vinginevyo tutalia, nchi tukaililia,

Tanzania, Tanzania, nchi yangu wapotea,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Wote tunajitambua, uhai unatufaa,

Wazushi wa kuzuzua, lazima kuwafichua,

Mkao wanaokaa, haunao njema nia,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Wengine wanahofiwa, shetani awatumia,

Kichwani keshaingia, mbio awafukuzia,

Ya shari kukimbilia, nchi ije angamia,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Nusura tukiijua, vyema tutawachingua,

Sababu na yao nia, ukubwa kuulilia,

Au ikulu inshakuwa, danguro la kuhamia?

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Waliojaa madoa, na hata likiwa doa,

Ushauri nautoa, ngazi budi kuachia,

Safi tunaodhania, gidamu wakachukua,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Haiwi haitakuwa, ubora wa kununua,

Halali ukajitia, na ngazi kujipandia,

Hima haitasalia, nia itakubetua,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Mapema naashiria, siri zinafichuliwa,

Mengi tusiyoyajua, mbona sasa twayajua,

Kila mwanzia ubaya, hatima huwa ubaya,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Vyama vyetu hujifia, hoja zinapopungua,

Na uchafu kununua, wengine kuwatupia,

Hadhari ninaitoa, hiyo kwetu siyo njia,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Wanasiasa mwafaa,  kuikoa Tanzania,

Nafasi mkiachia, mtakuja kuzomewa,

Umoja mngeanzia, wa vyama kupigania,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Kisha mkajichungua, bora wenu kuwajua,

Bila ya kufikiria, chama gani atokea,

Nahodha anayefaa, nchi hii kuokoa,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Mipaka mkaondoa, kwa adili kuijua,

Na safi kilichokuwa, nchi mkaipatia,

Imani zinatakiwa, kazi hii kutetea,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Twataka atayetufaa, na wala sio balaa,

Tunataka manufaa, wala si kuhofia,

Salama ya Tanzania, alo bora kuchagua,

Umoja wa kitaifa, ni vigumu kukwepeka!

 

Yamo Kwenye Mashairi...


Mengi yamehadithiwa, na mifano kutolewa,

Vipande vya historia, darasa mkajaliwa,

Ni vito vilivyokuwa, kinyesini vyafukiwa,

Yamo kwenye mashairi, ila nani anasoma ?

 

Akili waliojaa, viini wajimwagia,

Kubaini wafulia, sio waliochaguliwa,

Neema ya kubabia, huishi kuiogea,

Yamo kwenye mashairi, nani wa kutafakari ?

 

Maandishi hutokea, bali hutojisomea,

Akili zikakwambia, wewe sana unajua,

Hadi unakoelekea, njia zako kufungiwa,

Yamo kwenye mashairi, ila nani anasoma ?

 

Ulidhani wasikiwa, watu viziwi wakawa,

Ulidhani wayajua, ukakuta hayakuwa,

Bishara zikakwambia, njia umeshapotea,

Yamo kwenye mashairi, nani wa kutafakari ?

 

Zama zilizoishia, mawazo yalifukiwa,

Leo yanachimbuliwa, mengi watu wanajua,

Vitendo wakumbukia, awali vilivyokuwa,

Yamo kwenye mashairi, ila nani anasoma ?

 

Mizani waichukua, kisha wakaangalia,

Kama sawa imekuwa, au vitu imetiwa,

Kila inapopwelea, kelele utasikia,

Yamo kwenye mashairi, nani wa kutafakari ?

 

Maji yamewazidia, waogopa angamia,

Bahari nchi kavu kuwa,kwao taabu itakuwa,

Bado hawajatembea, majini wakaelea,

Yamo kwenye mashairi, ila nani anasoma ?

 

Neema zimesambaa, ja senene na mvua,

Yawashinda magunia, wapi kwingine kukaa,

Na kumbikumbi wazaa, si muda watatokea,

Yamo kwenye mashairi, nani wa kutafakari ?

 

Isije kuwa balaa, ikawa  kizaazaa,

Kasi itapopungua, mwendo rudi nyuma ukawa,

Na ari ikaishia, moshini kuyoyomea,

Yamo kwenye mashairi, ila nani anasoma ?

 

Tabia naihofia, dhrau iliyojaa,

Hoja inayonyanyapaa, bila asili kujua,

Mioyo kukangamaa, kama kaukau zikawa,

Yamo kwenye mashairi, nani wa kutafakari ?

 

Yamo Kwenye Mashairi...


Mengi yamehadithiwa, na mifano kutolewa,

Vipande vya historia, darasa mkajaliwa,

Ni vito vilivyokuwa, kinyesini vyafukiwa,

Yamo kwenye mashairi, ila nani anasoma ?

 

Akili waliojaa, viini wajimwagia,

Kubaini wafulia, sio waliochaguliwa,

Neema ya kubabia, huishi kuiogea,

Yamo kwenye mashairi, nani wa kutafakari ?

 

Maandishi hutokea, bali hutojisomea,

Akili zikakwambia, wewe sana unajua,

Hadi unakoelekea, njia zako kufungiwa,

Yamo kwenye mashairi, ila nani anasoma ?

 

Ulidhani wasikiwa, watu viziwi wakawa,

Ulidhani wayajua, ukakuta hayakuwa,

Bishara zikakwambia, njia umeshapotea,

Yamo kwenye mashairi, nani wa kutafakari ?

 

Zama zilizoishia, mawazo yalifukiwa,

Leo yanachimbuliwa, mengi watu wanajua,

Vitendo wakumbukia, awali vilivyokuwa,

Yamo kwenye mashairi, ila nani anasoma ?

 

Mizani waichukua, kisha wakaangalia,

Kama sawa imekuwa, au vitu imetiwa,

Kila inapopwelea, kelele utasikia,

Yamo kwenye mashairi, nani wa kutafakari ?

 

Maji yamewazidia, waogopa angamia,

Bahari nchi kavu kuwa,kwao taabu itakuwa,

Bado hawajatembea, majini wakaelea,

Yamo kwenye mashairi, ila nani anasoma ?

 

Neema zimesambaa, ja senene na mvua,

Yawashinda magunia, wapi kwingine kukaa,

Na kumbikumbi wazaa, si muda watatokea,

Yamo kwenye mashairi, nani wa kutafakari ?

 

Isije kuwa balaa, ikawa  kizaazaa,

Kasi itapopungua, mwendo rudi nyuma ukawa,

Na ari ikaishia, moshini kuyoyomea,

Yamo kwenye mashairi, ila nani anasoma ?

 

Tabia naihofia, dhrau iliyojaa,

Hoja inayonyanyapaa, bila asili kujua,

Mioyo kukangamaa, kama kaukau zikawa,

Yamo kwenye mashairi, nani wa kutafakari ?